1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Italia ahitaji muda kuamua

30 Januari 2008
https://p.dw.com/p/CzXZ

Rais wa Italia, Giorgio Napolitano, amesema anahitaji muda zaidi kuamua ikiwa aitishe uchaguzi wa mapema au aunde serikali ya mpito kufuatia kujiuzulu kwa waziri mkuu wa nchi hiyo, Romano Prodi, wiki iliyopita.

Rais Napolitano ameyasema hayo baada ya kukamilisha mazungumzo ya siku nne na viongozi wa kisiasa akiwemo kiongozi wa chama cha upinzani cha Forza Italia, waziri mkuu wa zamani Silvio Berlusconi, anayeshinikiza uchaguzi uitishwe mara moja nchini Italia.

Kwa mujibu wa kura za maoni Berlusconi huenda akashinda na kurudi madarakani iwapo uchaguzi wa mapema utaitishwa nchini Italia.

Chama cha Romano Prodi kwa upande wake kinapendelea kuundwe serikali ya mpito itakayoendeleza mageuzi ya sheria za uchaguzi wazo ambalo linapingwa na Silvio Berlusconi.

Rais Napolitano amesema ni vigumu kuamua kutokana na mipasuko ya kisiasa na hajasema anahitaji muda gani kufikia uamuzi wake.