Mgomo Ufaransa
23 Oktoba 2010Licha ya kuwepo migomo, maandamano na kuzuiliwa kwa mafuta nchini Ufaransa katika kupinga mswada wenye mzozo wa mageuzi ya pensheni, wa rais Nicolas Sarkozy, hapo jana Baraza la Senate nchini humo limeuidhinisha mswada huo. Mswada huo unaongeza umri wa kustaafu kutoka miaka 60 hadi 62. Awali vyama vikuu vya wafanyakazi nchini humo vilitangaza migomo ya siku mbili zaidi wiki ijayo. Masaa kadhaa baada ya kutolewa tangazo hilo, maafisa wa polisi waliwatawanya watu waliokuwa wamezuia kampuni ya kusafisha mafuta mashariki mwa mji mkuu wa Paris. Maafisa wa serikali waliwaamuru pia wafanyakazi wa kampuni hiyo ya mafuta kurudi kazini, wakitaja kuwepo tishio kwa utulivu wa wananchi.
Mswada huo sasa unatarajiwa kujumuishwa na mapendekzo ya baraza la wawakilishi kabla ya kuidhinishwa kwa kura ya mwisho siku ya jumatano.
Maandamano yanayofanyika nchini humo yamekuwa ndio vita vikuu katika hatamu ya kwanza ya serikali ya mrengo wa kulia ya rais Nicolas Sarkozy. Huku umaarufu wake ukiwa chini katika matokeo ya kura za kutafuta maoni, Rais Sarkozy anasema mageuzi hayo ni muhimu kupunguza nakisi ya serikali.
Mwandishi: Maryam Abdalla/DPAE/AFPE
Mhariri:Grace Patricia Kabogo.