1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Buhari arudi Nigeria

10 Machi 2017

Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari amerudi nyumbani Ijumaa baada kuwepo Uingereza kwa muda wa miezi miwili kwa ajili ya matibabu. Lakini haijaelezwa sababu za kukaa muda mrefu nje ya nchi.

https://p.dw.com/p/2Ywir
Muhammadu Buhari Nigeria
Rais wa Nigeria Muhammadu BuhariPicha: picture alliance/AP Photo/S.Alamba

Buhari ambaye ana umri wa miaka 74, alishuka kwenye ndege yake bila ya msaada wowote baada ya ndege hiyo kutua katika uwanja wa ndege wa jeshi la anga uliopo kaskazini katika mji wa wa Kaguna.

Mpaka sasa hakujatolewa  habari zaidi na hakuna ufafanuzi wowote juu ya hali yake na maradhi aliyokuwa nayo.  Picha zilizochapishwa na ofisi yake zinamuonesha Buhari akiwa amekonda, lakini mwenye tabasamu alipokuwa akisalimiana na askofu mkuu wa Canterbury Justin Welby kabla ya kuondoka mjini London.

Rais huyo aliondoka mjini Abuja tarehe 19 Januari kwa nia ya kukaa siku kumi tu Uingereza kwa ajili ya matibabu, lakini alilazimika kuongeza muda wake baada ya kushauriwa na madaktari.

Buhari kabla ya safari yake  alimtaka makamu wake Yemi Osinbajo, kuongoza nchi. Yemi Osinbajo ambaye pia ni mwanasheria, alikuwa na jukumu muhimu  katika mikutano ya baraza la Nigeria na kumalizia mipango ya mabadiliko ya kiuchumi, ikiwamo kupigana kupata mkopo kutoka benki ya dunia .

Mbali na hayo safari hiyo ya matibabu ya rais Buhari imezusha gumzo nchi humo. Baadhi  ya watu walionyesha hasira na kusema kuwa  matibabu hayo yanafadhiliwa na walipa kodi na pia maafisa ya ngazi za juu ndio wanaopata matibabu bora na kusafiri nje kufuata matibatu, huku raia wa kawaida wanahangaika ndani ya nchi kutafuta huduma bora za matibabu.

Wengine walipendekeza kwamba Makamu Rais Yemi Osinbajo, mwenye umri wa miaka 54,  anendelee kuiendhesha nchi badala ya rais Muhammadu Buhari.

Mwandishi: Najma Said

Mhariri: Iddi Ssessanga