1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Michezo wiki hii

24 Oktoba 2008

Hamburg yatetea uongozi kileleni mwa Bundesliga-Simba na Young Africans wana miadi Dar-es-salaam.

https://p.dw.com/p/FgG7
Munich ilipotamba mbele ya fiorentina.Picha: picture-alliance/dpa

Baada ya changamoto za champions League na kombe la ulaya la UEFA kati ya wiki,Ligi mashuhuri za ulaya zinarudi uwanjani mwishoni mwa wiki hii huku ulaya wakati nchini Tanzania jumamosi hii, mahasimu wawili wa jadi-young Africans na Simba Sports Club wana miadi ya kuonana uwanjani.Timu ya Taifa ya Ujerumani imo mashakani-baada ya kisa cha Kuranyi sasa ni cha nahodha Ballack na kocha wa timu ya Taifa.

Mtoto wa shule nchini Morocco shabiki wa FC Barcelona,miezi 18 korokoroni:kisa nini-ameingiza FC Barcelona katika wimbo wa Taifa mahala pa jina la mfalme Mohammed VI.Na Rais wa Halmashauri kuu ya Olimpik Ulimwenguni (IOC) Jacques Rogge wa Uswisi kugombea tena wadhifa huo.

Viongozi wa Bundesliga-Ligi ya Ujerumani Hamburg baada ya kutamba kati ya wiki katika Kombe la ulaya la UEFA walipoizaba Zilina ya Slovakia mabao 2-1, wana miadi kesho jumapili na Hoffenheim,timu ya chipukizi iliopanda msimu huu daraja ya kwsanza lakini iko nafasi ya pili ya ngazi ya Bundesliga.

Duru ya mwishoni mwa wiki hii ilifunguliwa jana ijumaa pale mahasimu wawili wa mtaani-Bayer Leverkusen na FC Cologne zilipopeana changamoto iliosubiriwa kwa hamu mno na mashabiki wa Cologne na kitongoji chake Leverkusen.

Lakini, mla wanasema ni mla leo,mla jana kala nini.Mabingwa Bayern munich baada ya kutamba nao katika champions League kwa mabao 3-0 mbele ya Fiorentina ya Itali kati ya wiki, imerudi uwanjani hivi punde kuania pointi 3 nyengine nyumbani mara hii kutoka kikapu cha Wolfsburg.

Jumamosi iliopita, Munich ilivuka chupu-chupu ilipojipatia bao 1 la ushindi dhidi ya Karlsruhe dakika za mwisho za mchezo.Lakini leo ikitiwa shime na ushindi wake katika champions League, inatumai firimbi ya mwisho ikilia hivi punde mjini Munich,Munich itaondoka na pointi 3 nyengine.

Katika mpambano huo lakini, kocha Jurgen klinsmann alipaswa kucheza bila ya beki wao mshahara Philipp Lahm na mshambulizi hatari mtaliana Luca Toni.Toni aliuumia mwishoni mwa wiki iliopita katika mpambano na Karlsruhe.Stuttgart ina miadi kesho na Bochum wakati Borusdsia Dortmund inatoana jasho na Hertha Berlin.

Katika timu ya taifa ya Ujerumani wakati huu mvutano unaendelea.Baada ya kutimuliwa nje kwa mshambulizi wake Kevin Kuranyi wa klabu ya Schalke sasa kumeibuka suittafaham kati ya kocha Joachim Loew na nahodha wake Michael Ballack-mvutano ambao unafuatia ule wa kwanza kati ya Ballack na meneja wa timu ya Taifa Oliver Bierhoff.

Nahodha wa Ujerumani Michael Ballack amekubali kukutana na kocha wa Taifa Joachim Loew (lov) katika ishara ya kwanza kwamba shetani aliepanda kati yao sasa anaanza kupungwa. Kocha Loew alijibu kwa hasira matamshi ya nahodha Ballack yaliochapishwa wiki hii ambayo hayakumpendeza .Ballack alidai wachezaji mashuhuri katika timu ya Taifa hawapewi heshima inayostahiki.

Shirikisho la dimba la Ujerumani DFB likarifu jana kwamba kocha Lew na nahodha Ballack wamezungumza kwa simu siku moja kabla baada ya kocha Loew kuwasiliana na Ballack na kuafikiana nae wakutane uso kwa uso.Haijulikani bado ni lini na wapi vigogo hivyo 2 vya dimba la ujerumani vitakutana .

Loew alitoa taarifa juzi akiyaeleza maneno aliosema Ballack hayakubaliki.Akasema kwamba Ballack itampasa akubali kukutana nae uso kwa uso na kwamba kuendelea kwake kuiongoza timu ya Ujerumani kutategemea mkutano wao huo.

Wachezaji wa zamani na wa sasa wa timu ya Taifa ya Ujerumani wamekuwa wakitoa maoni yao juu ya soga hili. Vyombo vya habari vya ujerumani navyo vikahanikiza na kufika umbali wa kudai kwamba kocha Loew mwishoe atamtimua Ballack anaechezea Chelsea nje ya timu ya Taifa.Huenda Ballack asichezeshwe mpambano wa kirafiki wa mwezi ujao mjini Berlin kati ya Ujerumani na Uingereza.

Franz Beckenbauer,nahodha wa zamani wa timu ya Ujerumani na kocha wa ujerumani ilipotwaa kombe la dunia 1974 na 1990 amemtaka kocha Loev kumstahamilia Ballack na asimtimue nje ya timu ya taifa.Beckenbauer alinukuliwa kusema,

"Ballack ndie mchezaji bora kabisa tulienae na pekee wakati huu wa daraja ya dunia."

Stadi mwengine aliegonga vichwa vya habari kati ya wiki hii ni nahodha wa zamani wa Uingereza David Beckham:Rais wa Shirikisho la dimbala Itali Giancarlo Abete alihoji uamuzi wa klabu ya Itali ya AC Milan kumuajiri stadi wa sasa wa klabu ya Los Angeles Galaxy. Beckham stadi wa zamani wa Manchester United na Real Madrid,akiwa sasa na umri wa miaka 33 amekuwa akiichezea Los Angeles galaxy mnamo mwaka unusu uliopita katika Ligi ya Marekani.

Abete haelewi vipi Beckham atafit katika kikosi cha AC Milan cha kocha Carlo Ancelotti.AC Milan klabu ilioajiri mastadi kama Ronaldinho na Kaka wa Brazil kwamba inajadiliana na meneja wa Beckham ili kumhamishia Beckham Itali hapo januari,mwakani.

Binafsi, Beckham anavutiwa kuhamia Ligi ya ulaya ili kujiweka fit kuweza kurudi katika timu ya Taifa ya Uingereza na kutupiwa macho na kocha wake Fabio Capello. Beckham ameshaichezea England mara 107-mpambano mmoja tu kasoro kuliko Bobby Moore alieichezea England mara 108.

Katika Premier League-ligi ya Uingereza ,Wayne Rooney akitumai jumamosi hii kutia bao lake la 100 pale Manchester United ikitimiza miadi yake na Everton.Mwenzake wa bulgaria Dimitr Berbatov amepona sasa maumivu aliopata juzi wakati wa zahama za Champions League dhidi ya Celtic wakati Cristiano ronaldo pia ni fit kutamba tena baada ya kutolewa uwanjani jumaane kwa maumivu ya goti.Viongozi wa Premier League-Chelsea kesho wanatazamia kupanua uongozi wao kileleni hapo kesho watakapopapurana na Liverpool ambao wako nyuma yao kwa tofauti ya magoli.

Katika sere A, Ligi ya Itali ,kutamba juzi mbele ya Real Madrid kwa Juventus kutawatia moyo leo kuwika nyumbani mbele ya Torino.Juventus iliitandika Real 2-1. Hata Roma imeanza kupata nafuu baada ya kuizaba Chelsea ugenini bao 1:0 katika champions League.Maadui zao lakini, ni Udinese wenye pointi 14 wakiwa nafasi ya pili.Atalanta lakini, haiko mbali nao karibu na AC Milan kwa pointi zao 13.Timu nyengine zenye pointi 13 pia ni Lazio Roma na Fiorentina zinazocheza kesho Jumapili. fiorentina ilizabwa kati ya wiki mabao 3-0 na mabingwa wa ujerumani Bayern Munich.

Leo (Jumamosi) mjini Dar-es-salaam, mahasimu wawili wa jadi-Simba na Yanga wanakutana katika Ligi kuu ya Tanzania Bara.Swali lililoulizwa na mashabiki wengi wa simba kabla firimbi kulia ni je: Simba wamenoa tena makucha yao kuwanyofoa Younga ? kwani Younga ikiendelea kutamba karibuni wakati Simba amerowa maji .

Huko nchini Morocco, chipukizi mmoja wa shule amepewa kifungo cha miezi 18 korokoroni.Kosa lakini nini ? Amelichanganya jina la mfalme MohammddVI wa Morocco na klabu ya FC Barcelona ya Spain. ilikuaje ?Yassine Belassal,akionesha shabiki mkubwa wa Barcelona ya Spian , alibadili kidogo biramu la Taifa alipoasndika kwenye ubao shuleni "Mungu,taifa,Barcelona."

Mzaha wake haukumfurahisha mkuu wa shule alieiarifu polisi.Belassal alimalizikia gerezani huko Marrakesh pamoja na wahalifu wakubwa na alishindwa kuhetimu mtihani wake wa mwisho shuleni.kisa chake kimeyastusha mashirika ya haki za binadamu ambavyo vimelala mika katika wizara ya sheria ya Morocco.Wakereketwa wengine kupitia mtandao wameitaka FC barcelona kuingilia kati kumuokoa shabiki wao.Siju iwapo samuel Eto-o ataitikia ?

Rais wa Halmashauri kuu ya olimpik ulimwenguni (IOC) mbelgiji Jacques Rogge, anakusudia kugombea wadhifa wapili wa kuiongoza Halmashauri kuu ya olimpik Ulimwenguni. Uchaguzi wa rais utafanyika mwakani mwezi kama huu mjini Copenhagen,Denmark.Rogge akiwa sasa na umri wa miaka 66 alishika wadhifa huo kutoka kwa mspain Juan Antonio Samaranch hapo 2001.