1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Putin ziarani mjini New Delhi

11 Desemba 2014

Rais Vladimir Putin wa Urusi yuko ziarani India kuzungumzia ushirikiano wa kibiashara na nishati,katika wakati ambapo vikwazo vya nchi za magharibi vinatishia kuzorotesha shughuli za kiuchumi nchini mwake.

https://p.dw.com/p/1E2WR
Rais Putin (kushoto) akikaribishwa na waziri mkuu wa India ModiPicha: Reuters/A. Abidi

Mazungumzo ya rais Vladimir Putin pamoja na waziri mkuu wa India Narendra Modi yamelenga namna ya kuimarisha ushirikiano katika wakati ambapo New Delhi inaangaliwa kuijongelea zaidi Marekani hasa katika sekta za ulinzi na uwekezaji.

Mafisa wa serikali ya India wanasema makubaliano karibu 20 kuhusu miongoni mwa mengineyo ushirikiano wa anga za juu,ulinzi na pia nishati yatatiwa saini.

Muda mfupi kabla ya kuwasili mjini New Delhi rais Putin alinukuliwa akisema amedhamiria kuimarisha " ushirikiano maalum wa kimkakati" pamoja na New Delhi,akitaja uwezekano wa kufikiwa makubaliano kuhusu mitambo mipya ya nuklea na kuhusu biashara ya vifaa vya kijeshi.

Uhusiano kufikishwa "kipeo kipya"

Kwa upande wake waziri mkuu Modi ameamesema kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter "uhusiano kati ya wananchi wa Urusi na India ni madhubuti" na kwamba anataraji kuufikisha katika "kipeo kipya."

Indien - Der russische Präsident Wladimir Putin in Neu Delhi
Rais Putin akiamkiana na balozi wa Urusi mjini New Delhi baada ya kuwasiliPicha: picture-alliance/dpa/Michael Klimentyev

Ziara ya Putin inafanyika katika wakati ambapo Urusi inazongwa na kishindo cha kuporomoka bei ya mafuta na kupungua thamani sarafu ya nchi hiyo-Rubble.

Uhusiano wa Urusi na nchi za magharibi umedhoofika tangu nchi hiyo ilipoliteka jimbo la Ukraine la Crimea mwezi Machi mwaka huu.

Mkutano huu wa kilele wa kila mwaka utazifungulia njia nchi hizo mbili kutathmini ushirikiano maalum na wa kimkakati wanaojivunia" amesema Ajay Bisaria,afisa wa ngazi ya juu katika wizara ya mambo ya nchi za nje ya India."Hii ni ziara muhimu,Urusi ni mshirika wetu mkubwa wa sekta ya ulinzi na itaendelea kuwa hivyo kwa miongo kadhaa inayokuja-amesisitiza.Hata hivyo India itataka kupata hakikisho kutoka kwa rais Putin kwamba matatizo ya Urusi pamoja na ulimwengu wa magharibi hayatakuwa sababu ya kuijiongeza zaidi nchi hiyo na China.

Kiongozi wa Crimea pia mjini New Delhi

Wakati huo huo kiongozi wa jimbo lililounganishwa na Urusi la Crimea Sergey Aksyonov amewasili pia New Delhi kwa ziara ambayo si rasmi.Amekutana na wafanyabiashara wa India wa kile kinachojulikana kama "jumuia ya ushirikiano kati ya India na Crimea na kuzungumzia namna ya kuimarisha biashara pamoja na jimbo hilo linalopakana na bahari nyeusi.

Fährenverbindung zwischen der Krim und Russland
Mawasiliano kwa njia ya baharini Kati ya Urusi na CrimeaPicha: DW/A. Miroschnitschenko

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AP/Reuters

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman