1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa Francis haendi DRC mpaka ifanye uchaguzi

Grace Kabogo
15 Septemba 2017

Mwakilishi wa kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis, katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, anasema kiongozi huyo hatoizuru nchi hiyo hadi hapo uchaguzi uliocheleweshwa kwa muda mrefu utakapofanyika.

https://p.dw.com/p/2k2pV
Vatikan Papst Franziskus hält Pfingsrede vor dem Petersdom
Picha: picture-alliance/dpa/S. Spaziani

Mwezi Machi mwaka huu, Papa Francis alifuta ziara yake ya Kinshasa iliyokuwa ifanyike wakati wa majira ya joto kutokana na mzozo wa kisiasa, ingawa alikutana na Rais Joseph Kabila mjini Vatican mwaka uliopita.

Monsinyoo Luis Mariano Montemayor amenukuliwa jana akisema Papa Francis anasikitishwa na hali inayoendelea kati ya viongozi kisiasa na wananchi wake.

Kauli hiyo ameitoa baada ya kulizuru jimbo la Kasai lenye utajiri wa madini ya almasi, ambako mashirika ya chakula ya Umoja wa Mataifa yameonya kuwa mamilioni ya watu wanakabiliwa na njaa kutokana na mzozo huo.

Kanisa Katoliki lina ushawishi mkubwa katika nchi hiyo yenye watu milioni 70 ambako nusu yake wanaifata imani ya kanisa hilo na mwezi Desemba mwaka uliopita lilikuwa mpatanishi katika mazungumzo ya kitaifa kati ya serikali na vyama vya upinzani, ambayo yanatarajiwa kuifanya nchi hiyo kufanya uchaguzi wake kabla ya kumalizika kwa mwaka huu.