1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Polisi Washington wauza silaha zinazotumika katika uhalifu

9 Januari 2018

Uchambuzi uliofanywa kwa mwaka mmoja na AP umebaini kuwa silaha zaidi ya dazani zilizouzwa na  vitengo vya polisi  vya Washington, tangu mwaka 2010,baadaye zilitumika kama ushahidi katika uchunguzi wa uhalifu mpya.

https://p.dw.com/p/2qYeX
Halbautomatische Waffe
Picha: picture-alliance/AP Photo/A. Breed

Kuzitambua bunduki zilizouzwa na taasisi za sheria na kuzioanisha na uhalifu mpya, kunahitaji uchunguzi wa kina na dazani ya  kumbukumbu zilizochukuliwa kutoka katika mashirika binafsi.

Kwa kutumia rekodi hizo, Shirika la AP; lilitengeneza kanzidata ya silaha 6000 zilizouzwa na taasisi za kusimamia sheria tangu mwaka 2010.   Wakala wa vileo, tumbaku; silaha na milipuko,  walikataa kutoa taarifa kuhusu silaha zilizohusika katika uhalifu. Hivyo basi AP ilikusanya taarifa kutoka kwa mashirika binafsi na kuzilinganisha  na taarifa kutoka  katika  kanzidata yake  kwa kuangalia uwiano katika namba tambulishi, sifa na  muundo.

Zifuatazo ni taarifa kuhusu silaha zilizouzwa na taasisi za polisi na baadaye zilipatikana katika matukio ya uhalifu.

 Kitengo cha usalama cha Washington, kiliwauzia  silaha zilizotumika katika uhalifu, wafanyabiashara za bunduki mwaka 2010. Miongoni mwa silaha hizo ni pamoja na bastola aina ya Lorcin 380. Aprili 2015 mwanachama  wa genge hilo  alirusha risasi katika gari iliyokuwa imewabeba mke na mume waliokuwa na mtoto wao wa mwaka mmoja.  Risasi moja ilimpata mtoto kichwani na kumuua. Wakati wanapekua katika nyumba inayotumiwa mara nyingi na mtuhumiwa aliyefanya mauaji . Kitengo cha Polisi cha Kent, kilibaini bastola hiyo, aina ya  Lorcin 380 iliuzwa na kitengo cha doria.

Katika matukio mengine, ofisi ya msaidizi wa polisi katika jimbo la Pierce, mwaka 2014 iliuza orodha ya bunduki katika mnada ambapo pia iliuzwa bunduki aina ya shortgun ya Mobserg 12.  Oktoba 2016, Mtu mmoja kwa jina la Jaylen Bolar alimtumia ujumbe mama yake, akimtishia kumuua yeye pamoja na watu wengine. Mama wa mtoto huyo, Angela Almo, aliwasiliana na vituo vya afya ya akili, badala ya polisi kwa sababu alijua mtoto wake ana silaha, ikiwamo hiyo aina ya Mossberg. Bolar pia alitishia kumuua mwanamke aliyewahi kuwa bosi wake. Alipokamatwa na upekuzi kufanywa nyumbani kwake, ilibainika  kuwa kuna silaha mbili chumbani mwake. Moja ya silaha hizo ni ile ya Mossberg iliyouzwa na ofisi ya msaidizi wa polisi.

Makarow Pistole
Picha: Imageo

 Matukio mengine ya silaha hizo

Kitengo cha polisi cha Aberdeenm, kiliuza bastola aina ya Lorcin L380, Februari 2011. Mei 2016, kitengo cha polisi cha Kent, kiligundua gari lililoibwa,  likiwa limeegesgwa katika kijiji cha Benson, na kuikuta silaha hiyo chini ya kiti. Silaha hiyo, Lorcin Model L380 iliuzwa na polisi wa Aberdeen.  Watoto watatu, ambao waliiba gari hilo, walikuwa ni wahalifu.

Katika tukio jingine, Ofisi ya msaidizi wa polisi ya Kitsap, iliuza bastola aina ya Hi Point9 mm, Machi 2014. Oktoba 2015, ofisi ya msaidizi wa polisi ya Snohomish,  iliitikia wito wa simu ya dharura iliyotoka kwa mwanamke ambaye alisema amesikia milio ya risasi na alipokwenda nje, alikuta rafiki wa kiume wa binti yake akiwa amelewa na hajitambui.  Bastola aina ya Hi Point mm ilikuwa chini karibu na alipolala. Silaha hiyo, ni ile  iliyouzwa na ofisi ya polisi ya Kitsap. Uchunguzi ulibaini kuwa mtu huyo ni mhalifu na alizuiwa kumiliki silaha.

Mwandishi: Florence Majani(AP)

Mhariri: Saumu Yusuf