1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Msiba nchini Libnan baada ya jenerali Al Hajj kuuliwa

Oummilkheir14 Desemba 2007

Walimwengu walaani mauwaji nchini Libnan na Syria yatakiwa iache kushawishi mambo nchini humo

https://p.dw.com/p/CbaY
Jenerali Francois el HajjPicha: AP

Msiba umeigubika Libnan ,nchi inayojiandaa kwa mazishi ya jenerali Francois el-Hajj,aliyeuliwa jumatano iliyopita,gari moja liliporipuliwa karibu na Beyrouth.Rais George W. Bush amekosoa ushawishi wa Syria nchini Libnan.

Bila ya kujali mvua kali inayonyesha Beyrouth,jeneza la afisa huyo wa ngazi ya juu wa kijeshi,likifunikwa bendera ya Libnan lilibebwa alfajiri ya leo toa jumba la maiti hadi nyumbani kwake mjini Baabda,kitongoji cha mji mkuu Beyrouth wanakoishi waumini wengi wa kikristo-kabla ya ya mazishi rasmi .

Ibada ya maiti itafanyika katika kanisa kuu la Harissa,kaskazini mashariki ya Bayrouth kabla ya maiti ya jenerali huyo kuzikwa katika mji alikozaliwa huko Rmeich,eneo la kusini mwa Libnan linalopakana na Israel.

Leo ni siku ya msiba wa taifa nchini Libnan na shule na vyuo vikuu vimefungwa.

Jenerali Francois el Hajj, aliyekua akiongoza opereshini za jeshi alikua mshirika mkubwa wa kiongozi wa vikosi vya wanajeshi vya Libnan Michel Suleiman,anaepewa nafasi nzuri ya kuteuliwa kua rais wa Libnan.Jenerali Francois el Hajj aliyekua na umri wa miaka 54 ameuliwa pamoja na mlinzi wake jumatano iliyopita mjini Baabda.

Mauwaji hayo yaliyolaaniwa na ulimwengu mzima ni ya mwisho katika mlolongo wa mashambulio yaliyoanza mwaka 2004 dhidi ya wanasiasa wanaoipinga Syria-na kugharimu maisha ya wanasiasa wanane-ikiwa ni oamoja na waziri mkuu wa zamani Rafic Hariri aliyeuliwa february mwaka 2005.

Rais George W.Bush wa Marekani amelaa ni vikali mauwaji hayo.Katika taarifa yake rais Bush amesema pia anataraji ushawishi wa Syria utakoma nchini Libnan.

Rais George W. Bush amesema tunanukuu:”Katika wakati ambapo Libnan inajitahidi kujitafutia rais kwa kufuata misingi ya kidemokrasia na kuambatana na katiba,ushawishi wa Syria na washirika wake,wenye lengo la kuwatisha walibnan,unabidi ukome.”Mwisho wa kumnukuu rais Bush,ambae safari hii hakuifungamanisha Syria moja kwa moja na kuuliwa jenerali Francois el Hajj.

Hata msemaji wa ikulu ya Marekani Dana Perino amekiri aliposema tunanukuu:“Bado hatujafikia daraja hiyo.“Mwisho wa kumnukuu.

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani Condoleezza Rice amezungumza kwa simu na waziri mkuu wa Libnan Fouad Siniora,kumpa salam zake za rambi rambi na “kumhakikishia uungaji mkono wa marekani katika juhudi za walio wengi za kuteuliwa rais.

Msemaji wake Sean McCormark amekitaja kisa cha kuuliwa jenerali Francois el Hajj kua ni “cha kustaajabisha”.Sean McCormark ameongeza kusema hawajui sababu za mauwaji hayo wala hawajui nani yuko nyuma.

Mauwaji haya yamejiri katika wakati ambapo upande wa upinzani unaoungwa mkono na Syria na wabunge walio wengi wanaoipinga Syria,wanazozana bado kuhusu utaratibu wa kuifanyia marekebisho katiba ili jenerali Michel Suleiman aweze kuchaguliwa kua rais –wanazozana pia juu ya namna ya kuunda serikali mpya ya nchi hiyo.Marehemu Fracois el Hajj alipewa nafasi nzuri ya kuuwa mkuu wa vikosi vya wanajeshi pindi jeneral Sleiman akiteuliwa kua rais wa Libnan.