1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Muda unayoyoma kwa Afrika Kusini kusuluhisha Zimbabwe

Mohamed Dahman24 Aprili 2007

Muda unayoyoma kwa serikali ya Afrika Kusini ambapo usuluhishi wake kwa mzozo wa kisiasa nchini Zimbabwe unaburuza miguu na wakati uchaguzi mkuu wa nchi hiyo hapo mwakani unaonekana kutotowa nafasi ya kufanikisha usuluhishi huo ambao matumaini ya kimataifa yako kwa uwezo wa Rais Thabo Mbeki kuanzisha mazungumzo kati ya chama tawala cha Rais Robert Mugabe na upinzani.

https://p.dw.com/p/CHFc
Rais Thabo Mbeki akipokewa kwa furaha na rafiki yake Rais Robert Mugabe mjini Harare mwaka 2002.
Rais Thabo Mbeki akipokewa kwa furaha na rafiki yake Rais Robert Mugabe mjini Harare mwaka 2002.Picha: AP

Hata hivyo kutokana na mamlaka ya Mbeki kuwa na kikomo kwenda pale yeye na wengine wameshindwa huko nyuma ikiwa ni pungufu ya mwaka kabla ya Zimbabwe kufanya uchaguzi mkuu na Mugabe kuonekana kuzidi kutumia mbavu wengi wanataraji kwamba mchakato huo utakuwa ni jitihada za mazimbwezimbwe(mizengwe).

Kwa mujibu wa mchambuzi wa kisiasa Moeletsi Mbeki sera ya kidiplomasia ya Afrika Kusini ya kubakia kimya juu ya mzozo huo wa Zimbabwe haisaidi hali hiyo.Anafikiri hatua ya serikali ni kutaka kuonekana kwamba inajaribu kuchukuwa hatua fulani lakini hakuna tishio kwa maslahi yake ya kutaka kufanya uwekezaji mzito wa kuleta mabadiliko nchini Zimbabwe.

Juhudi za usuluhishi zilizopita za Rais Mbeki na rais wa zamani wa Musmbiji Joaquim Chisano wa Msumbji zimekwenda kombo na bado Mugabe anaonekana kuwa hataki na Mbeki hawezi kuzilazimisha pande hizo zinazopingana kutatuwa matatizo yao.

Wakati alipoulizwa iwapo muda unayoyoma kwa Afrika Kusini mtaalamu huyo wa siasa za eneo hilo katika Chuo Kikuu cha Pretoria nchini Afrika Kusini ambaye ni kaka wa Rais Mbeki amesema kwa hakika kabisa wana mamlaka na watajaribu inavyowezekana lakini matumaini ya mafanikio ni jambo lisiloyumkinika.

Wiki iliopita waziri wa mambo ya nje wa Afrika Kusini Nkosazana Dlamini Zuma ameonya kwamba Afrika Kusini haiwezi kutegemewa kufanya miujiza kwa nchi hiyo jirani yake wakati naibu wake Aziz Pahad akisema juhudi za usuluhishi ndio kwanza ziko katika hatua ya maandalizi.

Chama cha Mugabe cha ZANU-PF inaonekana kuwa kimekusudia kufanya usuluhishi huo iwe vigumu kufanikiwa kadri inavyowezekana kwa kugoma kuzungumza hadi hapo upinzani utakapotii msimamo wake.

Katika uhariri wa toleo la karibuni la gazeti la The Voice ambao ni mdomo wa chama limesema upinzani lazima wavunje uhusiano wa kishetani na wakoloni wao wa zamani na kufuata kanuni za demokrasia kuingia katika madaraka ya kisiasa.

Lovemore Madhuku mkuu wa Baraza la Katiba nchini Zimbabwe amesema Mugabe ameonyesha hana utashi na mazungumzo na amekubali tu kufanyika usuluhishi kuwatuliza wenzake katika Jumuiya ya Maendeleo ya nchi za Kusini mwa Afrika SADC ambao wamemtaka Mbeki kuingilia kati hapo mwezi uliopita.

Wakati huo huo Umoja wa Ulaya mapema wiki hii imeongeza shinikizo kwa Rais Robert Mugabe kwa kuwakandamiza wapinzani ambapo imeahidi kupiga marufuku utowaji wa viza kwa maafisa zaidi wa serikali ya Zimbabwe.

Katika taarifa umesema itatanuwa orodha ya watu wa kuwanyima visa hususan viongozi waandamaizi wanaohusika na mgogoro wa utawala nchini Ziimbabwe na uvunjaji wa haki za binaadamu.

Umoja wa Ulaya mwezi huu uliwaongeza manaibu mawaziri watano kwa zaidi ya maafisa 100 wa serikali ya Zimbabwe akiwemo Mugabe mwenyewe ambao wamepigwa marufuku kuingia katika nchi za Umoja wa Ulaya na mali zao kuzuiliwa katika nchi hizo.