1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel aitaka Ulaya kupinga wanasiasa wanaonunulika

Sekione Kitojo
19 Mei 2019

 Kansela wa  Ujerumani  Angela  Merkel amesema Jumamosi(18.05.2019) kwamba wanasiasa wa Ulaya "wanapaswa kuwapinga, wanasiasa  wa siasa kali za mrengo wa kulia" aliowataja kuwa wananunulika.

https://p.dw.com/p/3IjBz
Kroatien Merkel in Zagreb
Picha: Reuters/Str.

Hii  ni baada ya tukio la kamera iliyofichwa kumwangusha makamu kansela wa Austria Heinz-Christian Strache kuhusiana  na madai kwamba ana kubali rushwa.

Kroatien Merkel in Zagreb
Waziri mkuu wa Croatia Andrej Plenkovic (katikati) akiwa pamoja na kansela wa Ujerumani Angela Merkel (kushoto)Picha: Reuters/Str.

Wakati vyama vya siasa kali  za  mrengo wa  kulia  vimekataa maadili  kama  kuwalinda  watu waliowachache pamoja  na haki za msingi  za  binadamu , Merkel  aliwaambia  waandishi  habari  katika mji  mkuu  wa  Croatia , Zagreb , kwamba  "wanasiasa  ambao wanaweza  kununuliwa wanawajibika, na tunapaswa  kuchukua hatua  kamili dhidi  ya  yote  hayo".

Magazeti  ya  Ujerumani  ya  Der Spiegel na  Sueddeutsche Zeitung jioni  ya Ijumaa  yalichapisha vidio iliyorekodiwa, ikidaiwa kumuonesha  kiongozi  wa  chama  cha  Fredom Party (FPOe) Strache  akiahidi  mikataba  wa  serikali ili  kuweza  kupata  msaada katika  kampeni  kutoka  kwa  mfanyakazi  wa  benki bandia  kutoka Urusi.

Merkel , mwanasiasa  mwenye  uzito  katika  kundi  la  vyama  vya siasa  za  wastani  za  mrengo  wa  kulia  katika  mataifa  ya  Umoja wa  Ulaya  EPP, alikuwa  akizungumza  kabla  ya  mkutano wa chama  cha  kihafidhina  nchini  Croatia  cha  HDZ wakati kampeni za uchaguzi wa  bunge  la  Ulaya zikifikia  mwisho.

Österreich | Heinz-Christian Strache
Makamu kansela wa Austria Heinz-Christian StrachePicha: Imago Images/photonews.at

Adui wa mradi wa Ulaya

Akizungumza  kwa  ukakamavu  kabisa  katika  tukio  hilo  la kampeni, amedai kwamba "uzalendo  na  mradi  wa  Ulaya havikinzani".

"Lakini siasa za kizalendo ni adui wa  mradi  wa  Ulaya, na tunapaswa kuweka  wazi  hilo  katika  siku  za  mwisho kabla  ya  uchaguzi," ameongeza.

Kuingilia  kati  kwa  Merkel  kunafuatia  wimbi  la  miito  kutoka wanasiasa viongozi  wa  Ujerumani  kwa  wapiga  kura  kutofuata mfano  wa  nchi  jirani  kwa  kuwaweka wanasiasa  wenye misimamo wa  siasa  kali za  mrengo  wa  kulia katika  nafasi  za  madaraka.

Österreich Regierungskrise | PK Sebastian Kurz
Kansela wa Austria Sebastian KurzPicha: picture-alliance/APA/picturedesk.com/R. Schlager

Kansela  mhafidhina  wa  Austria  Sebastian Kurz amekuwa ni  mtu ambaye hajaonesha uwajibikaji kwa  kukikaribisha chama  cha FPOe katika  serikali  yake , waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa Ujerumani  Heiko Maas wa chama  cha  siasa za wastani za  mrengo wa  kushoto  Social Democratic  SPD amesema, akiwaita "maadui wa  uhuru".

Wengine moja  kwa  moja  wamekionya  chama  cha  CDU kuachana na  uwezekano wa  ushirikiano  na chama  cha  siasa  kali  za mrengo  wa  kulia  nchini  Ujerumani  cha  Alternative for Germany , AfD.

Finnland PK Heiko Maas
Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani Heiko MaasPicha: Imago Images/photothek/F. Zahn

Wapiga  kura  baadaye  mwaka  huu  katika eneo  la  zamani mashariki  mwa  Ujerumani lililokuwa  la  kikomunist wanatarajiwa kukipa  chama  hicho matokeo  mazuri hali  inayoweza  kuwa  vigumu kujenga serikali  ya  mseto  katika  ngazi  ya  taifa  bila  chama hicho.

Vyama  vya  siasa  za  wastani  vya  mrengo  wa  kulia  katika  bara la  Ulaya "vinapaswa  kuacha  ushirika wao na  vyama vya  mrengo wa  kulia na  kujiweka  mbali  kwa  uwazi  na maadui  wa demokrasia," mgombea  wa  chama  cha  kijani  kwa  ajili  ya  bunge la  Ulaya  Sven  Giegold  ameyaambia  magazeti  ya  kundi  la Funke.