1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa baraza la haki za binaadam wafunguliwa Geneva

Oumilkheir Hamidou
27 Februari 2017

Mkutano wa baraza la Haki za Binaadamu umefunguliwa mjini Geneva Uswisi. Mada kuu zinazotazamiwa kujadiliwa ni uvunjwaji wa haki za binaadamu katika sehemu tofauti za dunia.

https://p.dw.com/p/2YKOr
Schweiz Genf Antonio Guterres
Picha: picture-alliance/AP Photo/S. Di Nolfi

 

Baraza hilo lenye wanachama 47 linapanga kuzungumzia masuala kuhusu Palastina, Myanmar, Korea ya kaskazini, SriLanka na Sudan Kusini. Wajumbe zaidi ya mia moja wanatarajiwa kuhutubia mkutano huo utakaoendelea hadi marchi 24 mjini Geneva. Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alikuwa wa mwanzo kuhutubia mkutano huo. Aliitaja  kuwa ni heshima na taadhima kubwa kwake kupata fursa ya kuhutubia mkutano huo. Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa ameendelea kusema: "Ni hishma kubwa kwangu kuhutubia mbele ya baraza la haki za binaadam. Miaka kumi iliyopita, pengine mlikuwa mkinijua kama mkuu wa halmashauri kuu. Hii ni fursa kubwa kwangu kuwa pamoja nanyi kwa mara ya kwanza, nikiwa katibu mkuu wa Umoja wa mataifa. Nimefika kutoa shukurani zangu na nimefika katika wakati wa dharura. Hali ya haki za binaadam  imegeuka kuwa ugonjwa na ni ugonjwav unaoenea kaskazini, kusini, mashariki na magharibi. Baraza la haki za binaadam linabidi ligeuke sehemu ya tiba."

Nembo ya shirika linalopigania haki za binaadam la Marekani Human Rights Watch
Nembo ya shirika linalopigania haki za binaadam la Marekani Human Rights WatchPicha: Getty Images/AFP/J. Macdougall

Haki za wahamiaji ziko matatani anasema Guterres

Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa Antonio Guterres ameelezea pia wasi wasi wake kutokana na kuchipuka hisia za uzalendo la siasa kali, hisia anazosema zinachochea chuki dhidi ya wageni, chuki dhidi ya wayahudi na chuki dhidi ya uislam, miongoni mwa mengineyo."Haki za wakimbizi na wahamiaji ziko mashakani. Na kutokana na mikururo ya watu wanaokimbia vita, jumuia ya kimataifa haiwezi kujitenga na majukumu yake."Amesisitiza katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres.

Kwa upande wake mwenyekiti wa halmashauri ya haki za binaadam Zeid Raad Al Hussein ametahadharisha dhidi ya wale aliowaita "wadau wa kisiasa wanaotishia mfumo unaohusisha pande tofauti au wenye azma ya kujitoa katika baadhi ya sekta za mfumo huo."Hatutokaa kitako, haki zetu, haki za wenzetu, mustakbali wa sayari yetu, haviwezi, havistahiki kuwekwa kando na wenye kujipendelea kisiasa."Amesema Zeid Raad Al Hussein.

 Jumuia ya kimataifa ipiganie ufumbuzi wa madola mawili

Kiongozi wa utawala wa ndani wa Palastina Mahmoud Abbas
Kiongozi wa utawala wa ndani wa Palastina Mahmoud AbbasPicha: picture-alliance/abaca

Kiongozi wa mamlaka ya wapalastina Mahmoud Abbas ameihimiza jumuia ya kimataifa itetee ufumbuzi wa madola mawili katika hotuba yake inayoangaliwa kuwa ni wito pia kwa Israel na utawala mpya wa Marekani. Mahmoud Abbas ameyatolea wito mataifa yanayounga mkono ufumbuzi wa madola mawili kuwa wakili wa njia hiyo na kulitambua taifa la wapalastina."Ufumbuzi wa madola mawili unabidi uhifadhiwe dhidi ya njama yoyote ya kujitenga na ufumbuzi huo au kutoutilia maanani."Amesistita.

Mahmpoud Abbas amekosoa ujenzi wa makaazi mepya ya wayahudi katika ardhi za wapalastina na kuonya dhidi ya kuihamishiwa ofisi za mabalozin wa nchi za nje mjini Jerusalem.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AP/AFP

Mhariri:Yusuf Saumu