1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Miaka 150 ya chama cha SPD

Admin.WagnerD23 Mei 2013

Chama cha Kisoshalisti cha Ujerumani, SPD, Alhamisi kimesherehekea miaka 150 ya kuanzishwa kwake, huku Kansela Angela Merkel akitoa sifa kwa wapinzani wake hao, kwa kuwaita sauti ya demokrasia isiyokubali kushindwa.

https://p.dw.com/p/18csC
Miaka 150 ya SPD
Miaka 150 ya SPDPicha: picture-alliance/dpa

Chama hicho kikongwe zaidi nchini Ujerumani kiliwaalika wakuu wa nchi na serikali karibu 50 wakiwemo viongozi waliopo madarani na wastaafu, wakati kikikumbuka historia yake iliyojaa misukosuko, ambayo ilikishuhudia kikipigania haki za wafanyakazi, kupinga Wanazi na kukonga nyoyo za wanawake. Chama hicho pia kinaangalia siku zijazo wakati kikilenga kujizindua upya wakati wa sherehe hizo zinazofanyika Leipzig, mji wa mashariki mwa Ujerumani ambako mtangulizi wa SPD, chama cha Wafanyakazi cha Ujerumani, kilianzishwa mwaka 1863.

Kansela Angela Merkel, mwenyekiti wa SPD Sigmar Gabriel, na rais Francoise Hollande katika sherehe ya miaka 150 ya SPD mjini Leipzig.
Kansela Angela Merkel, mwenyekiti wa SPD Sigmar Gabriel, na rais Francoise Hollande katika sherehe ya miaka 150 ya SPD mjini Leipzig.Picha: picture-alliance/dpa

Mwanzo mpya

Mwenyekiti wa SPD ngazi ya taifa, Sigmar Gabriel, ambae hapo awali alizielezea sherehe hizo kama tukio kubwa zaidi la kimataifa la kisiasa nchini Ujerumani mwaka huu, alisema chama hicho lazima kirudi kuwa kama vuguvugu la kijamii tena. SPD ambayo inapiga kampeni kwa kushirikiana na cha kijani, imewasilisha programu yake ya sera inayoelekea kushoto zaidi katika miaka mingi, ikishninikiza kulegeza hatua za kubana matumizi barani Ulaya, kuwepo na kiwango cha chini cha mshahara na kodi kubwa kwa matajiri.

Sherehe hizo zimefanyika katika ukumbi mkubwa uliokuwa na wageni 1,600, ambao ulipambwa na rangi nyenkundu, ambayo ni rangi rasmi ya chama hicho, huku msanii wa kimataifa Stevie Wonder akitumbuiza na wimbo wake wa 'Happy Birthday'. Makansela wa zamani wa Ujerumani Gerhard Shroeder na Helmut Schmidt walikaa mstari wa mbele, wakati huku televisheni kubwa zikionyesha picha za kumbukumbu kwa viongozi waliopita, akiwemo waziri mkuu wa zamani wa Uingereza, Tony Blair, na rais wa zamani wa Urusi, Mikhail Gorbachev.

Merkel aimwagia sifa

Kansela Angela Merkel, katika makala aliyoiandikia gazeti la Leipziger Volkszeitung alisifu mchango wa kihistoria wa  chama cha SPD, kama sauti ya kishujaa na isiyoyumbishwa ya kidemkrasia nchini Ujerumani, na kusema kuwa kwa huduma hizo ambazo haziwezi kuthaminiwa vya kutosha, chama cha SPD kinastahiki heshima na shukrani kutoka kwake.

Siku moja kabla ya sherehe hizo, kundi la kimataifa la karibu vyama 70 vya mrengo wa kati-kushoto vikiwemo chama cha Labour cha nchini Uingereza, ANC ya Afrika Kusini na chama cha Demokrats cha Marekani vilianzisha ushirikiano wa maendeleo mjini Leipzig.

Rais wa Ujerumani Joachim Gauck akiwasili katika sherehe za SPD mjini Leipzig, mashariki mwa Ujerumani.
Rais wa Ujerumani Joachim Gauck akiwasili katika sherehe za SPD mjini Leipzig, mashariki mwa Ujerumani.Picha: picture-alliance/dpa

Agenda kuu ya kuanzishwa kwake

Kikianzishwa kama mbadala wa muungano wa kimataifa wa kisoshalisti ulioanzishwa mjini Paris Ufaransa mwaka 1889, agenda kuu ya SPD ilikuwa maendeleo ya kidemokrasia, kijamii na kimazingira katika karne ya 21.Maafisa katika ikulu ya Ufaransa ya Elysee wamesema Hollande alihudhuria sherehe hiyo isiyoegemea vyama kwa baraka za Kansela Merkel, na kwamba hakuwa na nia ya kutumia sherehe hiyo kuwapigia kampeni wapinzani wa Merkel.

Merkel, ambae amechaguliwa kama mwanasiasa maarufu zaidi nchini Ujerumani mara kadhaa, na anaechukuliwa kuwa kiongozi mwenye nguvu zaidi barani Ulaya wakati wa mgogoro wa kiuchumi, hakutarajiwa kuzungumza katika sherehe hiyo, ambayo amehudhuria kama kiongozi wa kitaifa. Katika hotuba yake ya ufunguzi, rais  wa Ujerumani Joachim Gauck alisema siku hii ni ya kusherehekea si tu kwa chama kikongwe zaidi nchini Ujerumani, bali pia kwa mapambano ya bara la Ulaya kwa ajili ya uhuru na demokrasia.

Mwandishi: Iddi Ismail Ssessanga/afpe,
Mhariri: Mohammed Khelef