1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Muzbekistan mtuhumiwa wa shambulio liliouwa wanne Sweden.

8 Aprili 2017

Mwanaume wa miaka 39 raia wa Uzbekistan mbaroni kwa tuhuma za kuiteka nyara lori na kulibamiza kwa umati mkubwa wa watu Stockholm na kuuwa watu wanne kujeruhi wengine 15 katika shambulio la kigaidi.

https://p.dw.com/p/2avxL
Schweden - Stockholm nach dem Anschlag
Picha: Reuters/TT/A. Wikllund

Mwanaume mwenye umri wa miaka 39 raia wa Uzbekistan alioko kizuizini ni dereva anayetuhumiwa kuliteka nyara la kusambaza bia ambalo liliuvamia umati mkubwa wa watu katikati ya mji mkuu wa Stockholm na kuuwa watu wanne na kujeruhi wengine 15 katika kile kinachoonekana dhahir kuwa ni shambulio la kigaidi.

Mwanaume huyo ambaye alikuwa akijulikana kabla na mashirika ya ujasusi ya Sweden ambaye ni mtu aliyejitenga asiekuwa na uhusiano unaofahamika na makundi ya Kislamu ya itikadi kali anatuhumiwa kuwaponda wapita njia katika mtaa wenye harakati kubwa za manunuzi na kulibamiza gari hilo hadi ndani ya duka moja hapo Ijumaa (07.04.2017).

Dan Elliason mkuu wa jeshi la polisi nchini Sweden ameuambia mkutano wa wandishi wa habari hapo Jummamosi kwamba hakuna kinachoashiria kwamba mtu huyo waliemkamata sie aliehusika na shambulio hilo na kwamba kinyume chake tuhuma zimezidi kuimarika wakati uchunguzi ukiendelea.

Mtu huyo aliekamatwa Ijumaa usiku kwa madai ya kuhusika na ugaidi baada ya kutokea shambulio katikati ya mji mkuu wa Stockhlom inaonekana alichukuwa hatua hiyo peke yake lakini mkuu huyo wa polisi amesema "bado hawafuti uwezekano watu wengine zaidi wakawa wanahusika."

Hakuwa na uhusiano na makundi ya kigaidi

Schweden - Stockholm nach dem Anschlag - Prinzessin Victoria
Mwana mrithi wa ufalme Victoria nchini Sweden akiwasili na mwana mfalme Daniel katika eneo la maombolezo karibu na shambulio lilipotokeaPicha: picture alliance/Lehtikuva/dpa/A. Aimo-Koivisto

Kwa mujibu wa shirika la habari la taifa TT mtuhumiwa huyo kutoka Jamhuri ya Uzbekistan ilioko Asia ya kati atawakilishwa na wakili atakayeteuliwa na mahakama Johan Eriksson.Polisi hauikutaja jina la mtuhumiwa huyo na kwamba inaonekansa alikuwa pembezoni mwa repoti za ujasusi.Mkuu wa polisi wa usalama wa Sapo Anders Thornberg amesema wamepokea taarifa za ujasusi mwaka jana lakini hawakuona uhusiano wowote na makundi ya itikadi kali.

Mkuu wa jeshi la polisi Eliasson amesema shambulio hilo linafanana kabisa na lile lililokea London mwezi uliopita ambapo kwayo watu sita wameuwawa akiwemo mshambuliaji mwenyewe ambaye aliendesha gari lililokuwa limekodiwa na kuwagonga wapita njia waliokuwepo katika daraja nje ya bunge la Uingereza.

Magari pia yametumiwa kama silaha katika mji wa Nice nchini Ufaransa na Berlin nchini Ujerumani mwaka uliopita katika mashambulizi yanayodaiwa kufanywa na kundi linalojiita kundi la Dola la Kiislamu.

Hakukuwa na taarifa iliyotolewa mara moja kudai kuhusika na shambulio hilo nchini Sweden ambayo hadi hisi sasa ilikuwa hauikuguswa na mashambulio makubwa ya kigaidi na ambapo wengi walikuwa wakijivunia kuwa ni taifa la kidemokrasia lililo na uwazi.

Kifaa chafanana na bomu la kienyeji

Schweden - Stockholm nach dem Anschlag - Dan Eliasson
Mkuu wa jeshi la polisi Sweden Dan Eliasson -akizungumza na waandishi wa habari.Picha: Getty Images/AFP/TT/A. Wiklund

Polisi imesema imegunduwa kifaa chenye kutia shaka ndani ya gari hilo ambalo liliishia kujibamiza katika duka la Ahlens lakini imesema hawajui iwapo kifaa hicho lilikuwa bomu la kienyeji kama ilivyoripotiwa na kituo cha matangazo cha SVT.

Maafisa wa serikali za mitaa katika mji wa Stockholm ambapo bendera zimekuwa zikipepea nusu mlingoti kwenye majengo ikiwa ni pamoja na bunge na kasri la kifalme wamesema watu 10 akiwemo mtoto mmoja bado wanaendelea kupatiwa matibabu hospitali huku watu wazima wawili wakiwa kituo cha wagonjwa mahtuti.

Sweden hapo Jumatatu mchana itabaki kimya kwa dakika moja kuomboleza wale waliopoteza maisha yao.

Mwandishi : Mohamed Dahman/Reuters

Mahariri : Sudi Mnette