1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mpango wa FIFA na CAF kuwasilishwa mahakamani

Bruce Amani
22 Julai 2019

Mpango wa shirikisho la kandanda duniani – FIFA kuchukua mikoba ya uendeshwaji wa kandanda la Afrika unatarajiwa kukumbwa na kizuizi.

https://p.dw.com/p/3MXlq
Grindel und Infantino gemeinsam auf der Ehrentribüne
Picha: picture-alliance/Pressefoto ULMER/M.Ulmer

Hii ni kwa sababu kuna mwanachama mmoja wa kamati kuu ya Shirikisho la Kandanda Afrika – CAF anayesema kuwa atakwenda mahakamani kupinga uamuzi huo.

Hasan Bility, kutoka Liberia na ambaye amekuwa mwanachama wa kamati kuu ya CAF kwa miaka miwili iliyopita, amesema ataiomba mahakama ya upatanishi katika michezo yenye makao yake nchini Uswisi kutangaza kuwa batili makubaliano ambayo Katibu Mkuu wa FIFA Fatma Samoura atatumwa kwenda kulifanyia mageuzi shirikisho la kandanda Afrika.

69. Fifa-Kongress in Paris | Infantino und Fatma Samoura
Fatma Samoura kuongoza shughuli za CAF kwa miezi sitaPicha: AFP/F. Fife

Bility pia amesema ataitaka mahakama hiyo kuilazimisha CAF kuanzisha ukaguzi wa mahesabu yake ambayo amesema kamati kuu awali ilikubali lakini rais wa CAF Ahmad Ahmad akayakwamisha. Akizungumza wiki iliyopita katika mkutano wa baraza kuu la CAF mjini Cairo, Ahmad aliutetea uamuzi wa kuomba msaada wa FIFA katika uendeshwaji wa maswala yake "Wengi wenu bado hamjaelewa maana kamili ya vitendo vyangu kuhusiana na FIFA. Mimi mwenyewe nimelelewa Kiafrika kwa sababu nililelewa na babu na bibi yangu. Wakati nikiwa na matatizo nyumbani, kwanza lazima niwatafute wazazi wangu. Nani nitawasiliana naye kama nina tatizo kubwa na CAF? Au tumebadilisha mtazamo wetu kuwa FIFA sio shirikisho linalosimamia kandanda? Kwangu mimi ndilo shirikisho linalotuongoza sisi CAF. Ilibidi niiombe FIFA msaada.

CAF ipo katikati ya mgogoro kufuatia tuhuma za rushwa dhidi ya Ahmad ambazo anakanusha.

Infantino wiki iliyopita alidai kuwa hatua hiyo isiyo ya kawaida ya afisa wa FIFA kusimamia kandanda la Afrika itaimarisha pakubwa mchezo wa kandanda barani Ulaya "Na tumekuwa tukifanya kazi pamoja, katika miaka miaka mitatu iliyopita na tumefanikisha mengi katika FIFA na Fatma Samoura. Nini zaidi tunachoweza kufanya katika FIFA, kuliko kumtuma mtawala wetu mkuu na timu ya watalaamu kwenda Afrika kusiadia? Nimekuwa nikisikia kuhusu ukoloni, kwamba FIFA inaitawala Afrika tena. Wakati Fatma Samoura aliteuliwa katibu mkuu wa FUFA, sikusikua Afrika inaitawala FIFA. Nini maana ya ukoloni? sijui. sio sehemu ya msamiati wangu.

FIFA imeliambia leo shirika la habari la Reuters kuwa haina cha kuongezea kwa muongozo wa mpango wa kulisaidia kandanda la Afrika.