1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama-Guantanamo

Eric Kalume Ponda22 Januari 2009

Ni siku ya tatu tangu kuanza kazi yake katika ikulu ya White House, kama rais wa Marekani. Na tayari Rais Barack Obama amekuwa na shughuli nyingi tangu kuapishwa kwake siku ya Jumanne.

https://p.dw.com/p/Ge9D
Rais Barack Obama kulifunga Gereza la Guantanamo.Picha: AP

Leo rais anaelekea kutimiza moja wapo ya ahadi zake alizotoa wakati wa Kampeini ya uchaguzi juu ya kufungwa kwa gereza la Guantanamo.

Rais Barack Obama anatazamiwa kutia saini amri ya kufungwa kwa gereza hilo ambalo limekuwa kero kwa wengi duniani tangu lifunguliwe mwaka wa 2002.


Rais Barack Obama anasema kwenye agizo hilo kwamba anataka kulifunga gereza hilo wanakozuiliwa watuhumiwa 254 katika muda wa mwaka mmoja ujao.


Agizo hilo linafuatia jingine alilolitoa jana ya kusimamisha kwa muda wa siku 120 na kuchunguzwa upya kwa mashtaka yanayowakabili watuhumiwa katika gereza hilo.


Hatua hiyo imepongezwa na mashirika ya kimataifa ya kutetea haki za binadamu ingawa yanahoji kuwa muda huo wa mwaka mmoja ni mrefu mno.


Rais Barak Obama alilazimika kula kiapo tena baada ya kasoro kutokea wakati wa kuapishwa kwakwe siku ya Jumanne.


Baada ya kula kiapo Rais huyo alisema kuwa dhamira yake ni kubadili jinsi mambo yalivyokuwa yakiendeshwa katika ikulu ya White House. Akikutana na wafanyakazi wa Ikulu hiyo walioapishwa na makamu wa rais Joe Baiden. Rais Barack Obama alisema kuwa enzi za mambo kuwekwa siri katika ikulu hiyo zimekwisha. Rais Obama alisema ``Hatupasi kusahau kuwa sisi ni watumishi wa umma, na utumishi wa umma ni bahati na heshima kubwa, sio kuendeleza maslahi yako, sio kuendeleza maslahi ya jamaa zako au washirika wa kibiashara, sio kuendeleza maadili na ajenda au maslahi ya mashirika yoyote. Utumishi wa Umma ni wazi kabisa, na si suala la kujadilia, ni kuendeleza maslahi ya raia wa Marekani´´


Wakati huo huo chaguo la Rais huyo; Bibi Hilary Clinton kuwa waziri wake wa mambo ya nchi za nje liliidhinishwa na bunge la Marekani baada ya kuungwa mkono kwa kura 94 dhidi ya 2.


Mara baada ya kuidhinishwa Hilary Clinton alieleza mipango na sera za Marekani kwa mataifa ya kigeni, akisema kuwa suala la dharura kwa serikali hiyo ni kuleta amani katika eneo la mashariki ya kati.


Pia hakusita kuelezea dhamira ya serikali hiyo kuijongelea Iran ambayo imekuwa hasimu mkubwa wa Marekani kutokana na mpango wake wa zana za Kinuklia.


Aidha kwa upande mwengine baada ya kuzungumza kwa njia ya simu na viongozi wa eneo la mashariki ya kati, Rais Obama amesema kuwa hivi karibuni atakutana na rais Hosni Mubara wa Misri, waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert na kiongozi wa Wapalestina Mahmud Abas kujadili mzozo wa eneo la mashariki ya Kati.


Ponda/Afp