1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa Copenhagen waingia katika duru muhimu

Sekione Kitojo15 Desemba 2009

Katibu mkuu wa umoja wa mataifa Ban Ki-moon anaelekea mjini Copenhagen kuhudhuria mkutano wa umoja wa mataifa wa mabadiliko ya hali ya hewa.

https://p.dw.com/p/L2Ug
Katibu mkuu wa umoja wa mataifa Ban ki-Moon anaelekea mjini Copenhagen kwa ajili ya mkutano wa umoja wa mataifa wa hali ya hewa.Picha: AP

Katibu mkuu wa umoja wa mataifa ameonya leo kuwa wajumbe katika majadiliano ya mabadiliko ya hali ya hewa mjini Copenhagen wanakabiliwa na tatizo la muda kwenda mbio katika kuzuwia mkutano huo kumalizika kwa kushindwa baada ya mataifa yanayoendelea kujitoa katika mazungumzo hayo kwa muda wa saa tano jana. Katibu mkuu anaelekea leo mjini Copenhagen kuhudhuria mazungumzo hayo.

Mkutano huo unaochukua siku kumi na mbili uliingia katika hali ya mvutano mkubwa wakati nchi inayochafua zaidi hali ya hewa duniani China , ikizishutumu nchi za magharibi kwa kufanya ujanja na kujaribu kuilaumu kwa kushindwa kwa aina yoyote kwa mkutano wa Cpenhagen kufikia makubaliano ya kupambana na kupanda kwa ujoto duniani.

Rais wa Marekani Barack Obama, ambaye nchi yake ni ya pili kwa utoaji wa gesi zinazoharibu mazingira duniani , amesema kuwa anataka makubaliano ambayo yanaweka hatua muhimu.

Lakini mawaziri wamekiri kuwa wanapaswa kuanza kupiga hatua kubwa kabla ya Obama na kiasi viongozi wengine 120 wa taifa na serikali kukusanyika kwa ajili ya mkutano wa kilele katika mazungumzo hayo. Muda unakimbia, katibu mkuu Ban Ki-moon amewaambia waandishi habari mjini New York kabla ya kuondoka kuelekea mjini Copenhagen.

Iwapo kila kitu kitaachiwa viongozi wakitatue dakika za mwisho, kuna hatari ya kupatikana makubaliano dhaifu ama kutopata makubaliano kabisa. Na hii itakuwa kushindwa katika kiwango cha maafa.

Mkutano huo uliingia katika mtikisiko mkubwa jana Jumatatu wakati wajumbe wa bara la Afrika waliongoza ususiaji wa makundi ya utendaji ya mataifa yanayoendelea, na kurejea baada ya kupata uhakikisho kuwa mkutano huo hautaweka kando mazungumzo juu ya hali ya baadaye ya mkataba wa Kyoto.

Mjuumbe wa Nigeria katika mazungumzo hayo ya Copenhagen Victor Fodeke amelalamika kuwa mataifa tajiri yanaitenga kando Afrika.

Afrika imehukumiwa kifo. Na Afrika imewekwa kando na baadhi ya mataifa kwa kutotaka kuzungumzia lolote kuhusu mkataba wa Kyoto, hiki ndio chombo kinacholazimisha upunguzaji wa gesi zinazoharibu mazingira. Tunatarajia kuwa mji wa matumaini wa Copenhagen, hautakuwa matumaini yaliyopotea kwa mataifa yanayoendelea.

Mkataba huo wa Kyoto wa mwaka 1997 unaoweka viwango vya upunguzaji wa utoaji wa gesi zinazoharibu mazingira , ambao hauijumuishi Marekani , unazifunga nchi tajiri ambazo zimeuidhinisha kupunguza utoaji wa gesi , lakini sio nchi zinazoendelea.

China imezishutumu nchi zilizoendelea kwa kurudi nyuma katika majukumu yao ya kupambana na mabadiliko ya hali ya hewa na kuonya kuwa mkutano wa umoja wa mataifa wa hali ya hewa mjini Copenhagen umeingia katika duru ya umakinifu.

Klimagipfel Copenhagen Proteste
Waandamanaji wakiandamana karibu na eneo la mkutano wa hali ya hewa mjini Copenhagen .Picha: AP

Wakati huo huo polisi wa Denmark wamesema leo Jumanne kuwa wamewakamata kiasi watu 200 na kutumia mabomu ya gesi ya kutoa machozi usiku dhidi ya makundi ya waandamanaji katika mkutano huo wa umoja wa mataifa unaojadili mabadiliko ya hali ya hewa mjini Copenhagen. Wengi wa waandamanaji waliachiliwa baadaye lakini watu watano bado wanashikiliwa na polisi na huenda wakafikishwa mahakamani kwa madai ya kumshambulia afisa wa polisi. Tangu Jumamosi polsi wamewakamata waandamanaji 1,300 katika mkutano huo, lakini wengi wamekwisha achiliwa huru.

Mwandishi: Sekione Kitojo/ AFPE / DPAE

Mhariri: Abdul-Rahman