1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa Francis kuongoza misa kubwa katika eneo la Aparacida Brazil

MjahidA24 Julai 2013

Kiongozi wa kanisa katoliki Ulimwenguni Papa Francis hii leo anatarajiwa kuongoza misa kubwa tangu alipowasili nchini Brazil siku ya Jumatatu. Papa ataongoza misa katika mji wa Aparacida ambao ni maarufu kwa mahujaji.

https://p.dw.com/p/19DY3
Papa Francis
Papa FrancisPicha: AFP/Getty Images

Kiongozi huyo wa kwanza kutoka Amerika ya Kusini anasubiriwa kwa hamu na ghamu katika eneo hilo la Aparecida.

Barabara za mji wa Rio de Janeiro hapo jana zilijaa waumini wengi waliokuwa na hamu ya kumuiona Papa.

Hata hivyo ziara hiyo ya kwanza ya Papa Francis nchini Brazil ambayo tayari inakumbwa na changamoto za kiusalama imekuja sambamba na tamasha la kimataifa la vijana linalowashirikisha mahujaji wapatao nusu milioni.

Uwezo wa nchi hiyo wa kukabiliana na umati huu mkubwa wa watu unaonekana kama jaribio la namna itakavyokabiliana na michezo ya kombe la dunia yanayotarajiwa kufanyika nchini humo mwaka wa 2016.

Papa Francis na rais wa Brazil Dilma Rousseff
Papa Francis na rais wa Brazil Dilma RousseffPicha: Reuters

Papa Francis ataoongoza misa ya takriban watu 15,000 ndani ya uwanja wa kanisa huku watu wengine takriban 200,000 wakiwa nje na polisi takriban 5000 pamoja na wanajeshi wakitarajiwa kuimarisha usalama.

Kulingana na wawakilishi wa papa Francis, nia ya kiongozi huyo wa kikatoliki wiki hii ni ya kuunganisha vijana na ujumbe wa kanisa huku akijaribu kulitakasa kanisa kutokana na kashfa za fedha na pia dhuluma za kimapenzi kwa watoto.

Maandamano wa matumizi makubwa ya fedha kwa ujio wa Papa

Kando na papa kuwa maarufu kote ulimwenguni ziara yake imekumbwa na maandamano ya kupinga matumizi ya juu ya fedha ya Takriban dola milioni 53 zilizotumika katika matayarisho ya kumpokea na kuandaa tamasha la kimataifa la Vijana.

''Tatizo ni serikali yetu. Ziara ya Papa itagharimu dola milioni 53, hizo ni pesa nyingi sana. Fedha hizo zingeweza kuwekezwa katika sekta ya afya au elimu''. Alisema mmoja wa waandamanaji

Baada ya Misa hiyo papa atapanda katika gari lililowazi kwa juu ili apate kuonekana, kisha gari hilo kuendeshwa takriban kilomita mbili kutoka eneo la mahujaji la Aparacida hadi katika seminari ya kikatoliki ya Bom Jesus ambapo atapata chakula cha mchana.

Maandamano Brazil
Maandamano BrazilPicha: Reuters

Papa Francis atakuwa papa wa tatu kutembelea eneo hilo la mahujaji baada ya John Paul wa pili kulitembelea mwezi Julai mwaka wa 1980, na papa Benedict wa 16 mwezi May mwaka wa 2007.

Mwandishi:Amina Abubakar/AFP

Mhariri:Yusuf Saumu