1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Syria yazilaumu nchi za magharibi na Uturuki

Zainab Aziz
12 Novemba 2020

Rais wa Syria Bashar al-Assad amezilaumu nchi za magharibi, na nchi jirani ya Uturuki kwa kuwazuia wakimbizi wa Syria kurejea nyumbani.

https://p.dw.com/p/3lBZR
Russischer Außenminister Lawrow zu Besuch in Syrien
Picha: Foreign Ministry Press Service/AP/picture-alliance

Rais al- Assad alisema hayo kwenye mkutano uliofanyika kwa njia ya video mjini Damascus, kujadili suala la wakimbizi. Mkutano huo ulidhaminiwa na Urusi. Assad amedai kwamba nchi za magharibi zikiongozwa na Marekani pamoja na zile ambazo ni jirani wa Syria na hasa, Uturuki zinabuni mazingira ya kuwafurusha wasyria kutoka kwenye nchi yao ili kupata kisingizio cha kujiingiza katika mambo ya ndani ya nchi yake. Syria: Maelfu wakimbilia kuvuka mpaka wa Ugiriki na Uturuki

Yaliyozungumzwa kwenye mkutano huo

Televisheni ya serikali nchini Syria imeripoti kwamba mkutano huo wa siku mbili umejadili njia za kuwawezesha wakimbizi wa Syria kurejea nyumbani kwa njia salama. Rais al- Assad ameleleza kuwa suala la wakimbizi ni wajibu wa kitaifa na pia ni la wajibu wa kibinadamu. Amesisitiza kwamba Syria inafanya bidii kubwa ili wakimbizi waweze kurudi nyumbani.

Vikwazo 

Nobelpreisträger 2020 | Friedensnobelpreis | UN World Food Programme
Watu waliopoteza makazi yao wakifuata msaada wa chakula katika kambi ya Ain Issa SyriaPicha: Erik De Castro/Reuters

Akizungumzia juu ya vikwazo vilivyowekwa na nchi za magharibi kiongozi huyo wa Syria ameeleza kuwa hatua hiyo inaikosesha Syria nyenzo muhimu zinazohitajika kwa ajili ya kuijenga nchi upya na kusababisha nchi ianguke kiuchumi na hali ya maisha iwe mbaya.

Mnamo mwezi Juni, Marekani iliiwekea Syria vikwazo vipya dhidi ya baadhi ya maafisa wa serikali kama sehemu ya kuishinika serikali ya nchi hiyo kutokana na kukiuka haki za binadamu na kushindwa kufanya mazungumzo juu ya kumaliza vita vya nchini humo. Syria na Uturuki: Hali bado ni ya mvutano mjini Idlib

Watu zaidi ya milioni 12 wamekuwa wakimbizi wa ndani nchini Syria kutokana na vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo vimechukua takriban miaka 10 mamilioni wengine wameikimbia nchi.

Vladimir Putin

Rais wa Urusi Vladimir Putin amesisitiza kwenye mazungumzo na rais al- Assad kwamba ni muhimu kwa wakimbizi zaidi ya milioni 6.5 kurejea nchini Syria ili waweze kuijenga upya nchi yao. Baadhi ya wakimbizi wamesema watakuwa tayari kurejea nyumbani ikiwa usalama utahakikishwa. Na kwa mujibu wa taarifa ya shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR wakimbizi wa Syria 65,000 waliokuwapo nchini Lebanon wamesharejea nchini Syria kwa hiari yao tangu mwaka 2016.

 

Chanzo/DPA