1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel yuko Moscow kwa mkutano wa mwisho na Putin

Bruce Amani
20 Agosti 2021

Kansela Angela Merkel wa Ujerumani amemwambia Rais Vladmir Putin wa Urusi kuwa Moscow na Berlin zinapaswa kuzungumza licha ya tofauti kubwa zilizopo

https://p.dw.com/p/3zHfT
Russland Moskau | Angela Merkel und Vladimir Putin
Picha: Sputnik/REUTERS

Merkel ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya mwisho ya kikazi nchini Urusi kabla ya kuachia ngazi nafasi yake baada ya uchaguzi wa Ujerumani wa Septemba 26.

Soma pia: Merkel na Putin kujadili Afghanistan na masuala mengine

Ziara ya Merkel nchini Urusi imekuja katika mkesha wa kumbukumbu ya mwaka mmoja tangu shambulizi la sumu inayoathiri mishipa ya fahamu dhidi ya kiongozi wa upinzani ambaye sasa yuko jela Alexei Navalny, ambaye maisha yake yalinusuriwa na madaktari wa Berlin.

Russland | Moskau | PK Angela Merkel und Wladimir Putin
Merkel amemhimiza Putin kumwachilia huru NavalnyPicha: Mikhail Metzel/ITAR-TASS/imago images

Akizungumza katika kikao cha waandishi wa habari baada ya kufanya mazungumzo na mwenyeji wake, Merkel alimhimiza Putin kumuwachilia huru mwanaharakati huyo.

Kuhusu suala la Afghanistan ambako wanamgambo wa Taliban wamekamata udhibiti wa nchi baada ya kuiangusha serikali ya Kabul, Merkel amesema kwa sasa kipaumbele cha Ujerumani ni kuwahamisha Waafghanistan waliofanya kazi na Marekani na kuwapeleka Ujerumani. Rais Putin amesema nchi nyingine hazipaswi kuiwekea Afghanistan maadili yao na kuwa ukweli ni kwamba Taliban imechukua udhibiti wa eneo kubwa la nchi hiyo. Amesema anatumai Wataliban watatimiza ahadi zao za kurejesha utulivu Afghanistan na kuwa ni muhimu kuwazuia magaidi kuingia katika nchi jirani.

Soma zaidi: Urusi yamkamata mkosoaji mwingine wa Kremlin

Pia wamejadili mgogoro unaofukuta mashariki mwa Ukraine na ukandamizaji wa kimabavu nchini Belarus ambayo ni mshirika wa Urusi.

Amesema mazungumzo kuhusu Ukraine yamekwama na ana mpango wa kuyafufua. Putin alimpokea Merkel na shada la mauwa, kitendo anachowafanyia viongozi wanawake, na akasema anatumai ziara hiyo haitakuwa tu ya kwaheri bali yenye umuhimu

Russland | Moskau | PK Angela Merkel und Wladimir Putin
Putin amesema kufungwa Navalny hakujachochewa kisiasaPicha: Mikhail Metzel/ITAR-TASS/imago images

Kiongozi huyo wa Ujerumani mwenye umri wa miaka 67 ambaye atajiondoa kwenye siasa baada ya uchaguzi wa Ujerumani wa Septemba 26 anatarajiwa kukutana na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenesky Jumapili, wakati mvutano ukiendelea kuhusiana na urusi kuwapeleka wanajeshi wake kwenye mipaka ya Ukraine.

Ujerumani imekuwa mchangiaji muhimu katika juhudi za kuleta amani mashariki mwa Ukraine. Aidha huenda akaipa Ukraine uhakikisho kuhusu mradi wa bomba la gesi la Nord Stream 2, ambao unapingwa na Marekani.

Soma pia: Putin awaonya wanaoingilia masuala ya ndani ya Urusi

Mkuu wa Shirika la nishati la Ukraine Naftogaz limesema leo kuwa bomba hilo la gesi ni mradi wa kisiasa ambao unakiuka kanuni za Umoja wa Ulaya, usiweza kufanya kazi kibiashara na unaopaswa kusitishwa.

AFP/AP/DPA/Reuters