1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Pelosi amwuunga mkono Dalai Lama

Mtullya, Abdu Said21 Machi 2008

Spika wa baraza la wawakilishi nchini Marekani Nancy Pelosi leo amekutana na kiongozi wa kidini wa Tibet Dalai Lama kaskazini mwa India.

https://p.dw.com/p/DSGu
Spika wa bunge la Marekani Nancy PelosiPicha: AP

Spika wa baraza la wawakilishi nchini Marekani Nancy Pelosi ameitaka jumuiya ya kimataifa ishutumu  utawala wa China katika jimbo la Tibet na hatua inazochukua  dhidi ya wapinzani.

Pelosi amesema  hayo leo baada ya kukutana  na kiongozi wa kidini wa Tibet Dalai Lama mjini Dharamshala,kaskazini mwa  India.

Bibi Pelosi ni mwanasiasa wa kwanza wa  ngazi za juu kutoka  Marekani kukutakana na Dalai Lama tokea ghasia zifumuke katika jimbo la Tibet wiki iliyopita.

Spika Pelosi amekutana na Dalai Lama wakati ambapo China na viongozi wa upinzani wa Tibet wanabishana juu ya idadi ya watu waliokufa kutokana  na ghasia hizo.Idara za serikali za China zimesema maafisa wake  waliwapiga risasi na kuwajeruhi wapinzani wanne mwishoni mwa wiki,  na inawalaumu wapinzani hao kwa kuwaua raia 13 baada ya ghasia kutokea  ijumaa iliyopita katika mji wa Lhasa ndani ya Tibet.Lakini   wawakilishi wa upinzani wa Tibet wanaoishi nje wamesema watu wapatao mia moja wameuliwa na polisi wa China  tokea machafuko hayo yaanze.

Akizungumzia hali ya jimbo la Tibet spika wa baraza la wawakilishi la Marekani bibi Pelosi  amesema ikiwa jumuiya ya kimataifa haitasema chochote juu ya utawala wa China katika Tibet, basi dunia itakuwa  imepoteza uadilifu wote juu ya  suala la haki zabinadamu.

Lakini kiongozi wa kidini wa Tibet mwenyewe Dalai Lama amesema pamoja  na kuungwa mkono kutoka nje,

suluhisho  linapaswa kufikiwa baina ya China na wawakilishi wa Tibet.

Wakati huo huo China imekiri kwa mara ya kwanza kuwa maafisa wake wa usalama waliwashambulia wapinzani wa Tibet kwa risasi wakati wanajeshi wake leo wameendela na msako katika sehemu  kadhaa huku kukiwa na wasi wasi juu ya wapinzani zaidi kutiwa ndani.