1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Moise Katumbi amtambua Felix Tshisekedi kama rais wa DRC

Saleh Mwanamilongo (Mhariri: Saumu Mwasimba)27 Februari 2019

Chama cha upinzani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo cha Moise Katumbi kimemtambua rais Felix Tshisekedi kuwa rais halali wa nchi hiyo. Chama hicho kiko kwenye muungano wa LAMUKA uliomuunga mkono Martin Fayulu.

https://p.dw.com/p/3EAbh
Ruanda Kigali - Moise Katumbi Chapwe bei der Mo Ibrahim Award
Picha: DW/E. Topona

Mwanasiasa wa upinzani Moise Katumbi na chama chake cha ENSEMBLE wamemtambua Felix Tshisekedi kama rais wa Kongo ,na kumtolea mwito wa kutia juhudi za kisiasa  kumaliza  mgogoro wa uhalali wa madaraka. Hatua hiyo ya Katumbi inazusha maswali kuhusu hatma ya vuguvugu la LAMUKA ambalo lilikuwa likimuunga mkono mpinzani Martin Fayulu anaedai kuwa mshindi wa uchaguzi wa rais.

Kwenye mkutano na wandishi habari ,naibu mwenyekiti wa muungano wa vyama vinavyopigania mabadiliko vinavyomuunga mkono Moise Katumbi, ENSEMBLE POUR LE CHANGEMENT amesema kwamba kampeni ya kutaka kueko na ukweli wa matokeo ya uchaguzi imekuwa ni kitendawili kwa hiyo ni lazima kuweko mtizamo mpya kuhusu ujio wa taifa la Kongo : " Tuko katika hali ambayo haitabadilika tena, naomba tuwe na mtizamo wa mambo ulio imara.Mbali na kutetea ukweli wa matokeo ya uchaguzi naomba tuendeshe kwanza vita vya kisiasa kwa ajili ya kuweko na taifa la haki."

Kwa sasa ENSEMBLE POUR LE CHANGEMENT imejipanga kuendesha upinzani dhidi ya rais Felix Tshisekedi. Na lengo kubwa ni kutaka Moise Katumbi kiongozi wake arejee nchini.

Ensemble inaviti 163 bungeni na kwenye bunge la majimbo, kundi hilo limeoneka kuwa na wingi wa viti kuliko makundi mengine yote ya upinzani. Kwa hiyo kikatiba Moise katumbi ananafasi kubwa kuteuliwa kuwa msemaji wa upinzani nchini.

Rais wa DRC, Felix Tshisekedi alichukua hatamu za uongozi mnamo 24.01.2019 kutoka kwa aliyekuwa rais wa muda mrefu Joseph Kabila.
Rais wa DRC, Felix Tshisekedi alichukua hatamu za uongozi mnamo 24.01.2019 kutoka kwa aliyekuwa rais wa muda mrefu Joseph Kabila.Picha: picture-alliance/AP Photo/J. Delay

Msimamo huo wa kumtambua Felix Tshisekedi kama rais wa Kongo, unaizima  ndoto ya mpinzani Martin fayulu ambae aliungwa mkono na Moise Katumbi na Jeanpierre Bemba kwenye uchaguzi wa desemba 30. Fayulu anaendelea na kampeni yake ya kudai  ukweli wa matokeo ya uchaguzi ambayo amesema yalimpa ushindi.

Hata hivyo Ensemble imeweka masharti kadhaa kabla ya kuweko na ushirikiano wowote na rais Tshisekedi, moja wapo ni kuachiwa huru kwa wafungwa wote wa kisiasa na kuruhusu warejee nchini wapinzani wanaoishi uhamishoni.

ENSEMBLE pour LE CHANGEMENT inaomba pia kutokuweko na ushawishi wa kisaisa wa rais mustaafu Joseph Kabila kwenye taasisi za kitaifa.

Pendekezo hilo limepingwa na wanachama wa chama cha FCC cha Joseph kabila. Aime Kilolo ni msemaji wa FCC , amekosoa pendekezo hilo la upinzani :

" Tunaomba tukumbushe kwamba rais kabila ndie kiongozi wa FCC,ushawishi wake utaendelea kuwa mkubwa kutokana na kwamba ni chama chake kilicho na wingi wa viti bungeni "

Wakati hayo yaliendelea rais Felix Tshisekedi anaendelea na ziara yake ya siku mbili mjini Windoek,Namibia ambayo ni ziara ya kwanza kwa taifa hilo la kusini mwa afrika toka achaguliwe kuwa rais.