1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Raia wa Sudan washiriki katika uchaguzi mkuu

Admin.WagnerD13 Aprili 2015

Raia wa Sudan wameanza kupiga kura katika uchaguzi mkuu unaobashiriwa kumrejesha madarakani Rasi Omar Al Bashir ambaye ameliongoza taifa hilo kwa miaka 25

https://p.dw.com/p/1F6sx
Picha: AFP/Getty Images/A. Shazly

Vyama vikuu vya upinzani nchini Sudan vinaususia uchaguzi huo unaoanza leo hadi Jumatano na hivyo inamaanisha rais wa sasa Bashir, mgombea wa chama tawala cha National Congress Party NPC anachuana na wagombea kumi na watano wa vyama vidogo vya kisiasa visivyojulikana au wagombea huru.

Vyama vikuu vya upinzani vinavyoususia uchaguzi huo vimesema ukandamizaji wa wanasiasa wa upinzani, vyombo vya habari na asasi za kiraia unafanya mazingira kuwa magumu mno kugombea dhidi ya Bashir.

Upinzani wasusia uchaguzi

Taifa hilo la Sudan lina idadi ya watu milioni 38 na milioni 13.3 kati yao wamesajiliwa kama wapiga kura ila wengi wao wanatarajiwa kususia shughuli hiyo.Hii ndiyo mara ya kwanza Sudan inaendesha uchaguzi mkuu tangu nchi hiyo kugawanyika mara mbili wakati Sudan Kusini ilipojinyakulia uhuru kutoka kwa Sudan mwaka 2011.

Rais wa Sudan Omar al Bashir
Rais wa Sudan Omar al BashirPicha: Ashraf Shazly/AFP/Getty Images

Kiasi ya askari 70,00 wametumwa kushika doria katika zaidi ya vituo 7,000 vya kupigia kura kote nchii humo. Al Bashir ambaye aliingia madarakani mwaka 1989 baada ya mapinduzi ya seikali ameshinda katika chaguzi mara tatu.

Kiongozi hiyo mwenye umri wa miaka 71 anashutumiwa kwa kupitisha sheria ambazo zinampa nguvuzaidi madarakani, kukandamiza maandamano na kuwakamata wapinzani wake.

Mahakama ya kimataifa inayoshughulikia kesi za uhalifu ya ICC ilitoa kibali cha kukamatwa kwa Rais huyo wa Sudan kwa madai ya kuhusika katika uhalifu wa kivita na mauaji ya halaiki katika eneo la Darfur mwaka 2008.

Katika kipindi cha kampeini, Bashir aliahidi kuuoboresha uchumi wa nchi yake ambako mfumko wa bei na ukosefu wa ajira uko kiwango cha juu na pia ameahidi kudumisha uthabiti na kuonya kuingia madarakani kwa utawala mpya ni hatari kwa kanda hiyo ikizingatiwa mizozo inayoendelea Libya,Yemen na kwingineko.

Nchi za magharibi zatilia shaka uhalali wa uchaguzi

Umoja wa Ulaya umeonya kuwa uchaguzi huo mkuu hauwezi kutoa matokeo halali yatakayokubalika kote nchini humo. Norway, Uingereza na Marekani pia zimesema hakuna mazingira muafaka ya kuendesha uchaguzi huru na wa haki nchini Sudan.

Wapiga kura wakipiga kura vituoni
Wapiga kura wakipiga kura vituoniPicha: AFP/Getty Images/A. Shazly

Tume ya uchaguzi nchini Sudan imesema waangalizi wa asasi za kimataifa wakiwemo wa kutoka jumuiya ya nchi za kiarabu, Umoja wa Afrika na jumuiya ya ushirikiano wa nchi za mashariki na pembe ya Afrika IGAD wanafuatilia chaguzi hizo. Shughuli ya kuhesabu kura inatarajiwa kuanza siku ya Alhamisi na matokeo rasmi hayatatangazwa kabla ya tarehe 27 mwezi huu.

Wapiga kura pia watawachagua wabuge wa kitaifa na wa majimbo katika chaguzi hizo za siku tatu ambapo chama tawala kinatarajiwa kushinda viti vingi. Serikali ya Sudan imetangaza siku ya mapumziko ili kuwaruhusu wapiga kura kujitokeza kushiriki katika shughuli hiyo.

Mwandishi: Caro Robi/dpa/Afp/Reuters

Mhariri: Yusuf Saumu