1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ni nani atakayefuzu kuelekea kombe la Dunia?

20 Septemba 2013

Italia, Ujerumani na Uholanzi na Uhispania zinaweza kujipa nafasi ya kushiriki katika Dimba la Dunia mwaka wa 2014 wakati timu za Ulaya zitakapoingia viwanjani tena Jumanne 10.09.2013 kwa mechi za kufuzu.

https://p.dw.com/p/19eHX
Cristiano Ronaldo wa Ureno akipambana na Steven Davis wa Ireland ya Kaskazini
Cristiano Ronaldo wa Ureno akipambana na Steven Davis wa Ireland ya KaskaziniPicha: Peter Muhly/AFP/Getty Images

Miamba wote wa soka barani Ulaya wamejiimarisha kileleni mwa makundi yao na watalenga kuepuka masaibu katika dakika za mwisho mwisho kwa kujikatia tikiti zao wakati kukiwa kumesalia mechi kadhaa za kuchezwa.

Italia itapata nafasi ya kwanza katika kundi B kama itashinda nyumbani mchuano wao na Jamhuri ya Czech lakini Wajerumani na Waholanzi wanahitaji ushindi dhidi ya Visiwa vya FAROE na Andorra, na pia wakitaraji kuwa matokeo ya mechi nyinegine yatawaendea ili wafuzu moja kwa moja. Ujerumani itatalenga kuwafunga WaFaroe mabao mengi lakini itajihakikishia nafasi tu ya kuongoza kundi C na kujipa tikiti ya 16 mfululizo ya kushiriki dimba la dunia kama nambari mbili Sweden watashindwa na Kazakhstan.

Uholanzi pia ni lazima iwaangamize Andorra ambayo haina pointi hata moja wala bao, kufikia sasa katika kundi D lakini inataraji kuwa nambari mbili Romania itadondosha pointi nyumbani itakapocheza na Uturuki. Mambo ni magumu zaidi hata kwa timu ya England, ambayo inaongoza kundi H lakini huenda ikatafuta tikiti yake kupitia mechi za mchujo kama itashindwa kutoka mjini Kiev, Ukraine na angalau pointi moja katika mechi hiyo kali ya kufuzu.

Mshambuliaji chipukizi wa Ujerumani Marco Reus atakosa mchuano dhidi ya Visiwa vya Faroe
Mshambuliaji chipukizi wa Ujerumani Marco Reus atakosa mchuano dhidi ya Visiwa vya FaroePicha: picture-alliance/dpa

Ukraine iko katika nafasi ya tatu na tofauti ya pointi moja na italenga kuipindua England kama itaweza kulipiza kisasi kichapo dhidi ya wapinzani hao katika mchuano wa makundi wa dimba la mataifa ya bara Ulaya UEFA Euro mwaka jana mjini Donetsk.

Katika mechi nyingine, Ufaransa ambayo matumaini yake yanadidimia, itachuana na Belarus, wakati Urusi ikiibandua uongozini Ureno katika kundi F kama itaishinda Israel ikiwa na mchuano mmoja wa ziada. Uswisi huenda ikapunguza uongozi wake wa kundi E kwa pointi moja kama itashindwa na Norway mjini Oslo. Bosnia-Herzegovina na Ugiriki zinaongoza kundi G na pointi 16 kila mmoja na zitamenyana na Slovakia na Latvia.

Tukiangalia Amerika ya Kusini, Argentina na Colombia zinaweza kujikatia tikiti hapo kesho. Timu hizo mbili zinaongoza kundi la nchi za Amerika ya Kusini zikiwa na pointi 26 kutokana na mechi 13. Argentina ambayo ina faida ya pengo kubwa la mabao, inaweza bado kufuzu hata kama itashindwa ugenini Paraguay, wakati sare yoyote nchini Uruguay ikitosha kuwapa Colombia nafasi ya kucheza katika Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza tangu mwaka wa 1998. Timu nne zitafuzu moja kwa moja kutoka Amerika ya Kusini, pamoja na nafasi ya kupata timu ya tano kupitia mechi ya mchujo dhidi ya timu ya bara Asia. Wenyeji Brazil walipewa tikiti ya moja kwa moja. Chile ni ya tatu na pointi 24 baada ya mechi 14, wakati Equador ikiwa ikiwa ya nne na pointi 21. Uruguay ni ya tano na pointi 19. Venezuela na Peru zina nafasi ndogo za kusafiri nchini Brazil.

Mwandishi: Bruce Amani/Reuters/AFP/DPA

Mhariri:Mohammed Abdul-Rahman