1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ndege za Ethiopia zashambulia maeneo mawili jimboni Tigray

Daniel Gakuba
25 Oktoba 2021

Jeshi la Ethiopia lilifanya mashambulizi mawili ya anga Jumapili, likilenga maeneo ambayo maafisa wa serikali wamesema ni ngome za vikosi vilivyoasi jimboni Tigray.

https://p.dw.com/p/429Gh
Äthiopien | Luftangriff auf der äthiopische Armee auf Mekelle
Picha: Million Haileselassie/DW

Mashambulizi hayo yaliyopiga mbali ya mji mkuu wa jimbo la Tigray, Mekele, yanaashiria azma ya serikali ya mjini Addis Ababa kupanua kampeni yake ya angani dhidi ya vikosi vya Kundi la Ukombozi wa Watu wa Tigray, TPLF.

Jumuiya ya kimataifa imeyalaani mashambulizi hayo ambayo yaliendelea kwa wiki nzima iliyopita, kwa kuvuruga mipango ya kusambaza chakula katika maeneo yenye kitisho cha njaa.

Msemaji wa serikali ya Ethiopia Selamawat Kassa amesema kituo kilicholengwa kilitumiwa kama kamandi na chuo cha mafunzo cha TPLF.

Kwa upnde wake, TPLF imeyakanusha hayo; msemaji wake Getachew Reda kupitia mtandao wa twitter amesema shambulizi la ndege za Ethiopia limeipiga hospitali ya Mai Tsebri pamoja na kiwanda cha nguo cha Adwa.