1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel kushiriki maandamano ya uvumilivu

13 Januari 2015

Kansela Angela Merkel wa Ujerumani anatazamiwa kushiriki maandamano ya jamii ya Waislamu leo hii kukuza suala la uvumilivu katika jamii na kulaani mashambulizi yaliofanywa na Waislamu wa itikadi kali mjini Paris.

https://p.dw.com/p/1EJLb
Maandamano ya vuguvugu la PEGIDA mjini Dresden. (12.01.2014)
Maandamano ya vuguvugu la PEGIDA mjini Dresden. (12.01.2014)Picha: Reuters/F. Bensch

Rais Joachim Gauck atahutubia katika maandamano hayo yatakayoanza saa moja usiku katika eneo mashuhuri la Lango la Bradenburg mjini Berlin maandamano yaliyoandaliwa na Baraza Kuu la Waislamu nchini Ujerumani chini ya beramu "Kuwepo mashirikiano.Ugaidi sio jina letu".

Merkel ambaye atakuwepo takriban na baraza lake lote la mwaziri katika maandamano hayo amelishutumu kundi la siasa kali za mrengo wa kulia linalojiita Wazalendo wa Ulaya Dhidi ya Kusilimishwa kwa Ulaya au PEGIDA kwa kifupi na kusisitiza hapo jana kwamba Uislamu ni sehemu ya Ujerumani.

PEGIDA hapo jana iliwavutia waandamanaji 25,000 katika maadanano yake ya 12 ya kila wiki mjini Dresden mji ulioko mashariki mwa Ujerumani ambayo zamani ilikuwa chini ya utawala wa Kikomunisti. Wafuasi wake waliokuwa wakipeperusha bendera walibaki kimya kwa dakika moja kutowa heshima zao kwa wahanga wa mashambulizi ya gazeti la Charlie Hebdo mjini Paris wiki iliopita.

Vuguvugu la kupinga PEGIDA lapata nguvu

Maandamano yao hayo yalikabiliwa na maandamano mengine yanayowapinga yaliohudhuriwa na watu 100,000 nchíni kote ambao wanaishutumu PEGIDA kwa kutumia vibaya kwa faida yao mashambulizi hayo yaliofanywa na Waislamu wa itikadi kali nchini Ufaransa ambapo wameelezea kuunga mkono kwao kuwepo kwa jamii ya tamaduni tafauti nchini Ujerumani.

Maandamano ya Leipzig dhidi ya PEGIDA. (12.01.2014)
Maandamano ya Leipzig dhidi ya PEGIDA. (12.01.2014)Picha: picture-alliance/dpa

Merkel hapo jana amewashukuru viongozi wa jamii ya Waislamu milioni nne wanaoishi Ujerumani kwa kulaani kwa haraka bila ya ajizi mauaji yaliofanyika kwa kutumia jina la dini yao mjini Paris wiki iliopita.

Amesema katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari uliohudhuriwa pia na Waziri Mkuu wa Uturuki Ahmet Davutoglu kwamba Ujerumani inataka Waislamu waishi kwa pamoja kwa amani na wafuasi wa dini nyengine na kwamba maandamano ya leo usiku yatatowa ujumbe mzito.

Merkel halazi damu

Merkel na Davotoglu wiki iliopita waliungana na Rais Farncois Hollande wa Ufaransa na viongozi wengine duniani katika maandamano makubwa kabisa ya mshikamano mjini Paris kufuatia mauaji ya watu 17 katika ofisi ya gazeti la dhihaka lilitolewalo kila wiki la Charlie Hebdo na katika tukio la kushikiliwa watu mateka katika duka moja la Kiyahudi.

Kansela Angela Merkel katika mkutano na waandishi wa habari mjini Berlin.(13.01.2014)
Kansela Angela Merkel katika mkutano na waandishi wa habari mjini Berlin.(13.01.2014)Picha: picture-alliance/AA/M. Kaynak

Katika taarifa yao Baraza la Waislamu na jamii ya Waturuki nchini Ujerumani wakati wakilani mashambulizi hayo ya Paris wamesema kuzuka kwa wimbi jipya la ubaguzi na chuki dhidi ya Uislamu katika mitaa ya Ujerumani kunazidi kuwapalilia wachochezi na magaidi .

Maoni yaliyotolewa kwenye mtandao wa gazeti la Spiegel nchini Ujerumani yamempongeza Merkel ambaye anajulikana sana kwa kutoyalazia damu masuala nyeti kwa kutowa kauli ya wazi kulaani chuki dhidi ya Uislamu hata kama anahatarisha kukipotezea wapiga kura chama chake cha kihafidhina.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AFP/dpa

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman