1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais mpya wa Ujerumani aapishwa

Sekione Kitojo2 Julai 2010

Christian Wulff, mwenye umri wa miaka 51, ameapishwa kushika wadhifa wa urais nchini Ujerumani leo Ijumaa akiwa rais wa kumi.

https://p.dw.com/p/O9Nu
Rais mpya wa Ujerumani Christian Wullf akiapa katika kikao cha bunge mjini Berlin, siku ya Ijumaa Julai 2, 2010.Picha: AP

Christian  Wulff,  mwenye  umri  wa  miaka  51, ameapishwa  kushika  wadhifa  wa  urais  nchini  Ujerumani leo  Ijumaa  akiwa   rais  wa  10. Waziri  mkuu  huyo  wa zamani  wa  jimbo  la  Lower Saxony , kutoka  chama  cha kansela  wa  Ujerumani  Angela  Merkel  cha  Christian Democratic  Union, alichaguliwa   kushika  wadhifa  huo siku  ya  Jumatano  wiki  hii, baada  ya  duru  tatu  za uchaguzi.

"Naapa  kutumia  uwezo  wangu  kuitumikia  jamii  ya Wajerumani, kuwaongezea  neema  na  kuwaepusha  na madhara. Nitailinda  katiba  na  sheria  za  nchi  hii, na kutekeleza  majukumu  yangu  kwa  kadiri  ya  uwezo wangu, na  kumtendea  haki  kila  mtu. Mungu  nisaidie."

Hayo  ni  maneno  ya  kuapa  aliyoyasema  rais  mpya  wa Ujerumani  Christian  Wulff  mjini  Berlin  leo katika  kikao cha  pamoja  cha  mabaraza  ya  bunge  la  wawakilishi  wa majimbo, Bundesrat  na  lile  la  shirikisho  la Bundestag.

Rais  huyo  mpya  wa  Ujerumani  Christian  Wulff aliapishwa  leo  Ijumaa  baada   ya  uchaguzi  mapema wiki  hii uliogeuka  kuwa   pigo  kwa  kansela  wa Ujerumani  Angela  Merkel.

Kwa  mara  nyingine  tena  kumekuwa  na  uchaguzi  wa kweli  kwa  wadhifa  wa   rais  wa  shirikisho  la  Ujerumani, amesema  Wulff  kutoka  chama  cha  kihafidhina  cha Christian  Democratic.

Kila unapofanyika  uchaguzi  wa  haki  ni   kitu  kizuri  kwa ajili  ya  demokrasia  yetu.

Rais  huyo  mpya   Christian  Wulff  anapendelea  kuona ukuaji  wa  pamoja  wa  sekta  mbali  mbali  za  jamii  ya Ujerumani. Nguvu  kubwa  ya  Ujerumani   ni  watu  wake, amesema  Wulff. 

Anataka  kuimarisha  mshikamano  baina  ya  vijana  na wazee, baina  ya  watu  kutoka  mashariki  na  magharibi ya  Ujerumani,  wahamiaji  na  watu wenye  asili  ya Ujerumani, waajiri  na  waajiriwa  pamoja  na  wale  ambao hawana  ajira, watu  wenye  ulemavu  na  wasio  walemavu.

Wulff  amedai  kuwa  unahitajika  mshikamano  zaidi badala  ya  mtengano. Kwa  hiyo  kutapatikana   kitu  kipya kizuri  kutokana  na  utamaduni   wa   nidhani  ya Kijerumani  ukichanganywa  na  uwezo  wa  kupenya penya wa  Kituruki  kwa  mfano,  urithi  wa  utamaduni  wa Kiprasha  wa  nidhamu  ya  uwajibikaji  na  mchanganyiko wa  utamaduni  wa   Kiingereza  na  Kijerumani, usiohitaji hali  ya  kuharakishwa, msingi  wa  maisha  ya  watu  wa eneo  la  kati  la  Ujerumani, pamoja  na  aina  ya  maisha ya  Kitaliani.

Kwa  upande  wa  vyama  ametoa  wito  kupambana  na hali  ya mivutano  ya  kisiasa.

Na  pia   raia  ambao  hawajishughulishi  na  vyama, wanapaswa  kupewa  kwa  wepesi  uzoefu,  wawapo  katika kazi  zinazohusu  vyama.

Waziri  mkuu  huyo  wa  zamani  wa  jimbo  la  Lower Saxony  alichaguliwa  katika  wadhifa  huo  baada  ya mtangulizi  wake Horst Koehler  kutangaza  kujiuzulu ghafla  mwezi  mmoja  uliopita.

Spika  wa  bunge  la  Ujerumani  Norbert Lammer alimsifu rais  wa  zamani  Koehler  na  kusema kuwa  aliyachukulia matatizo  ya  watu  na  mahitaji  yao  kwa  dhati, na wanampa  shukrani  kwa  mapenzi  ambayo  hayatakwisha.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / DPAE / RTRE

Mhariri : Josephat Charo