1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa awapa matumaini wahamiaji

16 Aprili 2016

Papa Francis amewafikishia ujumbe wa matumaini maelfu ya watu wanaokabiliwa na kutimuliwa Ugiriki kwa kutangaza "sisi sote ni wahamiaji" na kuishutumu jumuiya ya kimataifa kwa kutokomesha vita vinochochea mzozo huo.

https://p.dw.com/p/1IX1y
Papa Francis akilakiwa na Askofu Mkuu Ieronimos wa Kanisa la Orthodox nchini Ugirikli baada ya kuwasili kisiwa cha Lesbos (16.04.2016)
Papa Francis akilakiwa na Askofu Mkuu Ieronimos wa Kanisa la Orthodox nchini Ugirikli baada ya kuwasili kisiwa cha Lesbos (16.04.2016)Picha: Reuters/A. Konstantinidis

Katika ziara iliojaa hisia nzito ambayo imeshuhudia watu wakipiga magoti na kuchuruzika machozi miguuni mwa papa , kiongozi huyo wa kanisa katoliki duniani amewaambia wahamiaji hao kwamba"hawako peke yao"

Ameisihi dunia kuonyesha "utu wa pamoja" kufuatia msimamo mkali wa Umoja wa Ulaya kuhuhusiana na wahamiaji.

Na katika ujumbe wa wazi kwa mataifa yenye misimamo mikali ambayo yamekataa kushiriki katika mpango wa Umoja wa Ulaya kugawana wahamiaji hao Papa mwenye umri wa miaka 79 amezichukuwa familia tatu za Kiislamu za Syria ambazo nyumba zao zimeshambuliwa kwa mabomu nchini Syria.

Papa ambaye ameandamana na Askofu Mkuu wa Kanisa la Orthodox Ieronymos kiongozi wa kanisa la Ugiriki amewaambia wahamiaji walioko katika kituo cha usajili cha Moria ambako watu 3,000 wanashikiliwa kwamba "Hamko peke yenu ....msikate tamaa".

Wengi wa wahamiaji hao wameomba kupatiwa hifadhi lakini yumkini wakarudishwa makwao kwa kuzingatia makubaliano tata yaliofikiwa mwezi uliopita kushughulikia mzozo wa wakimbizi barani Ulaya kwa kuwawarudisha Uturuki wahamiaji wote walioko kinyume na sheria kutoka Ugiriki.

Hisia nzito

Wakati akisindikizwa huko Moria kukutana na baadhi ya wahamiaji mwanaume mmoja alibwaga kilio wakati alipoinama kwenye miguu ya papa na kuomba ambariki.

Papa Francis akisalimiana na wahamaji katika kituo cha Moria kisiwa cha Lesbos (16.04.2016)
Papa Francis akisalimiana na wahamaji katika kituo cha Moria kisiwa cha Lesbos (16.04.2016)Picha: Reuters/F. Monteforte/Pool

Mwanamke mwengine ambaye aliwapenya wana usalama kuwasiliana na papa alianguwa kilio wakati papa alipokuwa amesimama kumsikiliza.

Wahamiaji wengine walikusanyika nje wakiwa na ujumbe uliokuwa ukisomeka " "Tunataka uhuru", "Waachieni watu wangu" na "Papa jaribu kutuokowa."Kundi la watoto wadogo lilimkabidhi papa mchoro kadhaa.

Lesbos ni mojawapo ya bandari za mwanzo kuwasili katika nchi za Umoja wa Ulaya kwa maelfu ya watafuta hifadhi ambao wamekimbia vita,umaskini naukandamizaji Mashariki ya Kati na Asia kwa kuvuka bahari ya Aegean kwa kupitia Uuturuki mwaka jana.

Viongozi wa kidini walifanya maombi katika bandari ya Lesbos kuwaombea mamia ya wahamiaji waliokufa maji wakati wa safari zao kwenye maboti yaliofurika chini ya mikono ya watu wanaosafirisha binaadamu kwa magendo.

Awali walisaini azimio lenye kutowa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuchukuwa hatua ya kukabiliana na hali hiyo ya mzozo wa kibinaadamu kwa ushujaa na kwa jumuiya za kidini kuongeza juhudi za kuwasaidia wakimbizi.

Dunia kuhukumiwa kwa matendo yake

Papa amesisitiza kwamba wahamiaji sio idadi ya watu bali ni watu "wenye sura,majina na habari binafsi" ambao wanawindwa na makundi ya majambazi na ametaka juhudi madhubuti zichukuliwe kutokomeza biashara ya magendo ya silaha.

Papa Francis akisalimiana na wahamaji katika kituo cha Moria kisiwa cha Lesbos (16.04.2016)
Papa Francis akisalimiana na wahamaji katika kituo cha Moria kisiwa cha Lesbos (16.04.2016)Picha: Reuters/F. Monteforte

Papa amesema "Dunia itahukumiwa kwa namna ilivyowatendea.Na sote tutawajibika kwa namna tulivyoushughulikia mzozohuu na mzozo katika maeneo mnakotoka."

Wimbi la wakimbizi limesababisha sintafahamu kubwa kati ya nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya na kuufanya mfumo wa kuifanya mipaka baina ya nchi hiyo kubakia wazi kukaribia kusambaratika.

Wahamiaji wote wapya wanaowasili wanashikiliwa Moria wakati wakisubiri kushughulikiwa kwa maombi yao kuyakinisha iwapo wana uhalali wa kudai kupatiwa hifadhi au wanapaswa kurudishwa kutokana na kuwa "wahamiaji wa kiuchumi."Mashirika ya haki za binaadamu yameishutumu Ugiriki kwa kukigeuza kituo hicho kuwa kambi ya mahabusu.

Mwandishi : Mohamed Dahman /AFP /Reuters

Mhariri : Sudi Mnette