1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais mpya wa Afghanistan kuapishwa

28 Septemba 2014

Afghanistan itafanya sherehe kubwa za kuapishwa kwa rais mpya wa nchi hiyo Jumatatu(29.09.2014)ambapo Ashraf Ghani msomi ambaye aliwahi kuwa na makaazi yake nchini Marekani akichukua madarakani nchini humo.

https://p.dw.com/p/1DMBS
Afghanistan Stichwahl für das Präsidentenamt 14.6.2014
Rais mpya wa Afghanistan Ashraf GhaniPicha: Reuters/Omar Sobhani

Wakati huo huo majeshi yanayoongozwa na NATO yanafikisha mwisho miaka 13 ya vita bila ya kupata ushindi dhidi ya kundi la Taliban.

Ghani anachukua madaraka kutoka kwa rais anayeondoka madarakani Hamid Karzai baada ya mkwamo wa zaidi ya miezi mitatu kuhusiana na mzozo wa matokeo ya uchaguzi ambao umechochea mapigano na kuharibu mwelekeo wa kiuchumi wa Afghanistan.

Afghanistan Präsidentschaftswahl Kandidat Abdullah Abdullah Archiv 11.06.21014
Mgombea wa kiti cha urais Abdullah AbdullahPicha: Wakil Kohsar/AFP/Getty Images

Sherehe hizo zitakuwa za mara ya kwanza kwa nchi hiyo kubadilisha madaraka kidemokrasia, hali inayoonekana na wafadhili wa kimataifa kuwa muhimu baada ya vita vilivyokuwa na gharama kubwa pamoja na uingiliaji kati wa kiraia tangu kuanguka kwa utawala wa Taliban mwaka 2001.

Uchaguzi uliogubikwa na udanganyifu

Ghani na hasimu wake katika uchaguzi Abdullah Abdullah, mpiganaji wa zamani dhidi ya kundi la Taliban , wamedai kushinda uchaguzi huo uliogubikwa na udanganyifu mkubwa wa wizi wa kura uliofanyika hapo Juni 14 mwaka huu , na kuitumbukiza Afghanistan katika mzozo ambao ulitishia kuzusha ghasia nchi nzima.

Lakini chini ya mbinyo mkubwa kutoka Marekani na Umoja wa Mataifa, wagombea hao wawili walikubaliana kuunda serikali ya umoja wa kitaifa , na Ghani alitangazwa kuwa rais baada ya uhakiki wa kura zote karibu milioni nane zilizopigwa.

Demonstration in Kabul Wahlergebnisse Präsidentschaftswahl
Maandamano mjini Kabul kuhusiana na uchaguzi nchini AfghanistanPicha: DW/H. Sirat

Abdullah pia ataapishwa Jumatatu(29.09.2014) kuwa mtendaji mkuu, jukumu jipya sawa na waziri mkuu , katika mfumo wa serikali ambayo ni tofauti kabisa na rais Karzai ambaye alikuwa na madaraka yote.

Karzai amekuwa na uhusiano ambao si mzuri na muungano wa majeshi ya NATO yanayoongozwa na Marekani pamoja na waungaji wengine mkono wa kimataifa ambao wanaingiza fedha zao katika nchi hiyo iliyoharibiwa kwa vita, lakini ameweza kupata fursa ya maridhiano katika siku zake za mwisho akiwa madarakani.

"Naweza kusema kwa kujiamini kabisa kwamba Afghanistan hivi karibuni inashuhudia amani na uthabiti, na rais mpya na serikali yake itapata uungwaji mkono wenu," amewaambia mabalozi wa nje katika mkutano wake wa kuwaaga jana Jumamosi(27.09.2014).

Einigung über Einheitsregierung in Afghanistan unterzeichnet 21.9.2014
Mapatano kati ya Abdullah Abdullah(shoto) na Ashraf Ghani(kulia)Picha: Reuters

"Hivi sasa tunawaona watoto wakienda shule, barabara zinajengwa, maendeleo katika sekta ya afya na bendera ya Afghanistan inapepea kwa fahari duniani kote--haya ni kwa sababu ya msaada wa kimataifa na usaidizi.

Chini ya utawala wa Taliban mwaka 1996-2001, wasichana walipigwa marufuku kupata elimu na wanawake hawakuruhusiwa kutoka nje hadi pale wanapovaa burqa na wakiandamana na mwanamume.

Televisheni na muziki pia vilipigwa marufuku na wanaume walipigwa kwa kutofuga ndevu.

Ghani na Abdullah ni wenye misimamo wa wastani, wanaopendelea viongozi wa magharibi ambao wameapa kusonga mbele kusukuma maendeleo madogo yaliyofikiwa pamoja na maendeleo ya miundo mbinu tangu mwaka 2001, lakini nchi hiyo bado inakabiliwa na kitisho kikubwa kutoka kwa wanamgambo wa Taliban.

Karsai mit Abdullah und Ghani Jahrestag der Unabhängigkeit 19.08.2014
Rais anayeondoka madarakani Hamid KarzaiPicha: Reuters

Wanajeshi wa Afghanistan pamoja na polisi wamekuwa wakisumbuka kuwazuwia wapiganaji wa Taliban , huku ghasia zikiongezeka katika majimbo mengi.

Shughuli za NATO zimepunguzwa kwa kiasi kikubwa na ujumbe wake wa mapambano utafika mwisho mwishoni mwa mwaka huu. Ni vituo 33 tu vya NATO ambavyo hadi sasa vinaendelea na shughuli, ikiwa ni chini kutoka vituo 800, na kuliacha jeshi la nchi hiyo kupambana na Taliban likiwa na usaidizi unaozidi kupungua kila wakati.

Mwandishi: Sekione Kitojo / afpe

Mhariri: Sudi Mnette