1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uganda yapeta kuingia awamu ya makundi

16 Novemba 2015

Katika bara la Afrika, Uganda imesonga mbele katika awamu ya makundi kwa ajili ya kuwania kufuzu kucheza katika kombe la dunia mwaka 2018 katika bara la Afrika.

https://p.dw.com/p/1H6m2
CECAFA Fussball-Cup
Picha: EBRAHIM HAMID/AFP/Getty Images

Baada  ya  mashambulizi  mjini  Paris , ushindani  wa kiuhasama  baina ya timu  za  taifa  za  Uingereza  na Ufaransa  utashuhudia  ukurasa  mpya  wa  maombolezi na  ukimya  katika  uwanja  wa  Wembley  kesho  wakati timu  hizo  zitakapopambana.

Na kansela  wa  Ujerumani  Angela  Merkel  na  baraza lake  la  mawaziri  kuhudhuria  mpambano  wa  soka  wa kirafiki  kati  ya  Ujerumani  na  Uholanzi  kesho wakionesha  mshikamano  na  watu  wa  Ufaransa.

Morocco  na  jamhuri  ya  kidemokrasi  ya  Congo  zasonga mbele  na  kukata tikiti  katika  michuano  ya  makundi  ya kukata tikiti  za fainali za  kombe  la  dunia  nchini  Urusi mwaka  2018.

Yawezekana  kuiondoa  michezo ya  riadha  katika mashindano  ya  olimpiki  kutokana  na  matumizi makubwa  ya madawa  ya  kuongeza  nguvu  misuli , Doping ?

Kwa  hayo  na  mengi  mengine, jina  langu  ni  Sekione Kitojo, nakukaribisha  katika  ukurasa  huu  wa  michezo mwishoni  mwa  juma.

Michuano ya kirafiki barani Ulaya sehemu ya maombolezo kwa wahanga

Uingereza  na  Ufaransa  zitashuhudia  upinzani  wao mkubwa  ukitimiza  miaka  92  katika  soka  kesho Jumanne  lakini  mpambano  huo  utashuhudia  hali  ya ukimya  na  utulivu  mjini  London  katika  uwanja  wa Wembley  wakati  timu  hizo  zitakapopambana  na  timu hizo  zitaungana  katika  kuonesha  mshikamano siku  nne baada  ya  mashambulizi  ya  kigaidi  mjini  Paris.

Mashambulio  ya  Ijumaa  yamegusa  hususan  kandanda kwa  karibu, baada  ya  washambuliaji  watatu  wa  kujitoa muhanga  kujiripua  nje  ya  uwanja  wa  stade de France wakati  Ufaransa  ikicheza  na  Ujerumani.

Binamu  yake  mchezaji  wa  kati  wa  timu  ya  Ufaransa Lassana  Diarra  ni  mmoja  kati  ya  watu  129 waliouwawa , wakati  dada  yake  mchezaji  mwenzake  Antoine Griezmann alinusurika  bila  madhara  yoyote  kutoka katika  shambulio  hilo  katika  ukumbi  wa  burudani  wa Bataclan mjini  Paris.

Lakini  shirikisho  la  kandanda   la  Ufaransa  FFF, limesisitiza  kwamba  mchezo  huo  wa  kesho  uendelee na kwa  sasa  unaonekana  kama  fursa  ya  kuonesha mshikamano, na  huku  kampeni  katika  mitandao  ya kijamii  inawahimiza  mashabiki  wa  Uingereza  kujiunga na  kuimba  wimbo  wa  taifa  la  Ufaransa  "La marseillase" , kabla  ya  mchezo  huo  kuanza.

"Mchezo  huo  utakuwa  na  kila  ushindani,  lakini  pia utakuwa  unatoa  ishara  kwamba  ulimwengu  wa kandanda  uko  pamoja  dhidi  ya mauaji,"  amesema kocha  wa  Uingereza  Roy Hodgson.

Wakati  huo  huo  kansela  Angela  Merkel  wa  Ujerumani na  baraza  lake  la  mawaziri  watahudhuria  mchezo  wa kirafiki  kati  ya  Ujerumani  na  Uholanzi  mjini  Hannover kesho  ili  kuonesha  mshikamano  na  wahanga  wa shambulio  la  kigaidi  mjini  Paris.

Shirikisho  la  kandanda  la  Ujerumani  DFB lilifikiria kuufuta  mchezo  huo  wa  kirafiki  mjini  Hannover , lakini likaamua  kuendelea  na  mchezo  huo  ili  kutoa ujumbe wa  wazi  wakati  Ufaransa  itapambana  na  Uingereza usiku  huo mjini  London.

Rais  wa  muda  wa  shirikisho  la  kandanda  la  Ujerumani Reinhard Rauball  amesema  ujumbe  ni  wazi: "hatutatishwa  na  ugaidi."

Kikosi cha Ujerumani kupatiwa ulinzi zaidi Euro 2016

Maafisa  wa  kandanda  nchini  Ujerumani , wakati  huo huo  watafanya  mapitio  ya  usalama  katika  michuano  ya fainali  za  kombe  la  mataifa  ya  Ulaya  mwaka  2016 nchini  Ufaransa  kufuatia  mashambulizi  hayo  ya  kigaidi mjini  Paris.

Rais mwingine  wa  muda  wa  shirikisho  hilo  la  DFB rainer Koch  ameliambia  gazeti  la  Bild  leo  Jumatatu kwamba  shirikisho  hilo  litatafakari  hatua  gani  nyingine zichukuliwe.

Kikosi  cha  timu  ya  taifa  ya  Ujerumani  kililazimika kulala uwanjani  Stade de France kaskazini  mwa  Paris baada  ya  pambano  lao  la  kirafiki  dhidi  ya  Ufaransa siku  ya  Ijumaa.

Mashambulizi hatari  mjini  Paris  hayatadhuru  nafasi  za mji  huo  kuwa  mwenyeji  wa  michezo  ya  majira  ya  joto ya  Olimpiki  mwaka  2024, amesema  rais  wa   kamati  ya kimataifa  ya  Olimpiki  IOC Thomas Bach  leo.

Mji  ambao  utakuwa  mwenyeji  wa  mashindano  ya mwaka  2024, utajulikana  mwaka  2017  lakini  Bach anaamini  mashambulio  mjini  Paris , mji  ambao umetangazwa  kuwa  moja  na  miji  inayowania  kuwa mwenyeji  wa  mashindano  hayo,  hayatakuwa  na mwelekeo  wowote  katika  matokeo  ya  kura   itakayopigwa na  kamati  hiyo  ya  olimpiki.

Argentina  ni  kufa  kupona dhidi ya Columbia

Wakati  dunia  nzima  ikisimama  pamoja  na  Ufaransa baada  ya  mashambulizi  ya  kinyama  dhidi  ya  watu wasio  na  hatia  mjini  Paris  siku  ya  Ijumaa , mapambano ya  kandanda  duniani  kote  yanafanyika.

Kocha  wa  Argentina  Gerardo Martino  amesema mpambano  wa  kuwania  kufuzu  kucheza  katika  fainali za  kombe  la  dunia  mwaka  2018  nchini  Urusi , inalazimika  kushinda  licha  ya  kikosi  chake  kukumbwa na  wingi  wa  majeruhi, baada  ya   timu  hiyo  kuambulia sare  ya  bao  1-1  dhidi  ya  Brazil  iliyokuwa  na  wachezaji 10  uwanjani  baada  ya  David  Luiz  kutolewa  nje  kwa kadi nyekundu.

Argentina  inapambana  na  Colombia  kesho  katika mchezo  wa  kuwania  kufuzu  katika  fainali  za  kombe  la dunia  mwaka  2018  nchini  Urusi.

Hungary  yafanikiwa kucheza mashindano makubwa baada  ya  miaka 30

Hungary imemaliza  kipindi  cha  miaka 30  ya  kusubiri kufuzu  katika  fainali  za  mashindano  makubwa  kwa mara  ya  kwanza  tangu  mwaka  1986 ilipofikia  fainali  za kombe  la  dunia , baada  ya  kuishinda  Norway  kwa mabao  2-1 jana  Jumapili  na  kushinda  kwa  jumla  ya mabao  3-1  katika  pambano  la  mchujo  kwa  ajili  ya fainali  za  kombe  la  Ulaya  2016.

Kocha  wa  Hungary  Mjerumani Bernd Storck  akisaidiwa na  Andreas  Mueller  amelifikisha  taifa  hilo  katika  fainali za  mwakani  za  kombe  la  mataifa  ya  Ulaya. Storck amesema tulifanya  mazowezi  magumu na  kucheza  kwa nidhamu  ya  hali  ya  juu.

"Na  niliwaamini, niliwaona  wakifanya  mazowezi, tulifanya mazowezi  vizuri sana, wamejifunza  mengi, walitaka kujifunza  mengi, niliwaambia, chezeni  kwa  kujiamini, chezeni  bila  woga, na  kisha  mtafanikiwa. Na  nafikiri wamefanya  hivyo  leo. Leo mmeona. Kiwango  kilikuwa cha  kushangaza, nafikiri , ilikuwa  kiwango  cha  ajabu, kile tulichokiona  leo  kwa timu  yetu."

Mgombea  wa  kiti cha  urais wa FIFA Nakhid  akata rufaa

Na katika sakata  la  kuwania  kugombea  kiti  cha  urais wa  shirikisho  la  kandanda  duniani  FIFA , mchezaji  wa zamani  wa  kimataifa  wa  Trinidad na  Tobago  David Nakhid  amekata  rufaa  katika  mahakama  ya  juu  ya michezo  duniani  kuhusiana  na  uamuzi  wa  kumzuwia kugombea  urais  wa  shirikisho  hilo  lililokumbwa  na kashfa  la  FIFA.

Chini  ya  sheria  za  uchaguzi  za  FIFA , Nakhid  alihitaji uungwaji  mkono  kwa  maandishi  kutoka  kwa  vyama vitano  vya  taifa  vya  kandanda  ili  aweze  kugombea katika  uchaguzi  utakaofanyika  Februari  26 kutafuta  mtu atakayechukua  nafasi  ya  Sepp Blatter.

Amezuiwa  kujiandikisha  na  kamati  ya  uchaguzi  ya  FIFA mwezi  uliopita kwasababu  chama  kimoja  kilitia  saini barua  ya  kumuunga  mkono  Nakhid  pamoja  na mgombea  mwingine.

Leo (16.11.2015)mahakama  ya  upatanishi  yenye  makao yake  makuu  nchini  Uswisi  CAS imesema  Nakhid amekata  rufaa  dhidi  ya  uamuzi  huo.

Uganda yapeta kuingia awamu ya makundi

Na  katika  bara  la  Afrika , Uganda  imesonga  mbele katika  awamu  ya  makundi  kwa  ajili  ya  kuwania  kufuzu kucheza  katika  kombe  la  dunia  mwaka  2018  katika bara  la  Afrika.

Farouk Miya  mwenye umri  wa  miaka  17  alipachika  bao akiisaidia   Uganda  kuikandika  Togo  mabao  3-0.

Nahodha  Geoffrey Massa alipachika  mabao  mengine mawili  mjini  Kampala  na  kuihakikishia  Uganda  kuingia katika  awamu  ya  makundi  kwa  jumla  ya  mabao  4-0.

Zambia  pia  imesonga  mbele kwa  kuishinda  Sudan  kwa mabao  2-0  mjini  Ndola.

Licha  ya  kuwa  Jamhuri  ya  Kidemokrasi  ya  Congo ililazimishwa  sare  ya  mabao  2-2 nyumbani  na  Burundi na  Morocco  kupoteza  mchezo  wake  kwa  bao  1-0 dhidi ya  Guinea  ya  Ikweta , timu  hizo  mbili  zilizowahi  kufuzu kucheza  fainali  za  kombe  la  dunia   hapo nyuma zilitoka vifua  mbele.

Guinea , iliyolazimika  kucheza  michezo yake  katika  mji wa  Casablanca  nchini  Morocco  dhidi  ya  Namibia kutokana  na  ugonjwa  wa  Ebola , ilishinda  kwa  mabao 2-0 ikiingia  katika  mchezo  huo  na  ushindi  wa  bao 1-0 kutoka  mchezo  wa  kwanza.

Kenya  inakwenda  Cape Verde  kuwania  nafasi  hiyo katika  mchezo  utakaofanyika  kesho , baada  ya kuishinda  timu  hiyo  ya  visiwani  kwa  bao  1-0  mjini Nairobi  Ijumaa.

Nayo  Taifa  Stars  ya  tanzania  baada  ya  kuduwazwa  na sare  ya  mabao  2-2  mjini  Dar es Salaam  dhidi  ya Mbweha  wa  jangwani  Algeria, imewasili  mjini  Algiers tayari  kwa  pambano  lao  la  kuwania  kuingia  katika  duru ya  makundi  kesho  Jumanne.

Tanzania  ilikuwa  inaongoza  kwa  mabao  2-0  hadi mwishoni  mwa  kipindi  cha  pili  walipoachia fursa  hiyo adhimu  na  kuruhusu  Algeria  kurejesha  mabao  hayo mawili.

Kocha  Boniface  Mkwasa  ana  kibarua  kigumu  kuweza kuiwezesha  timu  hiyo  kuingia  katika  awamu  ya makundi licha  ya  kucheza  vizuri  katika  kipindi  cha kwanza  na  sehemu  ya  kipindi  cha  pili.

Makundi  ya  michuano  ya  CHAN yapangwa

Katika  kinyang'anyiro  cha   kombe  la  mataifa  ya  Afrika kwa  wachezaji  wa  ligi  za  ndani  maarufu  mashindano ya  CHAN , timu  zilizofuzu  kwa  michuano  hiyo zimepangwa  tayari  katika  makundi  mjini  Kigali  jana.

Wenyeji  Rwanda  wamewekwa  kundi  moja  na  Morocco na  Cote d'Ivoire. Wakati  Rwanda   haikushiriki  katika michuano  ya  mchujo  kwa  ajili  ya  mashindano  hayo , Wamorocco  na   Cote d'Ivoire  walifanya  vizuri  katika kupata  nafasi  ya  kucheza  katika  michuano  hiyo itakayojumuisha  timu  16.

Gabon  ambayo  inakamilisha  kundi  A litakalocheza michezo  yake  mjini  Kigali , itakayofanyika  kuanzia Januari  16  hadi  Februari  7 , ilichukua  njia  tofauti  kabisa hadi  kufika  hapo , ikishinda  ugenini  na  kupoteza mchezo  nyumbani  dhidi  ya  Chad.

Makundi  yamepangwa  kama  ifuatavyo ; Kundi  A , Rwanda , Gabon, Morocco  na  Cote d'Ivoire , kundi  B  lina timu  za  Jamhuri  ya  kidemokrasi  ya  Congo, Angola, Cameron  na  Ethiopia , Kundi  C ni  timu  za  ; Tunisia , Nigeria , Niger  na  Guinea  na  kundi  D  lina  timu  za Zimbabwe , Mali , Uganda  na  Zambia.

WADA  yaja juu

Na  kwa  upande  wa  riadha , shirika  la  dunia  la kupambana  na  matumizi  ya  madawa  ya  kuongeza nguvu  misuli , Doping, WADA  linatarajiwa  kutoa uamuzi dhidi  ya  shirika   la   kupambana  na  Doping  la  Urusi katika  mkutano  muhimu  mjini  Colorado  nchini  Marekani siku  ya  Jumatano ambao  utalenga  kuweka  mikakati  kwa ajili  ya  vita  dhidi  ya  Doping  duniani.

Uongozi  wa  WADA  utakutana  kutathmini  uchunguzi wao  wa  jopo  lake  huru , ambalo  limefichua  mpango mkubwa  uliokuwa  ukiungwa  mkono  na  taifa  wa  Doping nchini  Urusi  ambao  umeutumbukiza  mchezo  wa  riadha katika  mzozo  mkubwa  katika  historia.

Shirika  la  vyama  vya  riadha  duniani  IAAF  siku  ya Ijumaa  limewazuwia  wanariadha  wa  Urusi  kushiriki mashindano  ya  kimataifa, na  kuweka  ushiriki  wa wanariadha  hao  katika  michezo  ya  Olimpiki  ya  Rio de Janeiro  katika  mashaka .

Lakini  pia  shirikisho  la  kimataifa  la  vyama  vya  riadha IAAF  linaweza  kukabiliana  na uwezekano  ambao  ni pamoja  na  kuondolewa  kutoka  katika  mashindano  ya Olimpiki wakati  sehemu  ya  pili  ya  shirika  la  kupambana na  Doping  itakapowasilishwa, kwa  mujibu  wa  mmoja  wa makamishina  wa  tume  huru  ya  shirikisho  hilo.

Lakini  uamuzi  wowote  wa  kuisimamisha  IAAF kutoshiriki katika  michezo   utahitaji  kufanywa  na  kamati  maalum ya  kimataifa  ya  Olimpiki IOC.

Mwandishi: Sekione Kitojo / rtre / afpe / dpae

Mhariri: Mohammed Abdul Rahman