1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NAIROBI : Serikali yagoma kutangaza maafa ya kitaifa

5 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCmW

Serikali ya Kenya hapo jana imesisitiza kwamba ina uwezo wa kuwasaidia takriban watu 700,000 walioathiriwa na mafuriko licha ya kuonywa na makundi ya misaada ya kibinadamu kwamba hali inazidi kuwa mbaya nchini kote.

Msemaji wa serikali Alfred Mutua amesema serikali haitotangaza mafuriko hayo kuwa ni maafa ya kitaifa licha ya wito wa kufanya hivyo uliotolewa na mashirika ya misaada ikiwa ni pamoja na shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya na Action Aid.

Amewaambia waandishi wa habari kwamba hawakutangaza hali hiyo kuwa maafa ya kitaifa kwa sababu hawaoni haja ya kufanya hivyo kwa wakati huu.

Mwishoni mwa mwezi uliopita mashirika hayo mawili yalitowa wito kwa Rais Mwai Kibaki kutangaza mafuriko hayo kuwa maafa ya kitaifa kwa kusema kwamba hilo lingeliweza kuwasaidia katika juhudi zao za kuratibu shughuli za misaada na kuboresha itikio la wafadhili.

Mafuriko nchini Kenya hadi sasa yameuwa watu 51 na kuwaathiri wengine 723,000 ikiwa ni pamoja na maelfu ya wakimbizi wa Somali.