1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Raila apinga mwito wa kushiriki katika serikali ya umoja wa taifa

Oummilkheir6 Januari 2008
https://p.dw.com/p/Cl1f

Mjumbe maalum wa Marekani Jendayi Frazer anaendelea na juhudi za upatanishi kumaliza mzozo wa kisiasa unaoitikisa Kenya,kufuatia uchaguzi wa rais unaobishwa.Baada ya mazungumzo pamoja na rais Mwai Kibaki,hapo jana,bibi Jendayi Frazer alisema pande zote mbili zimekubaliana matumizi ya nguvu yakome.Wakati huo huo mwenyekiti wa Umoja wa Afrika,rais John Kufour wa Ghana anatazamiwa kuwasili Kenya wakati wowote kutoka sasa.Rais Mwai Kibaki amekubali pendekezo la kuundwa serikali ya umoja wa taifa.Pendekewzo ,hilo lakini linapingwa na upande wa upinzani unaoongozwa na Raila odinga.Juhudi za pamoja za upatanishi kati ya Umoja wa Afrika na jumuia ya madola Commonwealth zimefifia baada ya kuondoka Nairobi mjumbe maalum wa jumuia hiyo,rais wa zamani wa Sierra Leone Ahmed Teja Kabbah.Upande wa upinzani unaoongozwa na Raila Odinga unashurutisha kushiriki katika meza ya mazungumzo ya amani na kubatilishwa ushindi wa rais Mwai Kibaki katika uchaguzi wa rais December 27 iliyopita.Upande wa upinzani unadai pia upatanishi wa kimataifa kwa mzozo wa Kenya.Zaidi ya watu 350 wamepoteza maisha yao kufuatia machafuko yaliyosababishwa na matokeo hayo ya uchaguzi.Na zaidi ya laki mbili wameyapa kisogo maskani yao.