1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ni Senegal na Algeria fainali ya AFCON

Sekione Kitojo
18 Julai 2019

Senegal iko umbali wa ushindi mmoja tu kuweza kunyakua taji hilo la mataifa ya Afrika kwa mara ya  kwanza na kwa kocha Aliou Cisse mafanikio hayo yatakamilisha  miaka 17 ya kusubiri kutawazwa mabingwa wa Afrika.

https://p.dw.com/p/3MGzG
Africa Cup of Nations 2019 - Viertelfinale - Senegal gegen Benin | Jubel
Picha: Reuters/M. A. El Ghany

Kizazi cha dhahabu  cha wachezaji wa  Senegal kinataka  kuandika historia  katika fainali ya  kombe  la  mataifa  ya  Afrika, Afcon leo jioni wakati  watakapotiana  kifuani  na  Algeria mjini  Cairo.  

Africa Cup of Nations 2019 - Viertelfinale - Senegal gegen Benin
Mlinzi wa Senegal Kalidou Koulibaly katikati akiondoa mpira karibu na lango lake dhidi ya mshambuliaji wa Benin Emmanuel ImorouPicha: Getty Images/AFP/J. Soriano

Akiwa  mchezaji  wa  kiungo Cisse  alikuwa  nahodha  wa  Senegal ambayo  ilikuwa  kizazi kikuu  cha  dhahabu, hadi  sasa  kikiwa  ni kizazi  ambacho  kilifikia  robo  fainali  ya  kombe  la  dunia  mwaka 2002 na  kushindwa  na  Cameroon  katika  fainali  ya  mataifa  ya Afrika katika  mwaka  huo  kwa  mikwaju  ya  penalti.

Cisse alikuwa  wa  mwisho  kati  ya  wachezaji  watatu  wa  Senegal kukosa  penalti  mjini  Bamako  mji  mkuu  wa  Mali  lakini  ana matumaini  makubwa  ya  kuepuka  kurejewa  kwa  hali  hiyo  Ijumaa hii  mjini  Cairo.

"Nina  waamini  sana  wachezaji  wangu  na nahisi  kwamba wanataka  kufanikisha  kitu," Cisse  ameuambia  mtandao wa CAFOnline.com baada  ya  ushindi  katika mchezo  wa  nusu  fainali dhidi  ya  Tunisia.

"Kizazi  hiki ni  bora  kuliko  kile  cha  mwaka 2002. Wachezaji wangu  wameniambia  watakuwa  wazuri  zaidi kuliko  sisi, na wameweza.

Afrika-Cup 2019 Halbfinale | Senegal - Tunesien
Mchezo wa nusu fainali kati ya Senegal na Tunisia ambapo , Senegal ilishinda kwa bao 1-0Picha: Reuters/S. Salem

Wakiongozwa  na  Sadio Mane, ambaye ametawazwa  hivi  karibuni bingwa  ligi  ya  vilabu  bingwa  barani  Ulaya  Champions League akiwa  na  Liverpool , maendeleo  yao  nchini  Misri hayajaanguka patupu.

Walihitaji  ushindi  dhidi  ya  Kenya  kuweza  kusonga  mbele  kutoka katika  kundi C ambalo  lilikuwa  na  Algeria, Tanzania  na  Kenya , baada  ya  hapo  kabla  kushindwa  na  wapinzani  wao  katika fainali  hii  Algeria na  ushindi wao katika  michezo  minne imekuja kupitia dakika  za  nyongeza, goli  la  kujifunga baada  ya  pande zote  mbili kukosa  penalti katika  dakika  za  mwisho katika  wakati wa  kawaida.

"Haya  ni  matunda  ya  matayarisho  ya  muda  mrefu," alisema Cisse. Wachezaji  hawa  wamefanyakazi kwa  nguvu  kwa  miaka mitano mizima na  sasa  tunapata matunda  yake ya  kazi  yao ngumu."

Sadio Mane Africa Cup
Mchezaji nyota wa Senegal Sadio ManePicha: picture alliance/empics/M. Ntombela

Algeria  na  nyota wake

Cisse  amekuwa  kocha  tangu  mwaka  2015 na  anasema mafanikio  yake  yanatokana  na uhusiano  wa  karibu  alionao  na wachezaji, kama  mlinzi  wa  Napoli Kalidou Kuolibaly ambaye alimshawishi  kuingia  katika  kikosi  cha  Simba  wa  Teranga  badala ya  Ufaransa.

Algeria  ina nyota  wake pia  wakubwa  katika  ligi, sio  mwingine zaidi  ya  mchezaji  mahiri  wa  kati  Riyad Mahrez wa  mabingwa  wa mataji  matatu  nchini  Uingereza katika  msimu  mmoja  manchester City.

Mahrez  alifunga  mkwaju  wa  dakika  za  mwisho  na  kuishinda Nigeria  kwa  mabao 2-1  katika  mchezo  wao  wa  nusu  fainali , na kuzusha  shangwe  na  hoi hoi  uwanjani  na  pia  Ufaransa, ambako mamia  ya  mashabiki walikamatwa  wakati  sherehe zilipofikia  hatua ya  kutoweza  kudhibitiwa.

"Tumekuwa  vizuri  sana  katika  mashindano  haya," Mahrez amesema. "Tumefunga  mabao 12  na  kufungwa mawili  tu,  lakini mchezo huu umetupa hali ya kujiamini  zaidi  kucheza fainali.

"Tuna uwezo  wa  kushinda."

Ägypten Afrika-Cup - Algerien vs. Guinea
Riad Mahrez (7) akiipatia timu yake bao la pili dhidi ya GuineaPicha: picture-alliance/AP Photo/A. Schalit

Hali ya wasi wasi

Ushindi  utaipa  Algeria  ushindi  wake  wa  pili  wa  AFCON baada ya  ule  wa  mwaka  1990, ambao  ni  pamoja  na ushindi  wa michezo  minne  dhidi  ya  Senegal.

"Tumecheza  na  Senegal  katika  awamu  ya  makundi  na tunafahamu kuwa ni  timu  nzuri  sana," amesema  Mahrez. "itakuwa fainali  ngumu. Lakini Senegal , tunafahamu  nguvu  zao  na  udhaifu wao  na  tutaingia  uwanjani  kuwapa  mchezo  mzuri."

Hali  ya  wasi  wasi  hata  hivyo  imehamia  Ufaransa  kuhusiana  na mchezo  huo  wa  fainali  ya  AFCON na  sio mjini Algiers  ama Dakar.

Polisi itaweka  vikosi  vyake usiku  wa  leo Ijumaa mjini  Paris kuhakikisha  usalama kwa  ajili  ya  fainali za  kombe  la  mataifa  la Afrika,  ambapo Senegal inacheza  na  Algeria. Polisi 2,500 watawekwa  Ijumaa  usiku  mjini  Paris  kuhakikisha  usalama  katika eneo  la  Champs-Elysee kwa  ajili  ya  fainali  hiyo.

sherehe za ghasia zilizuka  siku  ya  Jumapili  nchini  Ufaransa, ambako  wanaishi jamii  kubwa  ya watu  wenye  asili  ya  Algeria , baada  ya  Algeria  kuishinda  Nigeria  kwa  mabao 2-1. Polisi  ya Ufaransa  iliwatia nguvuni zaidi  ya  watu  200.