1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Pande pinzani nchini Palestina zaandaa mkutano wa pamoja

Tatu Karema
4 Septemba 2020

Kiongozi wa mamlaka ya Wapalestina Mahmoud Abbas ameandaa mkutano uliozishirikisha pande zinazopingana kuweka msimamo mmoja dhidi ya makubaliano ya kuwepo uhusiano wa kawaida kati ya Israel na Umoja wa Falme za Kiarabu

https://p.dw.com/p/3hzNf
Westjordanland Mahmud Abbas | Reaktion auf Friedensplan von Donald Trump & Benjamin Netanjahu
Picha: Reuters/R. Sawafta

Mkutano huo uliandaliwa kwa njia ya video ukiunganisha miji ya Ramallah ulioko katika ukingo wa Magharibi na Beirut  ambapo kiongozi wa kundi la Hamas Ismail Haniyeh na katibu mkuu wa kundi linalojiita Islamic Jihad Ziyad al-Nakhalah walishiriki. Ni nadra kwa kundi hilo la Hamas linaloshikilia misimamo ya kiislamu na chama cha Fatah kinachoongozwa na Abbas kuandaa mikutano ya kilele baada ya mapigano ya miaka kadhaa.

Wakati wa mkutano huo, Mahmoud Abbas alisema kwamba hawatamruhusu mtu yeyote kuwazungumzia na hawatairuhusu Marekanikuwa mpatanishi wa kipekee katika mazungumzo na Israeli na pia  hawatakubali mpango wake wa makubaliano ya amani huku akitoa wito wa umoja wa wapalestina wakati huu wa mpango huo wa Marekani.

Haniyeh ambaye vuguvugu lake la upinzani linadhibiti ukanda wa Gaza, pia alitoa wito wa muungano akiwa mjini Beirut. Kiongozi huyo wa kundi la Hamas amesema kuwa lazima umoja wa wapalaestina udumishwe na kumalizika kwa hali ya mgawanyiko na kuanzisha msimamo wa umoja wa Palestina.

Palästinensischer Hamas-Chef Ismail Haniyeh
Ismail Haniyeh- Kiongozi wa kundi la HamasPicha: picture-alliance/ZUMAPRESS/A. Amra

Palestina ilishangazwa na mkataba huo wa kurejesha uhusiano kati ya jumuiya ya falme za kiarabu na Israeli na kuuona kama usaliti ambao huenda ukadhoofisha msimamo wake wa muda mrefu wa muungano wa mataifa ya kiarabu unaoitaka Israeli kujiondoa kwenye makazi waliokalia. Mkataba huo ulisimamiwa na rais wa Marekani Donald Trump.

Abbas amekataa kushirikiana na serikali ya Trump kwa zaidi ya miaka miwili akiishtumu kwa kuipendelea Israeli na pia kukataa mpango wa Trump kwa Mashariki ya Kati uliozinduliwa mwezi Januari mwaka huu. Katika taarifa ya pamoja iliyotolewa baada ya mkutano huo, pande hizo za Palestina zilitangaza kuidhinisha kubuniwa kwa kamati ya pamoja katika muda wa wiki tano kuandaa 'upinzani maarufu' na pia kutia kikomo kwa migawanyiko kati yao.

Siku ya Jumatatu, maafisa wa ngazi ya juu wa Marekani na  Israeli walifanya ziara ya kihistoria mjini Abu Dhabi kuunga mkono kudumishwa kwa maktaba huo kati ya Israeli na Jumuiya ya falme za kiarabu.Mshauri wa Trump Jared Kushner, aliwaambia Wapalestina kwamba wanapaswa kukubali mkataba huo , kurejelea mazungumzo na Israeli na sio kukwama katika nyakati zilizopita.