1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Michezo mwishoni mwa juma

Sekione Kitojo26 Julai 2010

Real Madrid yaagana na Raul baada ya miaka 16 ya kuichezea timu hiyo na michuano ya riadha kwa mataifa ya Afrika kuanza Jumatano nchini Kenya.

https://p.dw.com/p/OUz6
Mshambuliaji wa Real Madrid Raul Gonzalez akishangilia bao katika moja kati ya michezo aliyoshiriki akiwa na timu hiyo ya Hispania .Picha: picture-alliance/dpa

Real Madrid  yasema  adios  kwa  Raul  aliyeitumikia   timu hiyo  ya  mjini  Madrid  kwa  muda  wa  miaka  18,

Mashindano  ya  ubingwa  wa  riadha  ya  bara  la  Ulaya kuanza  kesho  Jumanne, 

na   huko  katika  bara  la  Afrika  mashindano  ya  riadha ya  ubingwa  wa  Afrika   kuanza   Jumatano,  nchini Kenya.

Kwa  hayo  na  mengineyo  nasema  karibuni:

Real  Madrid  imethibitisha  kuwa  nahodha  wake  na  pia mpachika  mabao  maarufu   Raul  Gonzalez, ataiacha mkono  klabu  hiyo  maarufu  leo  Jumatatu  baada  ya kuitumikia  kwa  muda  wa  miaka  16  mfululizo  na huenda  atahamia  katika  klabu  ya  Ujerumani  ya Schalke 04.

Raul   ameichezea  Real   tangu  mwaka  1994, ameshinda ubingwa  wa  ligi  ya  Hispania, La  Liga  mara  sita  pamoja na   kombe  la  ligi  ya  mabingwa  mara  tatu katika  wakati wake  na  vigogo  hivyo  vya  soka  nchini  Hispania.

Amepachika  mabao  323  katika   mara  740  alizoingia uwanjani  na  timu  hiyo. Mchezaji  mwenzake  Gutti , akiwa nae  ni  matokeo  ya  mfumo  wa  timu  za  vijana   katika klabu  hiyo  ya  Real  na  ambaye  alinza  kuichezea  timu hiyo  mwaka  1995, amesema   mapema  jana  Jumapili kuwa   anaondoka  nae  katika  timu  hiyo  na  Besuktas nchini  Uturuki  ndiko  kutakuwa  nyumbani  kwake  hivi sasa.

Wachezaji  hao  wote  wawili  wameambiwa  na  kocha mpya  Jose  Mourinho  kuwa  hawatakuwa  sehemu  ya mipango  yake  kwa  ajili  ya  msimu  mpya.

Raul  mwenye  umri  wa  miaka  33 ambaye  ni  kipenzi  cha mashabiki  wa   Real , machozi  yalikuwa  yakimdondoka wakati  akitangaza  kuagana  na  klabu  hiyo katika mkutano  na  waandishi  habari  katika  uwanja  wa Bernabeu.

Sherehe  hizo  za  kumuaga  zimefanyika  mchana  wa  leo na  kukiri  kuwa   huenda  akahamia  katika  klabu  ya Bundesliga  ya  Schalke 04   timu  ambayo  imesema itampa  mkataba  wa  miaka  miwili, kwa  mujibu  wa vyombo  vya  habari  vya  Ujerumani , lakini  amesema  pia kuwa  kuna  uwezekano  akahamia  nchini  Uingereza.

Mchezaji  mwenzake  Gutti  amesema   kuwa  anafunga ukurasa  wa  enzi  yenye  utukufu  mkubwa  katika  wakati wake  wa  kucheza  soka ,baada  ya  miaka  15  ya kuichezea  Real  Madrid.

Huko  Amerika  ya  kusini,  wachezaji  wa   timu  ya Corinthians  wamempa  kocha  mpya   wa  Brazil  Mano Menezes  mkono  wa  kwaheri  kwa  kuichapa  Guarani kwa  mabao  3-1  na  kujiweka  kileleni  mwa  ubingwa  wa ligi  ya  Brazil. Menezes , ambaye  anachukua  hatamu  za kuifunza   timu  ya  taifa  ya  Brazil  leo  Jumatatu  ambapo anatarajiwa  kutangaza  kikosi  chake  kwa  ajili  ya  mchezo wa  kirafiki    na  Marekani  mwezi  ujao, alipewa  kwaheri stahili  baada  ya   mashabiki  kusimama  kwa  heshima yake  uwanjani  hapo.Menezes  ambaye  aliiongoza Corinthians   kutoka   daraja  la  pili  katika  msimu  wake wa  kwanza   akiwa  kocha  mwaka  2008,   nafasi  yake itarithiwa  na  Adilson Batista, ambaye  alifurushwa  na timu  ya  Cruzeiro  mwezi  uliopita.

Mawakala  wa  mchezaji  nyota  kijana  wa  Italia mshambuliaji  Mario Baloteli  wamekanusha  leo  Jumatatu kuwa  mchezaji  wao  ametia  saini  kuichezea  klabu  ya ligi  kuu  ya  Uingereza  Manchester  United. Ripoti  za hapo  kabla  katika  vyombo  vya  habari  nchini  Italia zimedai  kuwa  kijana  huyo  mwenye  umri  wa  miaka  19 mshambuliaji  wa  Inter Milan   tayari  amekubali  mkataba na  timu  hiyo  ya  ligi  kuu  ya  Uingereza  na  kwamba  kile kinachokosekana  kwa  sasa  ni  makubaliano  baina  ya vilabu  hivyo  viwili. Lakini  wakala  wake  Mono Raiola ameliambia  shirika  la  habari  la  Ansa, kuwa  hakuna  kitu kama  hicho  kilichotiwa  saini  kati  ya  Baloteli  na Manchester  City  na  sidhani  kama  kuna  kitu  kama hicho  kitatokea  katika  siku  chache  zijazo.

Na  wiki  moja  baada  ya  kukataliwa  kuhamia   Fulham  ya Uingereza, kocha  wa  Ajax  Amsterdam  Martin  Jol anapaswa  sasa  kukitayarisha  kikosi  chake  kupambana na   PAOK Salonika  ya  Ugiriki  katika  ligi  ya  mabingwa duru  ya  tatu  siku  ya  Jumatano.

Jol amewaongoza  mabingwa  mara  tano  wa  ligi  ya mabingwa  barani  Ulaya  Ajax  kuwa  makamu  bingwa  wa ligi  ya  Uholanzi, Eredivisie,  nyuma  ya  FC Twente  msimu uliopita, lakini  amekasirishwa  na  kile  anachokiona  kuwa ni  klabu  hiyo  kutokuwa    na  nia  ya  kuwazuwia wachezaji  wao  muhimu  kuondoka  katika  klabu  hiyo. Ni katika  wakati  huu  ndipo Jol  alipokubali  mualiko  wa kujiunga  na  Fulham  ya  Uingereza, lakini  alikataliwa ruhusa  ya  kuondoka  na  ameapa  kusahau  yote  hayo na  kuganga  yajayo.

Manchester  United  imepata  kipigo  chake  cha  kwanza katika  ziara  yake  ya  kabla  ya  kuanza  kwa  msimu  wa ligi  katika  mataifa  ya  Amerika  ya  kaskazini  wakati walipobanjuliwa  kwa  mabao  2-1  dhidi  ya  Kansas  City Wizards  mjini  Kansas  jana  Jumapili.

Mbele  ya  mashabiki  52,000  katika  uwanja  wa Arrowhead, Wizards  walifungua  ukurasa  wa  mabao katika  dakika  ya  11  kwa  bao  la  mchezaji  wa  kati  Davy Arnaud  kabla  ya  Dimitar  Berbatov  kurejesha  bao  hilo kwa  mkwaju  wa  penalti, lakini  Kei  Kamara  aliirejeshea ushindi  Kansas  dakika  moja  baadaye.

Dane  Richards  alipachika  bao  katika  dakika  ya  70 kuipa  ushindi  New York Red  Bulls  katika  ushindi  wa mabao  2-1  pia  dhidi  ya  timu  ya  ligi  kuu  nchini Uingereza   ya  Manchester  City  jana  Jumapili , timu ambayo  nayo  kama  Man United  iko  katika  ziara  katika bara  la  Amerika.

Tottenham  Hotspurs  wametoka  sare  ya  bao  2-2  dhidi ya  Sporting  Lisbon  katika  mchezo  wa  kirafiki  wa kimataifa mjini  New  Jersey  , Marekani  jana  Jumapili, ambako  timu  zote  hizo  mbili  ziko  ziarani  kwa  ajili  ya kujiandaa  na  ligi  za  nchi  zao.

Kiongozi  mkuu   mpya  wa  chama  cha   soka  nchini Japan   Junji Ogura  ataogoza  juhudi  za  nchi  hiyo   za kutaka  kuwa  mwenyeji  wa  fainali  za  kombe  la  dunia mwaka  2022, chama  hicho  kimesema  leo  Jumatatu.

Kiongozi  huyo  mwenye  umri  wa  miaka  71 ameteuliwa kuwa  rais  mpya  wa   chama  cha  soka  nchini  Japan , JFA, jana  Jumapili  baada  ya  mtangulizi  wake  Motoaki Inukai  kujiuzulu  baada  ya  kipindi  cha  utawala  cha miaka  miwili  akielezea     kujizulu  kwake   ni  kutokana  na sababu  za  kiafya.

Michezo ya riadha ya bara la Ulaya inaanza rasmi siku ya Jumanne mjini Barcelona. Na mwanariadha, Christophe  Lemaitre  mkimbiaji  kutoka  Ufaransa anakumbana  na  mkimbiaji  kutoka  Uingereza  Dwain Chambers  katika   pambano  la  mita  100  katika mashindano  ya  ubingwa  wa  riadha  katika  bara  la Ulaya  yanayoanza  kesho  Jumanne  mjini  Barcelona.

Kijana  huyo  mwenye  umri  wa  miaka  20  yuko  katika chati  za  juu  za  wakimbiaji  barani  Ulaya  kwa  mbio  za mita  100  na  200  akiwa  yuko  katika  hali  nzuri  kabisa katika  wakati  muhimu  kwa  ajili  ya  mashindano  hayo yanayofanyika  katika  mji  wa  Barcelona.

Mbio  hizo  za  mita 100  pia  hazitavuta  hisia  kwa wanariadha   hao  wawili  tu, ambapo  raia  wa  Norway Jaysuma Saidy Ndure  akiwa  nae  anawania  taji  hilo kama  alivyo  Martial Mbandjock  kutoka  Ufaransa  pia.

Kuruka  juu  wanawake  pia  ni  tukio  linalosubiriwa  kwa hamu  kubwa   wakati  bingwa  wa  dunia , mwaka  2007 na  2009, Blanka Vlasic  akilenga   kuivunja  rekodi  ya muda  mrefu  ya  dunia  ya  mita 2.09  iliyowekwa  na Stefka  Kostadinova.

Tennis.

Bingwa  wa  mchezo  wa  tennis  katika  michuano  ya Wimbledon  Serena  Williams  anaendelea  kuwa  katika nafasi  ya  juu  ya  orodha  ya  wachezaji  wa  tennis duniani  iliyotolewa  leo  na   shirikisho  la  tennis  duniani , WTA. Msichana  huyo  kutoka  Marekani  anafuatiwa  na Jelena  Jankovic  kutoka  Serbia  pamoja  na  dada  yake Venus  Williams  akishika  nafasi  ya  tatu.

Mwandishi : Sekione  Kitojo/ AFPE/ DPAE / RTRE

Mhariri : Josephat  Charo.