1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Misri: Polisi wapambana na waandamanaji

Zainab Aziz Mhariri: Tatu Karema
22 Septemba 2019

Vikosi vya usalama nchini Misri vimepambana na waandamanaji wanaompinga Rais Abdel Fatah al-Sisi katika mji wa bandari wa Suez. Polisi walitumia gesi ya kutoa machozi pamoja na risasi za moto dhidi ya waandamanaji.

https://p.dw.com/p/3Q1v1
Ägypten Kairo | Anti-Regierungsproteste
Picha: Getty Images/AFP

Maandamano yamefanyika katika miji kadhaa ya kumtaka Rais Abdel Fattah al-Sisi aondoke madarakani. Maandamano kama haya ni nadra baada ya Misri kuweka amri yakupiga marufuku maandamano chini ya sheria iliyopitishwa mnamo mwaka 2013 baada ya kuondolewa madarakani kufuatia kuondolewa madarakani na wanajeshi wa Rais wa zamani Mohamed Morsi.

Hali ya kutoridhika imeongezeka kutokana na kupanda kwa bei ya bidhaa nchini Misri, ambapo serikali ya al- Sissi imechukua hatua kali za kubana matumizi tangu mwaka 2016 kama sehemu ya kukabiliana na mkopo wa dola bilioni 12 kutoka shirika la Fedha la Kimataifa IMF.

Karibu kila mtu mmoja wa raia wa watatu wa Misri anaishi chini ya kiwango cha kimataifa cha umaskini kilichowekwa. Watu hao wanajikimu kwa kutumia chini ya dola 1.40 kwa siku, kulingana na takwimu rasmi iliyotolewa mnamo mwezi Julai.

Rais wa Misri Abdel Fattah al-Sisi
Rais wa Misri Abdel Fattah al-SisiPicha: Getty Images/AFP/B. R. Smith

Mnamo siku ya Jumamosi waandamanaji walikusanyika kuelekea katikati ya jiji la Suez ikiwa ni siku ya pili mfululizo, ambapo walikabiliwa na vikosi vya usalama vilivyozuia barabara kwa vifaru vya kijeshi. Chanzo kimoja kimeliambia shirika la habari la AFP kwamba karibu watu 74 walikamatwa katika mji mkuu Cairo.

Maandamano hayo yalifanyika baada ya Mohamed Aly, mfanyabiashara aliye uhamishoni na mpinzani wa  Rais al-Sisi kuposti mtandaoni wito wa kuwataka watu waandamane kumpinga kiongozi huyo wa Misri.

Mkandarasi huyo wa ujenzi amekuwa akichapisha video ambazo zimezagaa katika mitandao ya kijamii tangu mwanzoni mwa mwezi wa Septemba, akimtuhumu Rais wa Misri Abdel Fatah al-Sissi na jeshi kwa kuhusika rushwa iliyoenea nchini humo. Rais al Sisi alikanusha madai hayo wiki iliyopita, akisema kuwa yeye ni muadilifu na mwaminifu kwa watu wake na jeshi la nchi yake.

Kundi la kimataifa la kutetea haki za binadamu Human Rights Watch limetoa wito kwa serikali nchini Misri kulinda haki ya watu wanaoandamana kwa amani na kuwaachilia mara moja wale waliozuiwa.

Vyanzo/APE/AFPE