1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Ugaidi

Miripuko ya mabomu yatikisa Kanisa Ufilipino

Iddi Ssessanga
27 Januari 2019

Watu wasiopungua 20 wameuawa katika miripuko mwili ya mabomu Kanisani wakati wa misa ya Jumapili kusini mwa Ufilipino. Serikali imeapa kuwasaka "magaidi" waliohusika na shambulio hilo katika mkoa wenye Waislamu wengi.

https://p.dw.com/p/3CHBo
Philippinen Bomenanschlag in Jolo
Picha hii inaonyesha uharibifu uliosababishwa na miripuko kwenye kanisa la Jolo Januari 27, 2019, ambapo watu wasiopungua 18 waliuawa.Picha: picture-alliance/AP/WESMINCOM Armed Forces of the Philippines

Mabomu mawili yameripuka nje ya Kanisa wakati wa Misa ya Jumapili kusini mwa Ufilipino, na kuuawa watu 20 na kuwajeruhi wengine 77, maafisa wamesema. Bomu la kwanza liliripuka nje ya Kanisa Katoliki la Kirumi kwenye kisiwa cha Jolo katika mkoa wa Sulu, na la pili liliripuka dakika moja baadae karibu na lango kuu la kuingilia kanisani hapo.

Picha kutoka eneo la tukio zilionyesha mlango, mabenchi ya kanisani na madirisha ya vioo vya Kanisa la Mount Camel vikiwa vimevunjwa vunjwa, na miili ikiwa imetapakaa chini, alisema mpiga picha wa shirika la habari la Ufaransa AFP.

Msemaji wa Rais Rodrigo Duterte amelaani tukio hilo alilolitaja kuwa "kitendo cha ugaidi na mauaji." "Lengo kwa uhakika ni .... ugaidi. Hawa ni watu wasiopenda amani," msemaji wa jeshi kwenye mkoa huo Luteni Kanali Gerry Besana aliliambia  shirika la habari la AFP.

Alisema wachunguzi walikuwa wanajaribu kubaini aina ya vilipuzi vilivyotumiwa katika shambulio hilo ili kusaidia kuwabaini washukiwa. Hakuna kundi lililodai kuhusika na shambulizi hilo ambalo limegharimu maisha ya wanajeshi na pia raia.

Philippinen Bomenanschlag auf Kirche in Jolo
Maafisa wa polisi na jeshi wakiwa mbele ya Kanisa Katoliki ambako miripuko ya mabomu ilitokea, kijiji cha Jolo, mkoani Sulu kwenye kisiwa cha kusini mwa Ufilipino cha Mindanao.Picha: Getty Images/AFP/N. Butlangan

Makubaliano ya utawala wa ndani kwa Waislamu

Miripuko hiyo pacha imetokea karibu wiki moja baada ya Waislamu wachache katika taifa hilo lenye Wakatoliki wengi, kupiga kura kuunga mkono  utawala  wa ndani  katika mkoa wao kusini mwa Ufilipino.

Kuundwa kwa mkoa wa Bangsamoro wenye utawala wake wa mdani kwa  Waislamu wa Mindanao, ilikuwa sehemu ya makubaliano ya amani ya 2014 kati ya serikali ya Ufilipino na kundi la wapiganaji wa chini kwa chini la Moro Islamic Liberation Front (MILF), ambalo ndiyo kundi kubwa zaidi la waasi.

Ingawa maeneo mengi zaidi ya Waislamu yaliidhinisha makubaliano hayo ya kuwa na utawala wa ndani, wapigakura katika mkoa wa Sulu, iliko Jolo waliyakataa. Kisiwa cha Jolo kimekuwa ngome ya Abu Sayyaf, kundi la Kiislamu lenye itikadi kali lililoorodheshwa kama kundi la kigaidi na Marekani na Ufilipino.

Kundi hilo linafahamika kwa kufanya mashambulizi ya mabomu, maauwaji na utekaji nyara. Waziri wa ulinzi Delfin Lorenzana ameamuru usalama uimarishwe mkoani kote, wakati kukiwa na wasiwasi wa kutokea mashambulio zaidi.

"Nimeviagiza vikosi vyetu kuzidisha hali ya tahadhari, kuweka ulinzi kwenye maeneo yote ya ibada na ya umma mara moja, na kuanzisha hatua madhubuti za kiusalama ili kuzuwia mipango ya uadui."

Mwandishi: Iddi Ssessanga/DW

Mhariri: Oummilkheir Hamidou