1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa madola sita makuu kuhusu Iran

Hamidou, Oumilkher22 Januari 2008

Mawaziri wa mambo ya nchi za nje wa mataifa matano yenye kura ya turufu ndani ya baraza la usalama na Ujerumani unafnyika mjini Berlin

https://p.dw.com/p/Cw5L
Waziri wa mambo ya nchi za anje wa Ujerumani akiamkiana na mwenzake wa China mjini BerlinPicha: AP




Wawakilishi wa madola matano yenye kura ya turufu ndani ya baraza la usalama la umoja wa mataifa,na wa Ujerumani wanakutana mjini Berlin kuandaa azimio jipya kwa lengo la kuishawishi Iran iachane na mpango wa kinuklea wa matumizi ya kijeshi.


Lengo la mkutano wa Berlin ni kujadili njia inayobidi kufuatwa na kutathmini zimefikia wapi juhudi za mataifa matano yenye kura ya turufu ndani ya baraza la usalama na Ujerumani katika kuitanabahisha Iran iachilie mbali mpango wake wa kurutubisha maadini ya Uranium na kurejea katika meza ya mazungumzo.


Iran inakanusha dhana kwamba mpango wake wa kurutubisha maadini ya Uranium,inaouendeleza bila ya kujali vikwazo vya kimataifa,umelengwa kutengeneza silaha za kinuklea.


"Nnaamini moja kwa moja tutaondoka na matokeo na tutaionyesha kwa mara nyengine tena Iran kwamba hofu zetu ziko pale pale" amesema hayo waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinemeier kupitia kituo cha kwanza cha televisheni ya Ujerumani ARD hii leo.


Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani ameendelea kusema:


"Kwanza nnabidi kusema nimefurahi kuona mawaziri wa mambo ya nchi za nje kutoka nchi zote sita wanahudhuria mkutano huu.Tunachobidi kufanya kwasasa ni kuiidhihirishia Iran msimamo wa jumuia ya kimataifa ni mmoja na uko vile vile."


Kwa mujibu wa duru za kidiplomasia mjini Paris,madola hayo sita makuu:Ujerumani,Uchina,Marekani,Ufaransa,Uengereza,na Urusi yanapanga kuwasilisha mswaada wa azimio mbele ya baraza la usalama la umoja wa mataifa unao shauri Iran iwekewe vikwao.


Hata hivyo waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani bibi Condoleezza Rice amesema bado kuna vifungu vinavyozusha mabishano.


Hadi wakati huu Moscow na Beijing zimekua zikipinga fikra yoyote ya kuwekewa vikwazo Teheran ili kuitanabahisha iache kurutubisha maadini ya Uranium na kubainisha kwamba mpango wake una malengo ya amani na sio ya kijeshi.


Mjini Teheran msemaji wa serikali amesema hii leo nchi yake haitositisha harakati zake za kinuklea hata kama itawekewa vikwazo vipya na baraza la usalama.


Iran inatetea haki yake ya kutengeneza nishati ya atomiki kwa matumizi ya amani.Madola makuu lakini yanaituhumu kutaka kujitengenezea kisiri siri sailaha za kinuklea.


Iran inahisi hakuna sababu ya kuingilia kati baraza la usalama katika wakati ambapo wanazungumza moja kwa moja na shirika la kimataifa la nguvu za atomiki.


Mwenyekiti wa shirika hilo Mohammed el Baradei amesema january 13 iliyopita,wamekubaliana muda wa wiki nne pamoja na Teheran ili kuyapatia jibu masuala yote yaliyosalia kuhusu mradi wake wa kinuklea.


Ripoti ya idara za upelelezi za Marekani iliyochapishwa mwezi December mwaka jana,inasema Iran imesitisha mpango wa kutengeneza silaha za kinuklea tangu mwaka 2003.






►◄