1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bashir: Mitandao ya kijamii haiwezi kuwatoa marais uongozini

Amina Mjahid
31 Januari 2019

Rais wa Sudan Omar al Bashir amedhihaki hatua zinazochukuliwa na wapinzani wake za kutumia mitandao ya kijamii kushinikiza maandamano dhidi ya utawala wake, akisema mitandao hiyo haiwezi kuwaondoa marais madarakani.

https://p.dw.com/p/3CWyk
Türkei Ankara - Sudans Präsident - Omar Bashir
Picha: picture-alliance/AP Photo/B. Ozbilici

Waandaaji wa maandamano ya kuipinga serikali ya Bashir yalioitikisa Sudan kwa wiki kadhaa, wametumia mitandao ya kijamii kama Facebook, WhatsApp na Twitter, kushinikiza maandamano hayo.

Sudan Rede von Präsident Omar al-Bashir
Rais wa Sudan Omar al-BashirPicha: Getty Images/AFP/A. Shazly

"Kubadilisha serikali au marais hakuwezi kufanyika kupitia WhatsApp au Facebook," kunaweza tu kufanyika kupitia uchaguzi, ni watu pekee ndio wanaoamua nani atakuwa rais." alisema rais Bashir katika mkutano wake uliotangazwa kupitia televisheni ya kitaifa na uliohudhuriwa na wafuasi kwake katika mji wa Mashariki wa Kassala, wakati alipokuwa akifungua mpaka wa Sudan na Eritrea uliofungwa kwa muda mrefu na kuathiri eneo hilo kiuchumi.

Wanaharakati wamehifadhi matukio yote ya maandamano yalioanza tarehe 19 mwezi wa Desemba yaliosababisha vifo vya watu 30 huku video na picha za maandamano hayo pamoja na vurugu kati ya waandamanaji na vikosi vya usalama zikisambaa katika mitandao ya kijamii.

Maandamano yanaendeshwa na chama cha wataalamu wa Sudan SPA, kinachotoa matangazo ya moja kwa moja mitandaoni juu ya maandamano hayo kikitumia hastagi kama  #Sudan_cities_uprise 'Uasi miji ya Sudan' au #Just_Fall. 'Ng'atuka tu'

Hashtag nyengine kama #SudanRevolts 'Uasi wa Sudan'  na #SudanUprising pia zimesaidia kuzidisha kasi ya maadnamano huku zikiwekwa mara kadhaa chini ya saa moja.

Wanaharakati wasema serikali ya Bashir yataka kudhibiti matimizi ya mitandao ya kijamii

WhatsApp Logo
Nembo ya mtandao wa kijamii wa Whats upPicha: picture-alliance/dpa/S. Stein

Hata hivyo wanaharakati na wachambuzi wanasema kwa sasa serikali ya Sudan inataka kupunguza matumizi ya mitandao. Watumiaji wameripoti ugumu wa kufikia mitandao ya Facebook, Twitter na WhatsApp tangu siku za mwanzo za maandamano hayo yalioanzia mjini Atbara kufuatia hatua ya serikali kupandisha mara tatu bei ya mikate.

Lakini maandamano hayo yaliogeuka kuwa maandamano ya kitaifa yanaonekana kuwa kitisho kikubwa kwa utawala wa Bashir tangu alipoingia madarakani kupitia mapinduzi mwaka 1989. Hasira zimekuwa zikiongezeka kwa miaka kadhaa kufuatia hali mbaya ya maisha na uchumi kuzidi kudorora.

Matatizo ya kiuchumi  Sudan yalisababisha maandamano mwaka 2013 na 2016 yaliodhibitiwa kutokana na mauaji ya wengi lakini kwa wakati huu licha ya rais Bashir kutoa miito ya uvumilivu, chuki dhidi ya sera zake zinaongezeka.

Mwandishi: Amina Abubakar AFP

Mhariri: Iddi ssessanga