Mpango wa serikali ya Marekani kuokoa benki zilizo hatarini
19 Septemba 2008Pendekezo mojawapo ni kuundwa kwa shirika maalum la kiserikali kwa azma ya kuokoa mashirika ya fedha yaliyo matatani.Mzozo wa fedha unaoshuhudiwa hivi sasa kote duniani ni mkubwa kabisa kupata kutokea tangu ule msukosuko wa mwaka 1929 uliosababisha janga kubwa duniani baada ya makampuni kufilisika kwa mamia na mamilioni ya watu kukosa ajira.Sasa tena masoko ya fedha yamevurugika.Bila shaka kuna makosa yaliyofanywa na yanayohitaji kurekebishwa.
Sasa ndio serikali na Benki Kuu ya Marekani kwa utulivu zinaokoa benki na mashirika ya bima ili kuzuia maafa makubwa katika masoko ya fedha kote duniani.Kwa hivyo shirika kubwa kabisa la bima duniani AIG lenye zaidi ya wateja milioni 100 katika nchi 130 limeokolewa kwa kutaifishwa na serikali.Iwapo lingeachiwa kufilisika,basi mamilioni ya Wamarekani waliokuwa na bima wangepoteza malipo ya uzeeni.Si hilo tu kwani AIG ni shirika linalotoa bima kwa benki kote duniani.Kwa hivyo kufilisika kwa AIG kungesababisha maafa makubwa katika mifumo ya fedha duniani.Kwa upande mwingine kufilisika kwa benki ya uwekezaji ya Lehman Brothers iliweza kustahmiliwa licha ya kuumiza. Benki ya Lehman Brothers ilikuwa ya tatu kwa ukubwa miongoni mwa benki za uwekezaji nchini Marekani.
Ingawa kuna wasi wasi mkubwa katika masoko ya fedha wakati hisa zikipanda na zikishuka,serikali na benki kuu zinachukua hatua kwa utulivu. Sarafu mbali mbali zinamiminwa kwa mabilioni katika masoko ya fedha ili mfumo wa fedha uweze kufanya kazi.Wakati huo huo Waziri wa Fedha wa Marekani Henry Paulson na Rais wa Benki Kuu Ben Bernanke wanapendekeza pia kuundwa kwa shirika litakaloshughulikia mikopo mibaya na hisa za kubahatisha ambazo hivi sasa zinahatarisha uhai wa benki nyingi na hata kuzitia katika kitisho cha kufilisika.
Kwa maneno mengine,serikali inajitokeza kama mwokozi.Muda mfupi tu baada ya habari hiyo kuchomoza,bei za hisa ziliongezeka kwa kiwango kikubwa.Baada ya faida iliyopatikana kutiwa katika mifuko binafsi,sasa umma ndio unabebeshwa mzigo wa hasara iliyosababishwa na masoko ya fedha.Mashirika hayo yapo tayari kabisa kuokolewa lakini hupinga kufanyiwa marekebisho katika mfumo wao.Lakini pasipo na usimamizi mkali na marekebisho,basi uokozi wa serikali ni sawa na kupanda mbegu ya mzozo mwingine katika masoko ya fedha.