1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Colombia aonya kuwa mateka wote watakombolewa

Kalyango Siraj3 Julai 2008

Ingrid Betancourt aunganishwa tena na familia yake

https://p.dw.com/p/EVwb
Alvaro Uribe kulia na Ingrid Betancourt kushoto mjini Bogoto baada ya kukombolewa kutoka mikononi ya waasi wa FARCPicha: AP

Rais wa Colombia Alvaro Uribe ameapa kuwa mateka wote waliosalia mikononi mwa waasi wa FARC watakombolewa kwa njia moja ama nyingine.

Na kwa mda huohuo mwanasiasa mashuhuri nchini Colombia aliekuwa mikononi mwa waasi ameungana na familia yake kwa mara ya kwanza baada ya kupoteana kwa kipindi cha miaka sita.

Bi Ingrid Betancourt,mwanasiasa mashuhuri wa Colombia ambae pia anauraia wa Ufaransa na ambae alikombolewa jana kutoka mikononi mwa waasi wa FARC na jeshi la Colombia hatimae ameungana na familia yake.

Watoto wake wawili Melanie na Lorenzo wamekutana na mamayao alhamisi katika uwanja wa ndege wa Bogota baada ya mda wa miaka sita.

Katika hotuba fupi katika uwanja wa ndege Bi Betancourt amesema kuwa baada ya kuwa huru ataanza juhudi za kuona kama anawakutanisha pamoja rais wa Colombia pamoja na cheo somo wake wa Venezuela Hugo Chaves kuona kama mateka wengine waliosalia wanaachiliwa huru.

Aidha amesema yuko tayari kushiriki katika maandamano ya amani,ingawa hajui yatafanyika lini.Mmoja wa watoto wake alipoulizwa alihisi vipi kuhuru operesheni ya kumuokoa mamke alisema kuwa walikuwa na wasiwasi kuwa huenda mama yao au wengine wakaumia au kufa kutokana na risasi.

Lakini ilifana sana bila hata kufyatua risasi.

Kutokana na operesheni hiyo kufana, rais wa nchi hiyo Alvaro Uribe amesema kuwa , mateka wote walioko katika mikono ya waasi wa kikomunisti wa kundi la FARC watakombolewa.Hakusema kwa njia gani.

Kundi la FARC limeendesha vita vya msituni kwa kipindi cha miaka 40 sasa.

Limekuwa likitumia mbinu kadhaa dhidi ya serikali ya Bogota katika vita vyake.Miongoni vya mbinu hizo ni kuteka nyara watu mashuhuri au wanajeshi wa serikali.Mateka hao hutumiwa kama karata ya turufu.

Serikali imewakamata waasi wengi pamoja na wasaidizi wao na kuwaweka kizuizini.Waasi nao kila mara wamekuwa wakiitaka serikali kuwachiliwa watu wao kwanza ili nao kufanya hivyo.

Haijulikani ni mateka wangapi walioko katika mikono ya waasi hao.

Bi.Ingrid Betancourt alikuwa miongoni mwa mateka mashuhuri wa waasi hao.Aliwahi wakati moja kupigania kiti cha urais.Mama huyo alikamatwa miaka sita iliopita.Na juhudi za kimataifa zimekuwa zikichukuliwa ili kutaka aachiliwe huru.

Miongoni mwa watu wengine 14 waliokombelewa nae jumatano na makando wa jeshi la Colombia ni raia watatu wa Marekani.Waliosalia walikuwa wanajeshi wa Colombia waliochukuliwa wanashikiliwa.