1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Michezo mwishoni mwa wiki

14 Machi 2008

Ligi maarufu za ulaya pamoja na Bundesliga zarudi uwanjani leo na kesho.Kuba yapoteza wachezaji 7 wa taifa.

https://p.dw.com/p/DOMT

Baada ya changamoto za champions League na kombe la Ulaya la UEFA kati ya wiki, timu kadhaa zinarudi uwanjani mwishoni mwa wiki hii kunyan'ganyia mataji ya ubingwa na hasa katika Ligi mashuhuri za Ulaya-Premier League huko Uinghereza,La Liga nchini Spain ,Serie A nchini Itali na hata Bundesliga hapa Ujerumani.

►◄

Viongozi wa Bundesliga -Ligi ya Ujerumani Bayern Munich wanatumai leo kutoroka na pointi 3 nyengine huko mashariki mwa Ujerumani ambako wana miadi na Energie Cottbus inayoburura mkia wa Ligi na yaonesha haitaweza kuepuka kuteremshwa.Munich mwishoni mwa wiki iliopita iliizaba Karlsruhe mabao 2-0 na kupanua mwanya wake na Werder Bremen iliokua nafasi ya pili hadi pointi 7. Munich kabla ya changamoto za leo ina jumla ya pointi 50 kwa 43 za mahasimu wao wakubwa Werder Bremen.

Na wakati Munich ilitamba kati ya wiki na kukata tiketi yake ya robo-finali ya kombe la ulaya la UEFA,Bremen iliaga mashindano hayo baada ya kumudu ushindi wa bao 1:0 mbele ya Glasgow Rangers ya scotland bao ambalo halikuweza kufuta mabao 2 iliochapwa duru ya kwanza huko Glasgow.

Munich iliitoa Anderlecht ya Ubelgiji ilipoizaba mabao 5:0 kabla haikuzabwa mabao 2-1 na Anderlecht nyumbani mwao.

Mabingwa stuttgart wana miadi leo na Bochum na wakitoroka na pointi 3 nyengine bila ya shaka wataparamia zaidi kileleni mwa Ligi kutoka nafasi ya 6 waliopo sasa.

Mpambano wa leo unachezwa huku Stuttgart ikifurahia taarifa kwamba itajipatia uwanja mpya wa dimba.

Mpambano mwengine wa kusisimua utakua kati ya Hamburg na Borussia Dortmund wakati hansa Rostock inamenyana na Berlin.Hannover 96 inacheza nyumbani na arm.Bielefeld-jirani zao huku Eintracht Frankfurt ikikamilisha kalenda ya leo huko Karlsruhe.

Mapambano 2 yamepangwa kesho jumapili kati ya bayer Leverkusen iliokata nayo tiketi ya robo-finali ya kombe la ulaya la UEFA kama Bayern Munich ikiwa na miadi na Nüremberg iliopo mkiani mwa Ligi.Werder Bremen ilitolewa nje ya kombe la UEFA ina miadi nyumbani kesho na Wolfsburg.

Kinyan'ganyiro katika premier League-ligi ya uingereza kinanyemelea kupambamoto mwishoni mwa wiki hii huku viongozi wa Ligi-Arsenal ,manchester United na Chelseab zikiendelea kupapurana kileleni mwa Ligi hiyo.

Ushindi wa mabao 6-1 wa Chelsea dhidi ya cipukizi Derby kati ya wiki kumefanya pointi 5 tu zinazitenga klabu 3 za usoni.Manchester yaweza kuipiku Arsenal ikiilaza Derby kabla Arsenal kupambana na Middlesbrough baadae jioni ya leo.Manchester yaweza kupumua kwa kurudi uwanjani kwa stadi wao Gary Neville.

Kinyan'ganyiro katika serie A-Ligi ya Itali hakitakua rahisi kwa viongozi wa ligi -Inter Milan baada ya kupigwa kumbo kabisa kati ya wiki kutoka kombe la ulaya la klabu bingwa-champions league.Roma inayonyatia nafasi ya pili lazima imetambua mashaka ilionayo Inter wakati huu na wako tayari kufaidika kwa madhambi yoyote itakayofanya Inter mwishoni mwa wiki hii.

Nahodha wa AS Roma Francisco Totti anadai kinyan'ganyiro cha ubingwa wa Itali msimu huu mni kikali zaidi kulimko msimu uliopita pale Inter Milan ilipotoroka bila kutokwa jasho na taji la ubingwa.

Katika kinyan'ganyiro cha dimba la Olimpik huko Beijing, Kuba imepungukiwa na wachezaji kwa mpambano wake wa leo na panama.Wachezaji 7 wa taifa waliiachamkono timu yao na kutorokea Marekani kati ya wiki hii.kikosi chao cha wachezaji 18 kilisaliwa na wachezaji 11 tu.Si ajabu Kuba ilizabwa mabao 2 na Hondurus katika mpambano wake wapili ikicheza na wachezaji 10 tu.Uamuzi gani sasa utachukuliwa na CONCACAF-shirikisho la dimba la Amerika kaskazini haijulikani,lakini Kuba inadai itayari kuteremka uwanjani hata na wachezaji 7.Na sheria zawaruhusu .