Mwanasheria mkuu wa Marekani Jeff Sessions ang'atuka
8 Novemba 2018Mwanasheria mkuu wa Marekani Jeff Sessions amejiuzulu wadhifa wake, baada ya kuombwa kufanya hivyo na rais Donald Trump. Trump ametangaza kuondoka kwa Sessions kupitia ukurasa wake wa Twitter akisema tunamtakia kila la kheri.
Katika barua yake ya kujiuzulu isiyo na tarehe Sessions amebainisha kwamba uamuzi wa kujiuzulu haukuwa wake na alimjulisha rais Trump kwamba anawasilisha baraua kama alivyomuomba.
Nafasi yake itashikiliwa kwa muda na aliyekuwa mkuu wake wa utumishi Matthew Whitaker. Whitaker sasa atasimamia uchunguzi wa madai ya Urusi kushirikiana na kampeni za rais Trump mwaka 2016.
Nancy Pelosi, Mwanademocratik anayetarajiwa kuliongoza Baraza la wawakilishi amesema kujiuzulu huko ni jaribio la wazi la Trump, kumdhoofisha mchunguzi maalumu Robert Mueler anayeongoza uchunguzi ikiwa Urusi ilishirikiana na kampeni za Trump mwaka 2016.
Kiongozi mwingine wa Demokratik katika seneti Chuck Schumer amesema mabunge yote ya Marekani ni lazima yalinde uchunguzi huo.