1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama alijua nini hasa?

28 Oktoba 2013

Bado mpaka sasa Rais Barack Obama na Shirika la Ujasusi (NSA) wanatafuta la kusema baada ya kudhihirika kwamba simu ya mkononi ya Kansela Angela Merkel wa Ujerumani ilikuwa ikitegwa na maafisa wa ujasusi wa Marekani.

https://p.dw.com/p/1A79U
Picha inayoashiria unasaji wa simu za Ujerumani uliofanywa na Marekani.
Picha inayoashiria unasaji wa simu za Ujerumani uliofanywa na Marekani.Picha: picture-alliance/dpa

Gazeti la kila Jumapili la "Bild am Sonntag" linalosomwa na watu wengi nchini Ujerumani jana (tarehe 27 Oktoba) liliripoti kwamba Rais Obama alijua kwamba simu ya mkokoni ya Kansela Merkel ilikuwa inasikilizwa na NSA tokea mwaka 2010. Shirika hilo limeyakanusha madai hayo, lakini bado pana hitilafu nyingi.

Ikulu ya Marekani imenyamaza kimya na NSA inasubiri. Msemaji wa Idara ya Ujasusi ya Marekani ameeleza kuwa ripoti ya "Bild am Sonntag" siyo sahihi. Mkuu wa NSA, Keith Alexander, hakumpa taarifa Rais Obama binafsi juu ya shughuli za kusikilizwa kwa simu ya Kansela wa Ujerumani na NSA. Pana madai kwamba Mkurugenzi wa NSA na Rais Obama asilani hawakuzungumzia juu ya shughuli za upelelezi zilizomhusu Kansela Markel.

Jambo moja linaweza kuwa wazi kwa mujibu wa taarifa ya gazeti la New York Times , kwamba simu ya mkononi ya Kansela Merkel ilianza kusikilizwa na majasusi wa Marekani miaka 10 iliyopita au hata kabla ya hapo. Wakati huo Merkel bado alikuwa mwenyekiti tu wa chama cha CDU.

Aliyekuwa wakala mwaminifu wa NSA kwa muda wa miaka 18, Thomas Drake, ni mtu anayepaswa kuyajua ya jioni na ya asubuhi katika shirika hilo. Amesema hakushangazwa ni kilichotokea.

Kumbukumbu za Statsi

Kutokana na kukasirishwa juu ya kupelelezwa kwa simu za wananchi wa Marekani , Drake angelikuwa mtoboa siri siku nyingi kabla ya Edward Snowden.

Picha hii ya tarehe 2 Septemba 2009 inamuonesha Rais Barack Obama akiwa na Kansela Angela Merkel kwenye mkutano wa kilele wa G20 jijini London.
Picha hii ya tarehe 2 Septemba 2009 inamuonesha Rais Barack Obama akiwa na Kansela Angela Merkel kwenye mkutano wa kilele wa G20 jijini London.Picha: picture-alliance/dpa

Ameeleza kuwa alikuwa anatarajia kuyasikia mambo mengine yakifichuliwa kutokana na kile anachokijua kutokea ndani ya shirika la NSA. Yaliyotokea pia yanamkumbusha enzi za zamani.

"Hebu kumbuka enzi za ufashisti nchini Ujerunmani. Hebu kumbuka enzi za upelelezi wa shirika la ujasusi la Stasi katika Ujerumani Mashariki. Yaliyofanyika kwa Angela Merkel yamemgusa sana yeye binafsi kukumbuka mashambulizi ya nchini Marekani, kwa sababu wateka nyara walikuwapo nchini Ujerumani, waliishi Ujerumani na walikwenda Marekani kutokea Ujerumani. Na kwa hivyo serikali ya Marekani na shirika la NSA kwa pamoja waliamua kuwa Ujerumani inapaswa kuwa kituo kikuu cha kupelelezwa barani Ulaya."

Wakala huyo wa zamani wa shirika la NSA ameeleza kuwa yanayoibuka sasa na kutokea hadharani hayasemeki.

Thomas Drake, ambaye alifanya upelelezi dhidi ya Ujerumani ya Mashariki ya zamani, amesema kilichotokea "kinamkumbusha enzi za Statsi na pia yanamkumbusha enzi za mafashisti nchini Ujerumani."

Mwandshi wa habari aliyefichua kashfa ya Watergate, Bob Woodward, pia amezikosoa shughuli za shirika la NSA.

Mwandishi: Antje Passenheim
Tafsiri: Abdu Mtullya
Mhariri: Josephat Charo