1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mgogoro wa majeruhi waongezeka katika timu ya Bayern

11 Aprili 2015

Kocha wa Bayern Munich Pep Guardiola ameitaja hali ya majeruhi katika klabu hiyo kuwa “mbaya zaidi” baada ya beki wa kati Medhi Benatia kuwa mchezaji wa hivi punde kuongeza kwenye orodha hiyo

https://p.dw.com/p/1F6MY
Mehdi Benatia
Picha: AFP/Getty Images/C. Stache

Mchezaji huyo wa timu ya taifa ya Morocco huenda akakosa mipambano yote ya robo fainali ya Champions League dhidi ya Porto wiki ijayo kutokana na maumivu ya msuli ambayo aliyapata wakati wa mchuano wa Jumatano wa robo fainali ya Kombe la Shirikisho la Ujerumani ambao waliishinda Bayer Leverkusen.

Guardiola anasema walikuwa na matatizo na sasa wana matatizo mengi hata zaidi. Hali yao kwa sasa ni mbaya, mbaya sana. Anasema hajawahi kuwa katika hali hiyo ya majeruhi wengi lakini licha ya hayo yote, watafanya kila juhudi kutimiza malengo yao msimu huu.

Bayern wanaoongoza ligi na pengo la pointi kumi, wanalenga kunyakua mataji matatu, na kurudia mafanikio yao ya msimu wa 2013. Benatia sasa amejiunga na Bastian Schweinsteiger, David Alaba, Arjen Robben, Javi Martinez na mlinda mlango wa akiba Tom Starke katika orodha ya majeruhi.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/Reuters
Mhariri: Mohamed Dahman