1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Raia wakimbia kutoka Ghouta mashariki

Sekione Kitojo
17 Machi 2018

Mashambulizi ya anga yamewauwa dazeni kadhaa za raia Ghouta mashariki Ijumaa (16.03.2018)na maelfu wengine kulazimika kukimbia, wakati majeshi ya Syria yakiendelea na mashambulizi makali katika ngome ya mwisho ya waasi.

https://p.dw.com/p/2uV11
Syrien Massenflucht aus Ghuta
Picha: Getty Images/AFP/L. Beshara

Vifo  hivyo vya  hivi  karibuni  kabisa  vimefikisha  idadi  jumla ya mashambulizi yaliyodumu karibu  mwezi  mmoja  kufikia  watu 1,350,  huku  mataifa  makubwa  duniani  bado yakishindwa  kuzuwia  moja kati  ya  mizozo  mibaya  kabisa iliyosababisha  uharibifu.

Vita  nchini  Syria  vinaingia mwaka  wa  nane  kwa mashambulizi mengine  yanayosababisha  mauaji yakijitokeza  pia  upande  wa kaskazini, ambako majeshi  yanayoongozwa  na  Uturuki yameendelea  na  mashambulizi kulikamata jimbo  linaloishi  Wakurdi wengi  la  Afrin.

Syrien Massenflucht aus Ghuta
Misururu ya watu wakikimbia kutoka Ghouta masharikiPicha: Getty Images/AFP/L. Beshara

Operesheni  hiyo imesababisha  maelfu  ya  watu  kukimbia, huku mashambulizi  ya  mabomu  dhidi  ya  mji  wa  Afrin jana  Ijumaa yakiuwa  watu 43, theluthi  yao  wakiuwawa  katika  mashambulizi ya anga katika  hospitali.

Ukingoni mwa  mji  wa  Ghouta, eneo  kubwa linaloishi  watu  wa vijijini likiwa umbali mfupi  kutoka Damascus na rahisi  kufika makombora, zaidi ya  raia  2,400 walikimbia  kutoka  katika  miji iliyoharibiwa, wakibeba vitu  vichache katika  mifuko  na vilivyofungwa  katika  nguo.

Makundi ya  watu  yalijikusanya  katika  vituo  vya  serikali nje kidogo  ya  Ghouta  mashariki jana  Ijumaa, wakiwa  hawana uhakika watafanya  nini baada  ya  hapo  baada  ya  kuingia  moja kwa  moja  katika  udhibiti  wa  majeshi  ya  serikali  ambayo yamekuwa  yakishambulia  bila  kukoma nyumba  zao kwa  wiki kadhaa.

"Tulikuwa  tuna hofu ya  kuondoka, walituambia  jeshi  litatukamata," alisema  Abu Khaled  mwenye  umri  wa  miaka  35, ambaye  alikuwa akifanya  biashara  ya  kuuza  nguo mjini  Ghouta.

Syrien Flüchtlinge aus Ost-Ghuta
Watu darzeni kadhaa wakiwa katika maeneo ya serikali kutoka Ghouta masharikiPicha: Imago/Xinhua

"Tulikutana  na  jeshi  na  hatukuona  hivyo, lakini sasa  kimsingi tunaishi kambini," aliliambia  shirika  la  habari  la  Ufaransa  AFP.

Watu wengi zaidi wamekimbia

Balozi wa  Syria  katika  Umoja  wa  Mataifa  Bashar al-Jaafari amesema watu 40,000  wamekimbia  kutoka  Ghouta siku  ya Alhamis, na hatua  hiyo  ya  kukimbia watu  kwa  wingi inaonekana kutokea  bila  ya  serikali  kujitayarisha.

Misururu  mirefu ya  watu  ilionekana  nje  ya  vyoo  vya  umma, na familia  zilizokimbia  makaazi  yao  zililalamikia kukosekana  kwa  maji ama  magodoro.

Katika  ujumbe uliotangazwa kupitia  televisheni  ya  taifa  jeshi  la Syria  liliwataka  raia  wote kutumia eneo  maalum  lililotengwa na jeshi  hilo  kuondoka  kutoka  katika  eneo  hilo, likisema  limekamata asilimia  70  ya ardhi  iliyokuwa  ikidhibitiwa  na  waasi.

Mashambulizi  ya  ardhini  yaliyokuwa  yakifanywa  na  jeshi  la Syria  pamoja  na  wanamgambo  washirika wao yameligawa  eneo la  Ghouta  mashariki  katika  sehemu  mbali  mbali, kila  moja  likiwa linashikiliwa  na  kundi  tofauti.

Genf Syrischer UN-Botschafter Bashar al-Jaafari
Balozi wa Syria katika Umoja wa Mataifa Bashar al-JaafariPicha: Getty Images/AFP/F. Coffrini

Yale makundi matatu  ya  wapiganaji  wa  Kiislamu  yamesema  jana Ijumaa yatakuwa  tayari  kufanya  majadiliano  ya  moja  kwa  moja na  Urusi  kuhusiana  na  usitishaji  mapigano  katika  Ghouta, lakini hayakutaja  mazungumzo na  serikali  ya  Syria.

Taarifa  yao imekuja  masaa  machache  baada  ya  mjumbe  maalum wa  Umoja  wa  Mataifa  nchini  Syria Staffan de Mistura  kusema mazungumzo  yanaendelea  kati  ya  Urusi  na  moja  kati  ya makundi, Jaish al-Islam.

Mazungumzo  hayo  tayari  yamesababisha  kuwapo  na  siku  sita za  utulivu katika  mji  mkubwa wa eneo  la  Ghouta wa  Douma. Mji wa Douma  pia ulishuhudia  upelekaji  wa  chakula, na  mamia  ya raia  walipata usafiri  wa  mabasi  kuondoka  kutoka  katika  mji  huo kama  sehemu ya kuwaondoa  watu  kwa  ajili  ya  kupatiwa matibabu.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afpe

Mhariri: Yursa Buwayhid