1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NAIROBI: Kenya yaufunga mpaka wake na Somalia

4 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCdT

Kenya imeufunga mpaka wake na Somalia na kuwafukuza wakimbizi 400 katika juhudi za kuwazuia wanamgambo wa mahakama za kiislamu wasivuke mpaka. Uamuzi huo umechukuliwa baada ya kuthibitishwa kwamba wanajeshi wa Ethiopia walikishambulia kwa mabomu kituo cha mpakani mwa Kenya.

Waziri wa mashauri ya kigeni wa Kenya, bwana Raphael Tuju jana aliwaambia waandishi wa habari mjini Nairobi kwamba ni vigumu kutathmini ikiwa watu wanaovuka mpaka kutoka Somalia ni wakimbizi halali au wapiganaji.

Aidha Tuju alisema hatua ya serikali ya mpito ya Somalia kuidhibiti nchi hiyo si sababu ya kuwalazimu raia waikimbie nchi yao.

Shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa limeilaani hatua ya Kenya kuwarejesha wakimbizi hao. Akizungumza katika makao makuu ya shirika hilo mjini Geneva, Uswisi, kiongozi wa shirika hilo, Antonio Guteres, alisema Kenya ina jukumu la kuwalinda raia kwa mujibu wa sheria ya kimataifa.