1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Myanmar yapata rais wa kwanza wa kiraia

15 Machi 2016

Bunge la Myanmar limemchagua Htin Kyaw kuwa rais mpya wa nchi hiyo ya kusini mashariki mwa Asia, hivyo kuwa rais wa kwanza wa kiraia kwa zaidi ya miaka 50, hatua inayomaliza utawala wa muda mrefu wa kimabavu wa jeshi.

https://p.dw.com/p/1IDQA
Picha: picture-alliance/AP Photo/A. Shine Oo

Htin Kyaw mpambe wa karibu na rafiki wa muda mrefu wa mpigania demokrasia wa Myanmar, Aung San Suu Kyi, amechaguliwa katika tukio hilo la kihistoria katika nchi hiyo iliyoongozwa na utawala wa kijeshi. Kyaw ambaye aliwahi kufungwa na utawala wa kijeshi uliopita na alikuwa upande wa Suu Kyi wakati alipoachiwa huru kutoka kifungo cha nyumbani mwaka 2010, amepata kura 360 kati ya 652 zilizopigwa.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya ushindi huo, Kyaw, mwenye umri wa miaka 69, amesifu kuchaguliwa kwake katika wadhifa huo. ''Hii ni huruma na mapenzi waliotuonyesha watu. Huu ni ushindi kwa watu wote wa nchi hii. huu pia ni ushindi kwa Aung San Suu Kyi,'' alisema Kyaw.

Mfumo wa uchaguzi wa Myanmar unahitaji rais achaguliwe kutoka kwenye orodha ya majina ya wagombea watatu, huku jina moja likiwa limewasilishwa na mabunge yote mawili na jina la tatu litakalopendekezwa na jeshi, ambalo huchukua robo ya viti vya bunge.

NLD kilimteua Kyaw

Alhamisi iliyopita, chama cha Suu Kyi cha National League for Democracy-NLD, kilimteua Kyaw kuwa mgombea wake. Wagombea wengine wawili walikuwa ni Henry Van Thio, mshirika wa Suu Kyi, ambaye jina lake liliwasilishwa na bunge na jeshi lilimteua Myint Swe, jenerali mstaafu wa jeshi.

Wabunge wakiwasili bungeni, Myanmar
Wabunge wakiwasili bungeni, MyanmarPicha: Reuters/S. Zeya Tun

Swe atakuwa makamu wa kwanza wa rais baada ya kupata kura 213, huku Van Thio mbunge wa watu wa jamii ya Chin akiteuliwa kuwa makamu wa pili wa rais baada ya kupata kura 79.

Suu Kyi mwenye umri wa miaka 70, mshindi wa tuzo ya Nobel, na chama chake cha NLD walishinda katika uchaguzi wa Novemba ambao ulionekana kama kuidhinisha sera yake ya mabadiliko. Hata hivyo, Suu Kyi amezuiwa na katiba ya Myanmar iliyo chini ya jeshi, kugombea urais kwa sababu watoto wake wawili ni Waingereza.

Baraza jipya la mawaziri pia linatarajiwa kutangazwa kabla ya mwisho wa mwezi huu na litakuwa na majukumu ya kushughulikia changamoto kadhaa zinazolikabili taifa hilo, ikiwemo umasikini, ukosefu wa miundombinu na mizozo katika maeneo ya mipakani dhidi ya jamii ya watu wachache.

Rais Kyaw anatarajiwa kuapishwa Aprili Mosi, kuliongoza taifa hilo kwa miaka mitano na kuchukua nafasi ya rais anayeondoka madarakani, Thein Sein aliyekuwa akiungwa mkono na jeshi. Kiongozi huyo anasifiwa kwa kuliweka taifa hilo katika mkondo sahihi wa kuondokana na utawala wa moja kwa moja wa kijeshi.

Mwandishi: Grace Patricia Kabogo/AFP,AP,DPA
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman