1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mjumbe wa Marekani ziarani Mashariki ya Kati

P.Martin - (AFPE)26 Februari 2009

Mjumbe maalum wa Marekani katika Mashariki ya Kati George Mitchell, akiendelea na ziara yake katika kanda hiyo, anakutana na wanasiasa wa Kiisraeli mjini Tel Aviv kuijadili hali ya Ukanda wa Gaza.

https://p.dw.com/p/H1xp
Der neue US-Nahost-Vermittler George Mitchell wird in den kommenden Tagen zu einem Besuch in der Region erwartet
George Mitchell,mjumbe maalum wa Marekani katika Mashariki ya Kati.Picha: AP / DW

Mjumbe huyo wa Rais wa Marekani Barack Obama,anajaribu kuufufua mchakato wa amani uliokwama.Kabla ya kukutana na George Mitchell mjini Tel Aviv,Waziri wa Mambo ya Nje wa Israel Tzipi Livni anaeondoka madarakani aliwaambia waandishi wa habari,majadiliano yao yatahusika na hali ya Gaza.Amesema,Israel inaamini kuna haja ya kusaidia upande wa mahitaji ya kiutu na kutafuta njia ya kukidhi mahitaji hayo bila ya kuimarisha kundi la Hamas linalodhibiti Gaza.

Mitchell amepanga kukutana na Benjamin Netanyahu wa chama cha Likud cha mrengo wa kulia aliepewa dhamana ya kuunda serikali mpya nchini Israel.Vile vile anakutana na Waziri Mkuu Ehud Olmert na Waziri wa Ulinzi Ehud Barak wanaoondoka madarakani kufuatia uchaguzi uliofanywa mapema mwezi huu.George Mitchell,aliesaidia kutayarisha makubaliano yaliyopelekea amani kupatikana Ireland ya Kaskazini,vile vile atakutana na Rais wa Wapalestina Mahmoud Abbas na Waziri Mkuu Salam Fayyad siku ya Ijumaa.

Ziara ya George Mitchell inatangulia mkutano wa kimataifa kusaidia kujenga upya Ukanda wa Gaza.Mkutano huo wa wafadhili utaanza siku ya Jumatatu katika mji wa mapumziko Sharm el-Sheikh nchini Misri na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Hillary Clinton pia anatazamiwa kuhudhuria mkutano huo.Baadae,Clinton amepanga kwenda Israel na Ukingo wa Magharibi uliokaliwa na Israel.

Rais Obama ameahidi kushughulikia kwa dhati mgogoro wa Mashariki ya Kati katika jitahada ya kufufua majadiliano ya amani kati ya Waisraeli na Wapalestina.Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Israel,Mitchell anatazamia kukodi ofisi mjini Jerusalem kwa matumaini kuwa atatembelea kanda hiyo kila mwezi.Majadiliano ya amani yamekwama tangu Israel kuanzisha vita vyake vya siku 22 katika Ukanda wa Gaza kujibu mashambulio ya makombora ya wanamgambo wa Hamas.Vita hivyo vimeua zaidi ya Wapalestina 1,300 na Waisraeli 13.

Mjumbe wa Rais Obama kabla ya Israel alikuwepo Uturuki na alikutana na Waziri Mkuu Tayyip Erdogan.Baadae,Mitchell alisema Uturuki ni mshirika muhimu wa Marekani na ina dhima maalum katika jitahada za kutafuta amani katika Mashariki ya Kati.Uturuki pia ni mshirika mkuu wa Israel katika kand hiyo tangu makubaliano ya kushirkiana kijeshi kutiwa saini mwaka 1996. Lakini hali ya mvutano ilizuka kati ya nchi hizo mbili baada ya Uturuki kukosoa vikali operesheni ya kijeshi ya Israel iliosababisha umwagaji mkubwa wa damu katika Ukanda wa Gaza mwezi uliopita.