1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Real Madrid mabingwa wa Super Cup ya Uhispania

Bruce Amani
13 Januari 2020

Mashabiki wa kandanda nchini Saudi Arabia walishuhudia fainali ya kukata na shoka ya watani wa jiji la Madrid. Mechi iliyoamuliwa kwa matuta. Madrid waliibuka kidedea na watamshukuru mtu mmoja: Federico Valverde.

https://p.dw.com/p/3W8jm
Saudi-Arabien Supercup-Finale - Real Madrid vs. Atletico Madrid
Picha: picture-alliance/AP Photo/H. Ammar

Kiungo huyo wa Real Madrid alipata pongezi zisizo za kawaida kutoka kwa kocha wa Atletico Madrid Diego Simeone kwa kutafuta kadi nyekundu ya makusudi ambayo iliinyima Atletico nafasi ya kupata bao katika dakika za mwisho na mwishowe kupoteza fainali ya Kombe la Super Cup.

Fainali hiyo, ambayo Real ilishinda 4 -1 kupitia mikwaju ya penalty, matokeo yalikuwa bado ni sifuri kwa sifuri, zikiwa zimesalia dakika tano za muda wa ziada kumalizika wakati mshambuliaji wa Atletico Alvaro Morata alitimka na mpira kuelekea langoni mwa Madrid. Hata hivyo, alipigwa kiatu na Valverde, nje ya eneo la hatari na moja kwa moja akaonyeshwa kadi nyekundu.

Real waliponea dakika zilizobaki za mchezo na kuishia 0 – 0 na wakafunga penalti zao zote na kuwa timu ya kwanza kushinda kombe la Super Cup tangu michuano hiyo ilipobadilishwa kuzishirikisha timu nne na kuhamishiwa Saudi Arabia.

Kocha wa Atleti Simeone alimtuliza Valverde wakati akiondoka uwanjani "kadi nyekundu ya Valvarde, iIlikuwa sehemu muhimu sana ya mchezo, Morata angeweza kufunga bao. Nilimwambia, usiwe na wasiwasi, mtu mwingine yeyote angefanya hivyo tu kama angekuwa katika nafasi yako. Alifanya alichostahili kufanya. Tutaona ni siku ngapi atafungiwa nje.

Cha kushangaza hata zaidi ni kuwa Muuruguary Valverde pamoja na kadi yake nyekundu, alitajwa kuwa mchezaji bora wa fainali hiyo.

Hmm ni muhimu tutambue kuwa kuna kadi nyekundu za kujitafutia ambazo ni za muhimu sana kwenye mchezo….

Valverde mwenyewe alisema alizungumza na Morata baada ya mechi na kumuomba radhi kutokana na kitendo chake. Alimwambia kuwa na hapa namnukuu "Nilichokifanya sio kizuri lakini ndicho nilichoweza tu kufanya. Nna furaha kushinda Kombe lakini nna hisia kidogo za kujutia hilo. Mwisho wa nukuu.

Kocha wa Real Zinedine Zidane aliungana na rais wa klabu Florentino Perez kummiminia sifa Valverde kwa kujitolea mhanga na kuisaidia timu yake kushjinda kombe la kwanza msimu huu. "kitu sawa na hicho kilinikuta nikiwa mchezaji. Kila mara nilijitolea kwa nguvu zote nikiwa uwanjani. Nimeshinda mataji mengi nikiwa mchezaji na hilo linafanyika pia kwangu kama kocha. Lakini kwanza tunapaswa kuwapongeza wachezaji wote, kwa sababu ni wao waliopambana uwanjani. Hii pia ni desturi ya klabu hii