1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Shirikisho la Kandanda la Misri ajiuzulu

Bruce Amani
7 Julai 2019

Rais wa chama cha mpira wa miguu cha Misri Hany Abou Rida amejiuzulu na kuipiga kalamu timu yake ya kiufundi baada ya wenyeji wa Misri kuondolewa katika Kombe la Mataifa ya Afrika.

https://p.dw.com/p/3LhbK
Africa Cup of Nations 2019 - Ägypten vs Südafrika - Tor durch Thembinkosi Lorch
Picha: Reuters/A. Abdallah Dalsh

Taarifa ya chama cha kandanda imesema uamuzi huo ni wajibu wa kimaadili baada ya timu ya taifa kuduwazwa kwa kufungwa 1 – 0 na Afrika Kusini, ikiongeza kuwa wanachama wote wa bodi wameombwa kujiuzulu.

Kocha wa Misri Javier Aguirre amesema anabeba lawama kutokana na matokeo hayo ya kushangaza na akadokeza kuwa atafanya mazungumzo na chama cha kandanda cha Misri kuhsu mustakabali wake.

Misri walipigiwa upatu kubeba kombe hilo katika ardhi ya nyumbani lakini ikakutana na Afrika Kusini ambayo ilipena tu katika hatua ya mtoani kupitia nafasi nne za mwisho zilizowekewa timu ambazo zilikuwa bora katika nafasi ya tatu kwenye makundi yao. Thembinkosi Lorch alifunga bao hilo pekee la ushindi katika dakika ya 85 kwa upande wa Afrika Kusini

Afrika-Cup 2019 Achtelfinale | Ägypten vs. Südafrika
Misri walipigiwa upatu kutwaa kombe nyumbaniPicha: Reuters/A.A. Dalsh

Katika mechi nyingine, Nigeria iliwaondoa mabingwa watetezi Cameroon. Odion Ighalo alifunga bao katika dakika ya 19. Ilikuwa ni mara ya kwanza ambapo The Indomitable Lions walifungwa bao katika mashindano ya Misri, lakini baada ya kufunga mara mbili katika hatua ya makundi, Cameroon walifunga tena mabao mawili ya harakaharaka katika dakika tatu. Bahoken alisawasisha katika dakika ya 41 na kisha Clinton Njie akawaweka kifua mbele 2 -1

Nigeria walirudi katika kipindi cha pili na kupata bao la pili na la kusawazisha kupitia Ighalo. Sasa amemfikia Sadio Mane wa Senegal na mabao matatu kila mmoja kama wachezaji wenye mabao mengine katika mashindano hayo. Kisha Alex Iwobi akaifungia Nigeria bao la tatu la ushindi katika dakika ya 66. Nigeria sasa watakutana na Afrika Kusini katika robo fainali ya pili.

Madagascar itakabiliana na Congo wakati Algeria ikishuka dimbani na Guinea.